Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha
CHAMA cha waandishi wa habari mkoani Pwani, (CRPC)kimeelezea kusikitishwa na kitendo kinachodaiwa kufanywa na mkuu wa wilaya ya Kibaha Assumpter Mshama, cha kumdhalilisha mwandishi wa habari katika mkutano wa hadhara eneo la Mailmoja.
Mkuu wa wilaya huyo alifanya kitendo hicho novemba 29 mwaka huu,baada ya mwandishi huyo wa gazeti moja la kila siku nchini kutoa habari ya agizo la zoezi la usafi Kibaha kupuuzwa.
Akitoa tamko hilo mbele ya wanachama wa chama hicho,mwenyekiti wa CRCP, Ally Hengo,alisema chama kimesikitishwa kwani mkuu wa wilaya alipaswa kumuita ofisini na kumuonya kama aliona kuna kosa kuliko kumsuta hadharani .
Alielezea kuwa ,Assumpter alimwita mwandishi huyo wa habari na kuanza kumsuta kwa kumtolea maneno makali huku akiwashirikisha baadhi ya wafanyabiashara kumsakama.
"Kamtia aibu ,kamfedhehesha na pia akumbuke tasnia hii inamhimili wake,kwahiyo kukumbushwa wajibu wake wa kusimamia maagizo ya mkuu wa mkoa ama raisi sio kosa bali alitakiwa kuyafanyia kazi" alisema Hengo.
Hengo alisema kutokana na tukio hilo uongozi na wanachama wa klabu ya waandishi wa habari mkoa imekutana na kulaani kitendo hicho.
Chama kimemtaka aombe radhi kwa mwandishi huyo ndani ya siku saba na kama hatofanya hivyo waandishi wa mkoa huo watalazimika kususia shughuli zake atakazokuwa akifanya.
Hata hivyo Hengo alisema chama kimekubalina kwamba nae mwenyekiti wa soko la Mailmoja Ramadhani Ngowo ,kuomba radhi ndani ya muda huo kwa kudaiwa kumshurutisha mwandishi huyo kupiga magoti hadharani.
Alitoa wito kwa viongozi kuacha kutumia njia za ubabe na udhalilishaji na badala yake watumie vyama vya wanahabari mikoani na kamati za maadili za chama hivyo ama kumpa onyo faragha mhusika.
Kwa upande wake mwandishi huyo anaedaiwa kudhalilishwa (Sanjito Msafiri) alisema kuwa mnamo novemba 29 alipigiwa simu na kisha kuitwa kwenye mkutano wa hadhara na mkuu huyo.
Alifafanua kuwa baada ya kufika mkutanoni ndipo alipokutana na kushambuliwa kwa maneno ,na kuitwa mbele ya meza kuu na kushinikizwa aombe radhi umati wote kwa kuandika habari hiyo.
"Nilikataa kuomba msamaha kwake na kwa wananchi kwa kuwa nilikuwa najua naamini nilichokiandika kipo sawa ,na hata yeye kama ni mkuu wa serikali hawezi kunilazimisha kuomba msamaha watu kwa kuingilia majukumu yangu"
"Nimefanya nae kazi nyingi sana huyu mama,hata hawa wafanyabishara lakini nashangaa kwa hili kubadilika na kugeuka mbogo" alisema .
Mwandishi huyo ,aliwaomba viongozi mbalimbali kuheshimu kazi ya uandishi wa habari bila kuwadharau waandishi wakati kwenye mambo yao huwa wakiwakimbilia.
Alimwambia Assumpter kuwa hana tatizo na yeye na bado anamuheshimu licha ya kumkosea .
Alimtaka mwenyekiti wa soko la Mailmoja ,Ramadhani Ngowo kujitambua na kuacha kukurupuka katika mambo yasiyomuhusu.
Nao baadhi ya waandishi wa habari mkoani hapo ,akiwemo Julieth Piniel,Gustafu Haule ,Margareth Malisa na Ben Komba walieleza kwamba wapo baadhi ya viongozi ambao wanawadharau waandishi wa habari .
Walisema tasnia hiyo ni muhimu na imeshawavusha wengi kufika walipo sasa hivyo kuna kila sababu ya kuheshimiana na kuwekeana mipaka.
Gustafu alisema amesikitishwa na kitendo kilichotokea ,kinaonyesha udhalilishaji na hofu ya utawala ambayo husababisha viongozi wasiojiamini kukurupuka.
Katika toleo la gazeti hilo novemba 29 mwaka huu kuliandikwa kuwa agizo la mheshimiwa rais la kufanya usafi kila mwezi kwasasa wilayani Kibaha linaonekana kutozingatiwa kutokana na kigezo cha kulipa faini .
Mbali ya hilo wananchi wengi wamekuwa wakisubiri saa nne ifike asubuhi ndio wanatoka majumbani suala ambalo wilaya hiyo inatakiwa kulisimamia .
Mwisho
Comments