Mbunge wa Jimbo la Rufiji, Mohamed Mchengerwa (katikati) akiangalia daraja lililojengwa kuelekea lilipopita bomba la gesi wilayani humo na kukiita kitendo hicho kuwa ni uhujumu uchumi.
Na Mwandishi Wetu,Rufiji
MBUNGE wa Rufiji Mohammed Mchengerwa amesikitishwa na kitendo cha Wakala wa Barabara Nchini(Tanroads) mkoa wa Pwani kuhusika kutoa kibali kwa Taasisi ya Walemavu ili kuvunja daraja lililojengwa kuelekea lilipopita bomba la gesi wilayani humo na kukukiita kitendo hicho kuwa ni uhujumu uchumi.
Daraja hilo lililojengwa katika kijiji cha Umwe Kusini kwa msaada wa serikali ya China kwa gharama ya zaidi ya Sh bilioni moja lilivunjwa Novemba 28 mwaka jana na kusababisha wananchi kushindwa kuvuka kwenda katika eneo la lililopo bomba la gesi.
Akiwa katika eneo hilo Mchengerwa alikabidhiwa barua iliyotolewa na Tanroads Mkoani hapo kama kibali cha cha kuchukua chuma chakavu /makalvati mabovu
Akisoma barua hiyo mbele ya wananchi wa eneo hilo Mchengerwa alisema, barua hiyo iliyosainiwa na aliyekuwa Meneja wa Tanroads mkoani humo Mhandisi Tumaini Sarakikya ilichangia kubomolewa kwa daraja hilo baada ya meneja huyo kuagiza kutafutwa kwa vyuma chakavu katika barabara za wakala huo.
" Kwa mujibu wa barua iliyoandikwa Agosti tatu Mwaka 2016 iliyosainiwa na Meneja wa Tanroads mkoani hapa Mhandisi Sarakikya yenye kumbukumbu namba TRD /CR/R 10 -20/01/VOL.111/177 ilielekeza kutafutwa vyuma chakavu katika barabara zilizopo chini ya Wakala huo lakini sio za Halmashauri kama ambavyo imefanyika katika eneo hilo,"alisema Mchengerwa.
Alisema aina hiyo ya uharibifu wa miundombinu wa namna hiyo haukubaliki na kufananisha tukio hilo na uhujumu uchumi ambao hauvumiliki.
"Hii ni kesi ha uhujumu uchumi kwasababu ni uharibifu wa mindombinu , thamani ya uharibifu wa mali hii inafaa watu hawa kupelekwa katika mahakama ya mafisadi watu wamekuja kuvunja daraja ambalo tulipata msaada wa zaidi ya bilioni moja kwanini tunarudishwa nyuma? Kwa sasa watu wanaokwenda lilipo bomba la gesi hawawezi kwenda njia hakuna"alisema Mchengerwa
Hata hivyo Mbunge huyo alieleza kuwa amezungumza na Kaimu Meneja wa Tanroads Mkoani hapo ,Mhandisi Yudas Msangi ambaye ameeleza kutofahamu jambo hilo na hajawahi kuhusika kutoa kibali hicho .
Msangi aliahidi kufuatilia jambo hilo akieleza kuwa huenda kuna watendaji wa ofisi yake wasio waaminifu ambao wanashirikiana na watu wengine kufanya hujuma hizo.
Hata hivyo pamoja na Msangi kukataa kutofahamu jambo hilo juzi Maafisa waliojitambulisha kuwa wanatoka Tanroads walifika katika eneo hilo wakiomba ushirikiano kutoka kwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)Wilaya ya Rufiji,Mussa Mnyeresa, ili kuangalia namna uharibifu uliotokea.
Akizungumzia suala hilo Mnyeresa alisema"Hawa watu waliojitambulisha wanatoka Tanroads ni feki lakini nashangaa wanatumia gari la Wakala huo wakati huo Kaimu Meneja anadai hana taarifa hatuelewi hawa watu wanatuchanganya,"
Mnyeresa alionyesha wasiwasi wake na Mwenyekiti wa Kijiji hicho,Juma Libela na Mtendaji Kata ya Umwe Mkumba Amani kwamba wamehusika na uharibifu huo kwakuwa hata baada ya uharibifu huo walipigiwa simu ila hawakutaka kutoa ushirikiano na badala yake waliwakamata watu ambao ni vibarua lakini wahusika wakuu hawajawakamata.
Mwisho
Comments