Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aongoza ujumbe wa Tanzania kwenye kikao cha 25 cha Wakuu wa Nchi wanaoshiriki kwenye mchakato wa APRM


Mheshimiwa Kasim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Tanzania, aliongoza ujumbe wa Tanzania kwenye kikao cha 25 cha Wakuu wa Nchi wanaoshiriki kwenye mchakato wa APRM. Pia walikuwepo Mheshimiwa Dkt Susan Kolimba, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mheshimiwa Dkt. Khalid S. Mohamed, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. 
Kikao hicho kilifanyika mjini Nairobi, Kenya; kuanzia tarehe 21-26 Agosti 2016 na kilihudhuriwa na jumla ya Wakuu wa Nchi 22. 

APRM ni Mpango wa Kujitathmini Ki-Utawala Bora uliobuniwa na Wakuu wa Nchi za Kiafrika mwanzoni mwa miaka ya 2000, ili kutatua changamoto za utawala bora zinazolikabili bara la Afrika. Tanzania ni miongoni mwa nchi 35 zinazoshiriki kwenye Mpango huu. 

Kauli mbiu ya kikao hiki ni “kuwa na APRM Imara itakayosaidia kuleta Mabadiliko katika Uongozi barani Afrika” na hivyo kuendelea kuwa chombo kitakachosaidia katika kufikiwa kwa malengo ya Umoja wa Afrika (Agenda 2063) na Malengo Endelevu ya Maendeleo ya Umoja wa mataifa. 

Kwa mara ya kwanza katika historia ya kuanzishwa kwa Mpango huu, APRM ilipata muda wa siku takriban sita za kuangazia kwa kina masuala mbalimbali ambayo ni pamoja na Ripoti za Tathmini za nchi za Djibouti na Chad, Ripoti ya utekelezaji wa Mpango kazi wa Nchi ya Msumbiji, Mpango Mkakati wa APRM 2016-2020, Mpango Kazi na Bajeti kwa mwaka 2016/17, Masuala mbalimbali yanayohusu utendaji wa Jopo la Watu Mashuhuri, Hati ya Kuinganisha APRM kama Taasisi ndani ya Umoja wa nchi huru za Kiafrika, Taarifa ya Mkaguzi wa Mahesabu ya APRM, Vianzio vya Fedha na Maeneo ya changamoto yanayopendekezwa kuingizwa kwenye Hojaji Kuu ya APRM pamoja na kuzingatiwa kwenye mbinu za tathmini y utawala bora kwa vipindi vijavyo. 


Maeneo mtambuka katika Afrika yaliyoonekana kuhitaji mikakati endelevu ya pamoja katika kuyatafutia ufumbuzi ni pamoja na; Minyukano ya kimtazamo hasa juu ya itikadi, sekta binafsi kutowezeshwa vya kutosha, miundo mbinu duni ikiwa nia pamoja na nishati, barabara, reli, simu, mitandao ya mawasiliano n.k, dola zisizokuwa imara, changamoto zihusuzo masoko, ukosefu wa viwanda pamoja na usindikaji wa bidhaa usiyoridhisha, uhaba wa wataalam, maendeleo duni katika sekta ya kilimo, maendeleo duni katika sekta ya huduma ikiwa ni pamoja na benki, bima, utalii n.k, udhaifu kwenye mifumo ya kidemokrasia na udhaifu wa uwajibikaji katika sekta ya umma. Baada ya mjadala wa kina kuhusu maeneo yaliyotajwa hapo juu, ilikubalika kuwa, Hojaji Kuu ya APRM pamoja na mbinu za tathmini zifanyiwe marekebisho ili kulenga zaidi mambo hayo muhimu na hatimaye kuungezea mchakato wa APRM thamani zaidi. 

Tanzania inaendelea kutekeleza Mpango kazi wa APRM kwa kushirikiana na Wizara, Idara na Wakala za Serikali, pamoja na kuishirikisha Sekta Binafsi.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.