Na Richard Mwaikenda
WABUNGE wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wamesimama kwa dakika moja kuomboleza kifo cha Spika mstaafu wa bunge hilo, Samuel Sitta aliyefariki dunia alfajiri ya leo nchini Ujerumani.
Taarifa za msiba huo mkubwa, imetangazwa na Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu leo asubuhi wakati wa kikao cha Bunge mjini Dodoma.
Zungu alisema kuwa Sitta ambaye pia ni Spika Mstaafu wa Bunge la Katiba, amepatwa na mauti saa 7 mchana kwa saa za Ujerumani ambayo sawa na saa 10 alfajiri kwa saa za hapa Tanzania.
Alisema kuwa Sitta aliondoka nchini kwenda Ujerumani kwa matibabu Novemba 3, mwaka huu ambako matibabu yote yalikuwa yanagharamiwa na serikali.
Kwa niaba ya Bunge, alitoa salamu za rambirambi kwa familia ya marehemu Sitta na kwa mkewe, Margareth Sitta ambaye ni Mbunge wa Urambo.
Aliwaahidi wabunge kuwa watakuwa wanapewa taarifa za msiba huo kadri watakavyokuwa wanazipata.
Rais John Magufuli (kulia) akimjulia hali Spika mstaafu, Samuel Sitta miezi michache iliyopita nyumbani kwake Dar es Salaam.
Sitta enzi zake akijadiliana jambo na aliyekuwa mjumbe mwenzie wa Halmashauri Kuu ya CCM, ambaye sasa amehamia Chadema, Edward Lowassa
Comments