Na MatukiodaimaBlog
MADAWATI 745 ambayo yalitengenezwa na mfuko wa jimbo la Kilolo kwa gharama ya Tsh milioni 30 zilizotolewa na mbunge wa jimbo hilo Venance Mwamoto ambayo yalikataliwa na mbunge huyo na mkuu wa mkoa wa Iringa Amina Masenza yamekamilika kutengenezwa kwa ubora .
Akizungumza baada ya kukabidhiwa madawati hayo leo mbunge Mwamoto alisema kuwa amekubali kupokea madawati hayo baada ya kufurahishwa na ubora wake na hivyo imani yake kuona walimu wanasimamia utunzaji wa madawati hayo ili kuondokana na kero tena ya madawati katika shule zote za wilaya ya Kilolo.
Mbunge Mwamoto alisema kuwa kufuatia uhaba wa madawati uliyokuwa ukiikumba wilaya ya Kilolo na kama sehemu ya utekelezaji wa agizo la Rais Dr John Magufuli alilazimika kuidhinisha pesa kiasi cha Tsh milioni 30 kutoka mfuko wa jimbo la Kilolo ili kuweza kusaidia utengenezaji wa madawati 300 japo Halmashauri ya Kilolo kupitia wadau wake wa ndani na makusanyo ya ndani waliweza kuongeza kiasi cha Tsh milioni 19 na kufanya kuwepo kwa kiasi cha pesa cha Tsh milioni 49 ambazo zilifanikisha kutengeneza madawati zaidi ya 1000 .
Alisema kuwa pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Halmashauri hiyo katika kushughulikia kero ya madawati katika wilaya hiyo ya Kilolo ila mafundi ambao walipewa kazi ya kutengeneza madawati hayo hawakuwa wazuri kutokana na kushindwa kuifanya kazi hiyo kwa ubora uliotakiwa hivyo kupelekea kufanya kazi hiyo kwa kiwango cha chini zaidi.
"Nililazimika kukataa madawati 40 ambayo yalipelekwa shule ya Msingi Nyanzwa na Igunda baada ya kuyaona hayana ubora na wananchi kulalamika kuwa ni mabovu ukilinganisha na madawati ambayo yalitengenezwa kwa nguvu ya wananchi katika vijiji hivyo ......hivyo sikuwa tayari kupokea madawati hayo hali iliyopelekea mkuu wa mkoa wa Iringa kufika kuona madawati hayo na kulazimika kuyakataa madawati yote 745 kwa kutaka yatengenezwe kwa ubora"
Mwamoto alisema kuwa amefurahishwa na usimamizi mzuri wa mkuu wa wilaya ya Kilolo na timu yake ya mkurugenzi wa wataalam wengine ambao wameweza kuifanya kazi hiyo ya kusimamia ubora kwa muda mfupi wa wiki tatu kinyume na muda ule wa mwezi mmoja uliotolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa .
Hata hivyo Mwamoto alisema kuwa yawezekana wapo watendaji ambao walimchukia kwa yeye kukataa madawati hayo ila ukweli alifanya hivyo kusaidia watoto wa wana Kilolo kutoendelea kukaa chini na kuwa iwapo madawati hayo yangepelekwa shuleni bado wananchi wangebeba dhamana ya kuendelea kuchangishana kwa ajili ya kuchonga madawati.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kilolo Asia Abdalah alisema kuwa baada ya mkuu wa mkoa wa Iringa kumpa agizo la kusimamia zoezi hilo ndani ya mwezi mmoja alilazimika kuifanya kazi hiyo kwa haraka zaidi ndani ya wiki tatu ili kuona wanafunzi wote wanakaa kwenye madawati .
Alisema kuwa timu ya wakuu wa idaraka katika wilaya ya Kilolo wameonyesha ushirikiano mkubwa katika kutekeleza agizo hilo na kuwa baadhi yao walikuwa wanalala kwenye karakana zilizopewa kazi ya kutengeneza madawati hayo mapema kabla ya muda waliopewa na mkuu wa mkoa wa Iringa .
Wakati mkuu wa mkoa wa Iringa Bi Masenza pamoja na kumpongeza mkuu wa wilaya ya Kilolo na timu yake kwa kutekeleza zoezi la usimamiaji wa ubora wa madawati hayo bado alimpongeza mbunge wa Kilolo Bw Mwamoto kwa kubaini suala hilo huku akiwataka walimu katika shule zote kuhakikisha wanatunza madawati hayo ili kuondokana na adha ya kuchangia madawati mara kwa mara .
" Nimeridhishwa na ubora wa madawati hayo na yale machache ambayo yalipelekwa mashuleni wanaendelea kuyarekebisha ili yaweze kufanana na haya ambayo kweli yapo katika ubora mzuri "
TAZAMA VIDEO CHINI
|
Comments