KUTOKANA na hali ya huduma ya
miundombinu ya usafirishaji kuwa duni na ya aghali imeshindwa kukuza
biashara na uchumi katika kiwango kinachotegemewa katika mataifa mengi
ya barani Afrika. Sekta ya huduma ya miundombinu ambayo ni kichocheo
kikubwa katika kukua kwa uchumi imeshindwa kuleta mageuzi ya kutosha.
Taarifa hiyo imebainishwa katika
Ripoti ya UNCTAD ya Maendeleo ya Kiuchumi Barani Afrika ya Mwaka 2015
iliyozinduliwa Jijini Geneva na kusoma katika baadhi ya mataifa ya
Afrika. Akifafanua ripoti hiyo nchini Tanzania, Ofisa Mwandamizi
anayeshughulikia Masuala ya Uchumi UN, Laura Paez alisema huduma za
miundombinu ni muhimu katika kufikia malengo ya maendeleo endelevu
yaliyowekwa na Umoja wa Mataifa kwa ajili ya 2016-2030 na kujenga jukwaa
kwa ajili ya ukuaji mpana barani Afrika.
Alisema katika ripoti hiyo
inayotoa mwangaza wa uchumi wa Afrika imebainisha huduma za miundombinu
kama vile maji na afya zinahusishwa zinahusishwa na malengo muhimu ya
maendeleo endelevu katika kufikia matokeo ya maendeleo ya kijamii na
endelevu. Alisema huduma kama vile umeme, mawasiliano ya simu na usafiri
huchangia katika tija pia huamuwa ushindani wa makampuni ya Afrika.
“Afrika inawakilisha asilimia 15
ya idadi ya watu duniani lakini inatoa asilimia 2.2 tu ya huduma za
mauzo ya nje kimataifa, hali hii inaonesha kutotumika kikamilifu kwa
sekta hiyo,” anafafanua Katibu Mkuu wa UNCTAD Mukhisa Kituyi
akizungumzia ripoti hiyo ya Maendeleo ya Kiuchumi Barani Afrika ya Mwaka
2015.
Aliongeza kuwa ripoti ya Maendeleo
ya Kiuchumi Barani Afrika ya Mwaka 2015 inasisitiza umuhimu wa mataifa
ya Afrika kukabiliana na changamoto za mapungufu mbalimbali katika
udhibiti wa sera, ambayo yamechangia kukosekana kwa ufanisi wa kuweza
kutumia kikamilifu sekta ya huduma kuchochea maendeleo ya kiuchumi.
Ripoti hiyo pia inabainisha kuwa
katika kipindi cha mwaka 2009-2012 sekta ya huduma barani Afrika ilikuwa
kwa kiwango cha asilimia 4.6 ikilinganishwa na asilimia 5.4 katika nchi
zinazoendelea. Sekta ndogo za kihuduma zilizokuwa kwa kasi zaidi
zilikuwa usafiri, uhifadhi na mawasiliano.
Hata hivyo sekta ya huduma katika
Afrika iliongoza ukuwaji wa pato la taifa katika chi 30 kati ya nchi 54
katika kipindi cha 2009-2012, huku kati ya nchi 45 ambapo pato la sehemu
ya huduma lilipanda, 30 zilipata tatizo la kupungua kwa uzalishaji
viwandani kuanzia kipindi cha 2001-2004 hadi kipindi cha 2009-2012.
Aidha alisema baadhi ya nchi za
Afrika zimeendeleza huduma za viwanda vyao kwa mafanikio na hata
zinapeleka huduma zake katika masoko ya Afrika huku akizitaja nchi hizo
kuwa ni pamoja na Mauritius na Nigeria ambapo zinafanya vizuri sekta ya
huduma za kifedha na kibenki. Alisema kibiashara katika sekta ya usafiri
wa anga nchi za Ethiopia, Kenya na Afrika ya Kusini zinafanya vizuri
huku huduma za elimu ni Uganda, huduma za mawasiliano ya simu Misri na
huduma za Bandari ni nchi ya Djibouti na Kenya.
Baada ya ufafanuzi huo ripoti
imeshauri masuala kadhaa ikiwemo kuwa na kanuni ya ufanisi wa huduma ya
miundombinu. Alisema pamoja na hayo mataifa mengi yapo chini katika
uhuru udhibiti sekta zote na mifano ya viwango vya kimataifa vya
udhibiti wa miundombinu havitumiki barani Afrika ilhali vyombo vingi vya
udhibiti vipo katika hatua za awali za maendeleo na bajeti ya kawaida
na mara nyingi hata hukosa wafanyakazi wenye sifa.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com
*Imeandaliwa na www.thehabari.com
Comments