JAMHURI
YA MUUNGANO WA TANZANIA
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU
Simu:
255-22-2114512, 2116898
E-mail: press@ikulu.go.tz
Faksi: 255-22-2113425
|
OFISI YA RAIS,
IKULU,
1 BARABARA YA BARACK
OBAMA,
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
|
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Jamhuri
ya Zambia Mhe. Edgar Chagwa Lungu leo tarehe 28 Novemba, 2016 wamekubaliana
kuchukua hatua za haraka na madhubuti kuboresha utendaji kazi wa reli ya TAZARA
na bomba la mafuta la TAZAMA ili miradi hiyo miwili ilete manufaa
yaliyokusudiwa kwa wananchi Tanzania na Zambia.
Marais
hao wametangaza kuchukua hatua hizo Ikulu Jijini Dar es Salaam katika mkutano
na waandishi wa habari uliofanyika muda mfupi baada viongozi hao kufanya
mazungumzo rasmi ikiwa ni sehemu ya ziara ya siku 3 ya Rais Lungu iliyoanza
jana hapa nchini kwa mwaliko wa Rais Magufuli.
Katika
mkutano huo uliorushwa moja kwa moja na vyombo vya habari vya redio, tevisheni
na mitandao ya kijamii Rais Magufuli ameelezea kusikitishwa kwake na kuzorota
kwa utendaji kazi wa reli ya TAZARA ambao umeshuka kutoka usafirishaji wa tani
5,000,000 za mizigo mwaka 1976 hadi kufikia usafirishaji wa tani 128,000 kwa
mwaka hivi sasa, huku utendaji kazi wa bomba la mafuta la TAZAMA nao
ukiporomoka kutoka uwezo wake wa kusafirisha tani 1,100,000 za mafuta hadi
kufikia tani 600,000 kwa mwaka hivi sasa.
Marais
hao wamekubaliana kuwakutanisha wanasheria wakuu wa Serikali za nchi zote mbili
haraka iwezekanavyo kwa lengo la kufanya marekebisho ya kisheria kwa maeneo
yote yaliyoonesha kuwa kikwazo na pia kupanga upya menejimenti za TAZARA na
TAZAMA ili ziweze kuendesha vyombo hivyo kibiashara na kwa manufaa
yaliyokusudiwa wakati vilipoanzishwa na Waasisi wa mataifa haya mawili yaani
Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wa Tanzania na Mhe. Dkt. Kenneth Kaunda
wa Zambia.
"Tumekubaliana
ni lazima tubadilike na tubadilike kwa haraka, vikwazo vinavyotokana na sheria
viondolewe na manejimenti ya TAZARA ipangwe upya, na mimi nataka kusema kwa
uwazi, ukiwauliza TAZARA watakwambia tatizo ni mtaji lakini ukweli ni kwamba
tatizo ni menejimenti, ingekuwa tatizo ni mtaji, ule uliokuwepo mwaka 1976 umekwenda
wapi? maana sasa hivi TAZARA ina vichwa 14 tu vya kuendeshea treni na ina
upungufu mkubwa wa mabehewa"
amesema Rais Magufuli.
Kwa
upande wake Rais Lungu amesisitiza kuwa katika kuimarisha TAZARA wamekubaliana
kuweka pembeni siasa na kuirejesha TAZARA katika hali yake ya kibiashara kwa
kuhakikisha inafanya kazi ya kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo
iendayo kusini mwa Tanzania na nchini Zambia.
Mhe.
Lungu ameongeza kuwa pamoja na kuimarisha bomba la mafuta la TAZAMA, Zambia
inatarajia kunufaika na gesi iliyogunduliwa kwa kiasi kikubwa nchini Tanzania
na pia inajipanga kutumia vizuri fursa ya kufunguka kwa ukanda wa maendeleo wa
Mtwara (Mtwara Corridor) na mpango wa
ujenzi wa reli ya kati ambapo ukanda wa Kaskazini mwa Zambia una mawasiliano ya
karibu na bonde la ziwa Tanganyika.
"Mhe. Rais Magufuli
una muda wa kutosha katika uongozi wako na mimi nina muda wa kutosha pia, kwa
hiyo kwa pamoja tunaweza kuimarisha maeneo yote ya kuinua biashara na uwekezaji
kati ya nchi zetu mbili ikiwemo kuimarisha TAZARA
na
TAZAMA kwa manufaa ya wananchi wetu" amesisitiza
Rais Lungu.
Kuhusu
hali ya biashara kati ya Tanzania na Zambia, Rais Magufuli amesema Zambia ni
nchi inayoongoza kwa kupitisha mizigo mingi katika bandari ya Dar es Salaam
ambapo katika mwaka 2015 mizigo yenye uzito wa tani Milioni 1.9 ilipitishwa na
kwamba kumekuwa na ongezeko la biashara kati ya Zambia na Tanzania kutoka
Shilingi Bilioni 89.2 mwaka 2010 hadi kufikia Shilingi Bilioni 152.2 mwaka
2015.
Dkt.
Magufuli amemhakikishia Rais Lungu kuwa Tanzania inaendelea kuboresha mazingira
ya kufanyia biashara ikiwa ni pamoja na kuboresha zaidi bandari ya Dar es
Salaam, kupunguza vizuizi vya barabarani kutoka 8 hadi 4, kushughulikia tatizo
la vizuizi vya polisi na kujenga Kituo cha Pamoja
cha Utoaji wa Huduma za Mpakani (One Stop
Border Post)
"Tunataka
mambo haya yote yaende haraka, wataalamu wetu ni lazima waharakishe kurekebisha
vikwazo vyote vilivyokuwa vinatuchelewa, tufanye kazi pamoja kwa manufaa ya
wananchi" amesisitiza Rais
Magufuli.
Jioni
ya leo Rais Edgar Chagwa Lungu anatarajiwa kuhudhuria dhifa ya kitaifa aliyoandaliwa
na Mwenyeji wake Rais John Pombe Magufuli Ikulu Jijini Dar es Salaam na kesho
Rais Lungu anatarajiwa kumaliza ziara yake ya siku 3 hapa nchini.
Gerson
Msigwa
Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar
es Salaam
2
Comments