Afisa Habari wa Baraza la Sanaa
la Taifa (BASATA) Aristides Kwizela (Kushoto) akifuatilia burudani
zilizokuwa zikitolewa na watoto wanaondaliwa na Baraza hilo kupitia
programu ya ‘Sanaa kwa Watoto’ wakati wakitumbuiza kwenye Jukwaa la
Sanaa la BASATA mapema wiki hii. Watoto hao wanatoka shule ya Msingi ya
Msimbazi iliyoko Ilala jijini Dar es Salaam. Katikati ni Msanii wa
filamu Honeymoon Mohamed na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti na
Stadi za wasanii Bi. Vick Temu.
Wasanii kutoka Kundi la Ngoma za
Asili na Maigizo la Jivunie lenye makazi yake eneo la Mbagala jijini Dar
es Salaam wakionesha ufundi wao katika kuchenza ngoma za asili kwenye
Jukwaa la Sanaa la BASATA mapema wiki hii.
Katibu Mtendaji wa Baraza la
Sanaa la Taifa (BASATA) Bw. Godfrey Mngereza akitoa ufafanuzi wa masuala
mbalimbali kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA linalofanyika makao makuu
ya Baraza hilo Ilala Sharif Shamba kwa mwezi mara mbili siku za
Jumatatu.
………………………………………………………………….
Na Mwandishi Wetu
Wasanii nchini wametakiwa
kurejesha kwa jamii sehemu ya faida wanayoipata kupitia kazi zao za
Sanaa kwa kuwakumbuka watoto wenye mahitaji maalum ili kujijengea
mtandao wa kudumu wa masoko, uhalali na taswira nzuri kwa jamii.
Wito huo umetolewa mapema wiki
hii na mtengeneza filamu wa Tanzania mwenye makazi yake nchini Marekani
Bi. Honeymoon Mohamed wakati akiwasilisha mada kuhusu Filamu za Kitanzania na Masoko kwenye programu ya Jukwaa la Sanaa inayoandaliwa na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA).
“Wasanii wanaitegemea jamii kama
chanzo cha mapato yao hivyo ni lazima wajenge utamaduni wa kurejesha
kile kidogo wanachokivuna kutoka kwa jamii kupitia kusaidia watu wenye
uhitaji maalum” alisema Honeymoon ambaye filamu yake ya Daddy’s Wedding
imeshinda tuzo kwenye tamasha la kimataifa la filamu la Zanzibar
(ZIFF) lililomalizika hivi karibuni eneo la Ngome Kongwe, Zanzibar.
Aliongeza kwamba watoto wenye
uhitaji maalum wanapata faraja na kuhisi kupendwa na jamii pale
wanapotembelewa mara kwa mara na watu mbalimbali wenye umaarufu na
nafasi kubwa katika jamii hivyo wasanii wetu hawana budi kuwa sehemu ya
kujenga faraja hii kwa watoto hawa.
Kwa mujibu wa Honeymoon wasanii
wa Tanzania wako nyuma katika kuikumbuka jamii hususani kutembelea
makazi ya watoto wenye uhitaji maalumu na kuchangia huduma mbalimbali
zinazokuwa zinahitajika.“Watoto wenye utindio wa ubongo
wako wengi, kuna wale wenye ulemavu wa ngozi na wengine wanaishi wakiwa
yatima kwenye vituo mbalimbali lakini wasanii wetu wamekuwa wazito
kuwakumbuka. Wasanii hawana budi kuyakumbuka makundi haya maana wako kwa
ajili ya jamii” alisisitiza.
Awali kabla ya uwasilishaji wa
mada hiyo, watoto wanaoandaliwa kupitia programu ya BASATA ya ‘Sanaa kwa
Watoto’ kutoka Shule ya Msingi wa Msimbazi iliyopo Ilala jijini Dar es
Salaam walitoa burudani mbalimbali za Sanaa wakisaidiana na Kikundi cha
Sanaa cha Jivunie chenye maskani yake neo la Mbagala Manispaa ya Temeke.
Comments