MWALIMU COMMERCIAL BANK (MCB) YAFANYA MKUTANO WAKE WA KWANZA WA WANAHISA



NA K-VIS BLOG/Khalfan Said
BENKI ya Walimu, (Mwalimu Commercial Bank Plc-MCB)), iko mbioni kuanzisha huduma ya uwakala wa benki ambapo itashirikiana na mawakala wa sehemu mbalimbali nchini ili kuhakikisha inafikisha huduma za kibenki kwa wananchi  wote kwa urahisi, uhakika na unafuu.
Hayo yamesemwa Juni 22, 2017, mkoani Morogoro na Mwneyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya benki hiyo, Bw.Herman Mark Kessy, (pichani), kwenye Mkutano Mkuu wa Kwanza wa Wanahisa wa benki hiyo.
Aidha Mwenyekiti huyo aliwaambia wajumbe wa mkutano huo kuwa, benki hiyo pia iko katika mpango wa  kutumia huduma za ATM bila ya kadi (Cardless), huduma ambayo itasaidia sana wateja kutumia ATM hata bila ya kuwa na kadi.
“Kupitia huduma hii, wateja wataweza kupata pesa zao kupitia mawakala au kupakua programu maalum kwenye simu zao za kiganjani zitakazowezesha kulipa huduma za maji, umeme pia kutuma pesa kutoka kwenye akaunti zao kwenda kwenye huduma maalum ya benki kwa njia ya simu.” Alifafanua.
Akizungumzia hali ya taasisi za kifedha nchini, Bw.Kessy alisema, MCB iko imara licha ya changamoto zilizojitokeza hivi karibuni kufuatia agizo la serikali kuelekeza taasisi zake zote za serikali na umma kuhamisha na kupeleka fedha zote Benki Kuu na hivyo wateja wakubwa wa serikali walifunga akaunti zao na kuhamishia fedha zao BoT hali iliyosababisha ukwasi mkubwa.
“Lakini sio hilo katika zoezi la serikali la uhakiki wa watumishi wa umma, ilibaini watumishi hewa 19,000 na wakati zoezi hilo likiendelea kwa zaidi ya siku 90 urejeshaji wa makato ulisitishwa, hivyo basi mabenki ikiwemo benki yetu hatukupata marejesho ya mikopo kutoka kwa wafanyakazi walioathiriwa na zoezi hilo na pia kukosa mapato yatokanayo na riba ya mikopo hiyo.” Alisema.
Mwenyekiti huyo wa bodi aliwaambia wajumbe wa mkutano huo kuwa changamoto nyingine ni sheria inayotaka mabenki ili yaweze kufanya miamala ya fedha za kigeni nje ya nchi zinatakiwa kua na benki washirika ili kupitisha miamala hiyo.
“Kutokana na sheria hiyo, benki za Marekani zimeweka utaratibu mgumu kuhusu ushirikiano na mabenki ya nje, hivyo benki ndogo na za kati zimeshindwa kutimiza masharti ya kupata benki mshirika (Correspondence Banking), kutokana na hilo benki nyingi ndogo na za kati zimepoteza biashara na wateja.” Alifafanua Bw. Kessy.
Hata hivyo Bw. Kessy alisema pamoja na misukosuko hiyo, benki ya MCB imeendelea kufanya vizuri katika kuongeza wateja licha ya kuwa ngeni kwenye soko, ambapo hadi kufikia Juni, 2017  wateja wenye akaunti za akiba wamefikia 28,576 zenye thamani ya shilingi bilioni 5.3 huku idadi ya wateja wa mikopo ikifika 228 wenye thamani ya shilingi bilioni 3.1 na kwamba benki imeweza kuwafikia wateja katika sehemu mbalimbali za nchi.
Kuhusu mahusiano ya kibiashara na wanahisa waanzilishi wa benki hiyo, Bw. Kessy alisema, benki iemendelea kuimarisha uhusino wake na Chama cha walimu, pamoja na Mfuko wa Pensheni wa Watumishi wa Umma (PSPF).
“Mahusinao haya yamewezesha kuwapa wachangiaji wa Chama Cha Walimu, (CWT), mikopo yenye riba nafuu, vilevile tuko katika mkakati wa kushirikiana na PSPF kutoa mikopo ya riba nafuu kwa wanachama wake, hii yote ni katika kuwasaidia watumishi wa Umma kujikwamua kiuchumi na kuwa na maisha bora,” alisema.
Katika mkutano huo wa siku moja wajumbe watapokea taarifa na kuzijadili ambazo ni pamoja na taarifa ya fedha kwa kipindi cha mwaka 2016, kupitisha majina ya wakurugenzi wa bodi yaliyopendekezwa, kujadili na kupitisha posho za wakurugenzi, kujadili na kupitisha wakaguzi wan je wa benki kwa mwaka 2017 na pia kujadili na kupitisha mabadiliko yanayopendekezwa ya kubadilisha makala ya muundo, (MEMARTs) za kampuni.

 Wajumbe wa mkutano huo wakifuatilia maelezo yaliyokuwa yakitolewa
 Afisa Mtednaji Mkuu wa MCB, Ronald Manongi akizungumza kwenye ufunguzi wa mkutano huo
 Wajumbe wakifuatilia kwa utulivu mkutano huo
 Bw. Manongi
 Mkuu wa kitengo cha Hazina MCB, Nunu R. Saghal (kushoto), akijadiliana jambo na Mkuu wa kitengo cha fedha cha benki hiyo, Selemani Kijori

 Ambrose Mshula mjumbe wa bodi ya wakurugenzi MCB, (aliyesimama), akizungumza kwenye mkutano huo. Wengien kutoka kushoto, ni Mshauri wa ksiheria wa benki, Upendo Ngaponda, Afisa Mtendaji Mkuu wa MCB, Ronald Manongi, Mkurugenzi wa bodi ya benki, Said Kambi, Mwenyekiti wabodi ya wakurugenzi, Herman Kessy, George Fumbuka mwangalizi wa hisa na Mkurugenzi wa kampuni ya kimataifa ya ukaguzi wa mahesabu Ernst&Young, Deokan Mkenda
Mshauri wa kisheria wa MCB, Upendo Ngaponda akizungumzia
 Katibu wa CWT Manispaa ya Morogoro, Abubakar Rashid, (kushoto), na Mkuu wa kitengo cha ukuzaji biashara na masoko benki ya MCB, Valence Lutenganya, wakitazama kitu kwenye kompyuta
 Mjumbe akijisajili
 Maafisa wa juu wa benki ya MCB, kutoka kushoto, Charles Shedrack, Frederick Rwabukambara, Valence Lutenganya, na Selemani Kijori, wakijadiliana jambo
 Afisa Mtendaji Mkuu wa MCB, Ronald Manongi, (kushoto), akisalimiana na mwakilishi wa Mfuko wa Afya ya Jamii, (NHIF) Yasin Mwakababu. NHIF ni mmoja wa wanahisa wakubwa wa benki
 Msaidizi wa Afisa Mtendaji Mkuu wa MCB, Furaha Johnson, (kushoto), akiongozana na mmoja wa wakurugenzi wa benki hiyo, Dkt. Fidea Luhwano Mgina
 Wajumbe wakichukua makabrasha tayari kwa mkutano
 Wajumbe wakichukua makabrasha tayari kwa mkutano
 Wajumbe wakiwa kwenye mkutano na wengine wakipitia taarifa mbalimbali
 Mjumbe akipitia taarifa
 Wajumbe wakijisajili
 Mjumbe akielekea ukumbini


Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya Walimu (Mwalimu Commercial Bank Plc-MCB), Bw.Herman Mark Kessy, (katikati), akiongozana na Katibu Mkuu wa Chama Cha Walimu Tanzaia, Bw.Yahya Msulwa,(Kushoto) na Aifisa Mtendaji Mkuu wa MCB, Bw.Ronald Manongi..

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI