BODI YA MIKOPO YAIAGIZA DRAGON KUWASILISHA MAJINA YA WAAJIRIWA 200

Hussein Ndubikile

BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini (Heslb) imeiagiza Kampuni ya Uzalishaji Mabati na Usafirishaji ya Dragon kuwasilisha majina ya wafanyakazi 200 ili iweze kuwabaini wanufaika wanaotakiwa kuanza kurejesha fedha za mikopo.

Mwaka jana bodi hiyo ilitangaza mabadiliko ya sheria mpya ya urejeshaji wa mikopo iliyopitishwa na Bunge ambapo wanufaika walioko kwenye ajira rasmi wanatakiwa kukatwa asilimia 15 ya mishahara yao huku wasio kwenye ajira rasmi wakitakiwa kulipa asilimia 10 ya kipato wanachoingiza mwisho wa mwezi.

Baada ya mabadiliko hayo bodi hiyo ilianza msako wa kuwasaka waajiri ambao hawapeleki makato ya waajiriwa wanaufaika kwenye kampuni za umma, taasisi na mashirika binafsi lengo likiwa kuhakikisha fedha za mikopo zinarejeshwa ziwanufaishe wanafunzi wenye uhitaji.

Akizungumza na wanahabari jana jijini Dar es Salaam baada ya ukaguzi, Kaimu Mkurugenzi wa Urejeshaji wa Mikopo wa Heslb, Fidelis Joseph alisema baada kuzungumza na wahusika wa kampuni hiyo wamebaini wapo wafanyakazi watatu pekee wanaorejesha hivyo aliuagiza uongozi kuwasilisha majina yote.

Alisema kati ya wafanyakazi hao Dar es Salaam ni mmoja na wawili ni kutoka Dodoma hivyo kwakuwa kampuni hiyo ina wafanyakazi 200  ipo haja kwa wafanyakazi wengine kufanyiwa uhakiki kulingana na sheria zinazoiongoza bodi hiyo .

" Nimewaagiza wawasilishe majina mengine inawezekana katika wafanyakazi 200 kuna wengine wanaotakiwa kurejesha mikopo ili wanafunzi wenye uhitaji wanufaike,'' alisema Fidelis.

Alisema maelezo aliyopatiwa na viongozi wa kampuni hiyo hayatoshelezi kuamini wafanykazi watatu pekee kati ya 200 ndio wamenufaika na mikopo ya Heslb.

Aliwataka waajiri wote kuendelea kuwasilisha majina ya waajiriwa walionufaika ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kutozwa faini na kufikishwa mahakamani.


Kwa upande wake Msaidizi wa Kitengo cha Uendeshaji wa kampuni hiyo, Abeid Mwakikongo alisema walianza kuwasilisha makato ya waajiriwa wanufaika hao mwezi Aprili mwaka huu huku akiongeza leo watawasilisha majina ya wafanyakazi wote kama walivyoagizwa na Heslb.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI