BMT YASEMA HAITAMBUI YANGA KUKODISHWA


Na Mahmoud Zubeiry, DAR ES SALAAM
BARAZA la Michezo la Taifa (BMT) limesema kwamba halitambui klabu ya Yanga SC kukodishwa kwa kampuni ya Yanga Yetu, kwa kuwa taratibu haazikufuatwa na Baraza la Wadhamini la klabu hiyo halitambuliki.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Katibu wa BMT, Mohammed Kiganja amesema kwamba wao wanaendelea kutambua kama Yanga SC ni mali ya klabu na haijakodishwa kwa kampuni ya Yanga Yetu.
Kiganja amesema kwamba, taratibu hazikifuatwa katika mchakato mzima ulioifikisha Yanga SC kwenye kukodishwa, hivyo zoezi hilo ni batili.
“Hatupingi klabu zetu kufanya mabadiliko isipokuwa tunajaribu kuwakumbusha kufuata utaratibu wa kisheria na katiba zao. Kwa sababu unapobadilisha jina au kufanya marekebisho yoyote, ni lazima vikasajiliwe na kutambulika,”amesema.
Aidha, Kiganja amesema hata Baraza la Wadhamini wa Yanga lilipitisha uamuzi wa kuikodisha timu, haitambuliki kwa Msajili wa Vyama na Klabu na Michezo wa BMT, kwa Wajumbe wake wengi ni wa muda.
Amesema kati ya Wajumbe wa Baraza la Wadhamini la Yanga lililoundwa Julai 5, mwaka 1973 ni wawili tu wanaotambulika na walio hai hadi sasa, ambao ni Dk. Jabir Idrisa Katundu na Juma Mwambelo, wakati wengine wamekwishafariki dunia. 
“Mwembelo pamoja na kwamba bado yupo hai, lakini kwa muda sasa hahusishwi tena mambo yanayoendelea ya klabu hiyo,” amesema.
Kiganja amewataja Wajumbe wengine wa Baraza hilo la Muda, ambalo halikuwahi kusajiliwa wala kupitishwa kwenye Mkutano Mkuu ni Kapteni Mstaafu, George Mkuchika, Mama Fatuma Karume, Francis Kifukwe, Amri Ramadhan, Juma Kambi na Abeid Mohammed.
Na akasema ili Yanga ikodishwe, inazotakiwa kwanza kifanyike kikao cha Kamati ya Utendaji itakayochambua hoja na kukubaliana au kutokukubaliana kabla ya kwenda kwenye Mkutano Mkuu wa wanachama, uwe wa dharura au kawaida na maamuzi yatakayofikiwa katika Mkutano yatapelekwa Baraza la Wadhamini, ambalo ndilo litawasilisha suala hilo kwa Msajili.
“Sheria ya BMT ya mwaka 1967 kifungu namba 11 (1) kinasema chama chochote kinachofanya mabadiliko ya jina, anuani, madhumuni au kifungu chochote cha katiba yake kitatakiwa idhini ya Msajili. Kifungu namba 11 (3) Msajili anaweza kuyakataa maombi ya kubadili kifungu chochote cha Katiba kama ataona kuwa mabadiliko yanaweza kuhatarisha usalama na kuvuruga amani, au kama kuna malengo ya kuwanufaisha wachache au kama hayazingatii sera za michezo na sheria za BMT,” amesema Kiganja.
Katibu huyo wa BMT amesema kwamba mchakato huo wa Yanga kukodishwa ungekuwa halali tu kama taratibu hizo zingefuatwa na kupita kote.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI