Mwenyekiti kutoka Taasisi ya Daima Associates Ltd, Profesa Samuel Wangwe (kushoto) akibadilishana mawazo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa kabla ya kuanza kwa mkutano wa Nishati kwa Ukuaji wa Uchumi ulioshirikisha wadau wa nishati kwa ajili ya kujadili utafiti wa sekta ya nishati unaotarajiwa kufanyika nchini miaka mitano ijayo.
Mwenyekiti kutoka Taasisi ya Daima Associates Ltd, Profesa Samuel Wangwe akielezea Mpango wa Nishati kwa Ukuaji wa Uchumi kabla ya kumkaribisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa (hayupo pichani) kwenye mkutano uliokutanisha wadau wa nishati jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa (kulia) na washiriki wengine wakifuatilia mada iliyokuwa inawakilishwa na Profesa Catherine Wolfram kutoka Chuo Kikuu cha California, Berkeley (hayupo pichani) katika mkutano huo.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa akizungumza mbele ya washiriki kwenye ufunguzi wa mkutano wa Nishati kwa Ukuaji wa Uchumi ulioshirikisha wadau wa nishati kwa ajili ya kujadili utafiti wa sekta ya nishati unaotarajiwa kufanyika nchini miaka mitano ijayo.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa (mbele) akifungua mkutano wa Nishati kwa Ukuaji wa Uchumi ulioshirikisha wadau wa nishati kwa ajili ya kujadili utafiti wa sekta ya nishati unaotarajiwa kufanyika nchini miaka mitano ijayo.
Profesa Catherine Wolfram kutoka Chuo Kikuu cha California, Berkeley akielezea changamoto za sekta ya nishati Afrika Mashariki katika mkutano huo.
……………………………………………………………………………………………..
Na Greyson Mwase,
Imeelezwa kuwa nishati ya umeme inatarajia kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi kupitia kuongezeka kwa uwekezaji kwenye viwanda.
Hayo yalielezwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Profesa Justin Ntalikwa wakati akisoma hotuba ya ufunguzi kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo kwenye mkutano wa Nishati kwa Ukuaji wa Uchumi uliokutanisha wadau mbalimbali wa nishati kwa ajili ya kujadili utafiti kuhusu sekta ya nishati unaotarajiwa kufanyika kwa kipindi cha miaka mitano ijayo kuanzia sasa nchini Tanzania.
Mkutano huo uliofanyika jijini Dar es Salaam uliandaliwa na Kituo cha Usimamizi wa Sera cha Oxford kwa kushirikiana na Shirika la Misaada la Uingereza, na wawekezaji binafsi katika sekta ya nishati nchini.
Profesa Ntalikwa alisema Serikali imeweka mikakati katika kuhakikisha kuwa umeme wa uhakika unapatikana kwa gharama nafuu na hivyo kuinua uchumi wa mwananchi mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.
Akielezea historia ya uzalishaji wa umeme nchini, Profesa Ntalikwa alisema kuwa mwaka 2005 ni asilimia 10 tu ya wananchi walikuwa wanapata umeme hali iliyopelekea Serikali kuweka mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na uanzishwaji wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wenye jukumu la kusimamia miradi yote ya usambazaji wa umeme vijijini.
Aliendelea kusema hadi sasa ni asilimia 40 ya wananchi wanapata umeme na kusisitiza kuwa bado serikali imeendelea kuweka mikakati ya matumizi ya vyanzo vya nishati ili kuzalisha umeme wa uhakika.
Alitaja mikakati mingine kuwa ni pamoja na uanzishwaji wa miradi ya uzalishaji umeme kwa njia ya gesi ikiwa ni pamoja na upanuzi wa kituo cha Kinyerezi I (Megawati 185), Kinyerezi II (Megawati 240), Kinyerezi III ( Megawati 300) na Kinyerezi IV (Megawati 330) ambacho kiko katika hatua ya mwisho ya maandalizi yake.
Aliendelea kutaja miradi mingine kuwa ni pamoja na ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi cha Somanga Fungu (Megawati 320) ambapo wawekezaji wanahitajika na kituo cha Mtwara (Megawati 600) ambapo upembuzi yakinifu unaendelea bado
Alitaja miradi mingine kuwa ni pamoja na mradi wa umeme wa upepo wa Singida (Megawati 100), Mradi wa Kuzalisha Umeme kwa Kutumia Makaa ya Mawe wa Kiwira ( Megawati 200) unaomilikiwa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ambapo mbia anakaribishwa kuendeleza mradi huo.
“Kuna mradi wa makaa ya mawe wa Mchuchuma (Megawati 400) na Ngaka (Megawati 200) chini ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) ambapo wawekezaji wanakaribishwa,” alisema Profesa Ntalikwa
Alisema Tanzania ina vyanzo vingi vya nishati ya umeme ikiwa ni pamoja na gesi, maji, upepo, jotoardhi, makaa ya mawe na kuwakaribisha wawekezaji kwa ajili ya kuchangamkia fursa zilizopo
Comments