MAHAKAMA YA TANZANIA INAKUSUDIA KUONGEZA IDADI YA MAJAJI KATIKA KANDA YAKE YA MWANZA


 
Na Lydia Churi- Mwanza
Mahakama ya Tanzania inakusudia kuongeza idadi ya Majaji katika kanda yake ya Mwanza ili kuongeza msukumo wa kumaliza kesi za mauaji kutokana na kanda hiyo kuongoza kwa kuwa na kesi nyingi za mauaji nchi nzima.
Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli za kimahakama katika kanda ya Mwanza, Jaji Mkuu wa Tanzania Mheshimiwa Mohamed Chande Othman amesema ataongeza idadi ya majaji katika kanda hiyo ili kesi hizo za mauaji zimalizike kwa wakati.
Jaji Mkuu pia ameiagiza Mahakama Kuu kanda ya Mwanza kuzipa msukumo maalum kesi za mauaji ili kuhakikisha zinamalizika mapema na kupunguza mlundikano wa kesi katika mahakama za Tanzania.
Awali akisoma taaarifa ya hali halisi ya kesi katika Mahakama Kuu kanda ya Mwanza, Jaji Mfawidhi wa kanda hiyo Mheshimiwa Robert Makaramba alisema kanda ya Mwanza ndiyo inayoongoza kwa kuwa na kesi nyingi za mauaji nchini ambapo hadi kufikia Aprili mwaka huu kuna jumla ya kesi 512 za mauaji.
Pamoja na mkakati wa Jaji Mkuu kuongeza idadi ya Majaji ili kumaliza kesi hizo, Jaji Mfawidhi wa kanda ya Mwanza alisema wameshachambua kesi hizo za mauaji ambapo Jaji Kiongozi pia aliahidi kuwaongezea jumla ya Majaji 11 ili waweze kusaidia kusukuma kesi hizo.
Jaji Makaramba alisema kati ya mwezi Juni na Julai jumla ya vikao 11 vinatarajiwa kukaa ili kusikiliza kesi 123 zilizopangwa kusikilizwa. Alisema kati ya kesi hizo, 35 ni zile zitakazosikilizwa kwa mara ya kwanza na kesi 88 ni zile zitakazosikilizwa mpaka mwisho.
Alisema endapo vikao hivyo vitafanyika kama ilivyokusudiwa vitasaidia kupunguza kesi zilizopo mahakamani kwa miaka mingi.
Hadi kufikia mwezi April mwaka huu, Mahakama Kuu kanda ya Mwanza ina jumla ya kesi 2771 za aina zote zikiwemo zile za Madai ya kawaida, Madai ya Ardhi na za jinai. Ili kuongeza kasi ya usikilizwaji wa kesi hizo, kila Jaji amepangiwa kusikiliza kesi 346. Kanda hiyo ina Majaji nane (8).
Jaji Mkuu wa Tanzania ameanza ziara katika kanda ya Mwanza inayohusisha mikoa ya Geita, Mwanza na Mara ambapo atakagua shughuli mbalimbali za kimahakama katika kanda hiyo.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA