SERENGETI, NGORONGORO NA KILIMANJARO SI VIVUTIO PEKEE VINAVYOPATIKANA TANZANIA


Na Ripota wetu
Watalii wanaokuja Tanzania na kuelekea moja kwa moja kwenye hifadhi za taifa za Serengeti, Kilimanjaro au Ngorongoro inamaanisha nini? Ni kwamba wanakuwa wamekwishaambiwa kuwa ukifika Tanzania sehemu pekee za kutembelea ni hizo tu? Je tunawezaje kukabiliana na hali hii ambayo kwa namna moja ama nyingine inaweza kufifisha vivutio vilivyopo maeneo mengine nchini kutotembelewa?
Hakuna anayeweza kubisha kwamba sehemu ya Kaskazini mwa Tanzania imebarikiwa kwa kiasi kikubwa kuwa na vivutio visivyopatikana duniani kote. Vivutio kama hifadhi za kitaifa za Serengeti, bonge la Ngorongoro, Mlima Kilimanjaro na hivi karibuni mti mrefu zaidi barani Afrika uligunduliwa.

Tunapenda kukufahamisha kwamba tangu mwaka huu wa 2017 uanze nchi yetu imeshuhudia watu mbalimbali maarufu duniani wakifurika nyanda za Kaskazini wakiwemo Waziri Mkuu mstaafu wa Israel, Bw. Ehud Barak, muigizaji wa filamu kutokea Hollywood nchini Marekani, Will Smith na familia yake.

Kama hiyo haitoshi hazijapita hata wiki mbili tangu aliyekuwa nguli wa kusakata kabumbu nchini Uigereza, David Beckham ambaye aliwahi kuvichezea vilabu vya Manchester United, Real Madrid, LA Galaxy na PSG naye kutembelea hifadhi ya mbuga ya Serengeti akiwa na familia yake.

Huyo hakuwa mchezeji pekee kutokea bara la Ulaya kufanya hivyo kwani nyota anayechezea kwa mkopo katika klabu ya Crystal Palace inayoshiriki ligi kuu ya Uingereza akitokea Liverpool, Mamadou Sakho naye pamoja na mkewe na watoto wake wa kike wawili wameonekana wakifurahi mapumziko yao katika hifadhi ya mbuga ya wanyama ya Serengeti.
Jambo la msingi la kujiuliza hapa ni kwanini watu hao wote mashuhuri pindi tu watuapo uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwl. Nyerere hubadilisha ndege na kuelekea moja kwa moja uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro ambapo kutokea pale ni rahisi kwenda hifadhi za kitaifa za Serengeti, Ngorongoro na Mlima Kilimanjaro?

Tunafahamu kwamba suala la watalii kutembelea sehemu wanazozitaka wanapofika nchini Tanzania ni maamuzi yao na pia huchangiwa na sababu kadhaa kama vile vivutio miundombinu kama vile usafiri, hoteli zenye hadhi na kuvutia lakini pia na hali ya hewa kinaweza kuwa kigezo kingine.

Kwa kuzingatia sababu za miundombinu na huduma bora za malazi na zenye viwango vya kimataifa, hakuna ubishi kwamba nyanda za Kaskazini zimejitahidi kwa kiasi kikubwa kukidhi mahitaji ya watalii. Lakini linapokuja suala la vivutio vya kitalii na hali ya hewa bado Tanzania tumejaaliwa vivutio vya kila aina na hali ya hewa nzuri karibuni kila mikoa ya nchi hii.

Kwa mfano, ukitembelea mikoa ya Magharibi utakutana hifadhi za Gombe, Katavi, Mahale, Rubondo na Saanane. Kwa ukanda wa Mashariki kuna fukwe safi za bahari ya Hindi, visiwa vya Zanzibara, hifadhi ya Saadani, kisiwa cha Kilwa, mapango ya Amboni (Tanga) na Mikindani (Mtwara). Wakati ukienda Kusini mwa Tanzania yapo mengi ya kufurahi na kuyaona katika hifadhi za Kitulo, Mikumi, Ruaha na Udzungwa.
Utajiri wa maliasili unaopatikana katika hifadhi hizo hapo juu ni Dhahiri kwamba nchi ya Tanzania haijabarikiwa sehemu chache pekee. Bali tu ni namna tunavyovitangaza, kuvitolea elimu ya kutosha na kuvipa kipaumbele kwa wageni na watalii kuvitembelea.

Yapo mambo kadhaa ya kujifunza kutokana na ugeni wa watu hao mashuhuri kupendelea kuzuru baadhi ya sehemu tu nchini.

Kwanza kabisa, kuwa na vivutio pekee haitoshi kuwashawishi watalii kuja nchini kuvitembelea bila ya kuvitangaza. Dunia kwa sasa ina takribani zaidi ya nchi 190 na zote hizo zikiwa na vivutio vya kila namna. Watalii hawawezi kutembelea sehemu kama hawajafahamishwa ina mambo gani yatakayowavutia na kushawishika kutoka huko walipo. Hivyo basi badala ya kutegemea watalii na watu mbalimbali kusikia sifa za vivutio tulivyonavyo Tanzania kutoka kwa watu wao wa karibu, serikali na wananchi tunaowajibu wa kuvitangaza vivutio vyetu.
Lakini pia, sekta ya utalii kwa kiasi kikubwa huendena na uwepo wa miundombinu ya kisasa na ya kuvutia itakayowawezesha watalii kuvifikia vivutio na kufarahia muda wao pindi wanapokuwepo huko. Hapa tunazungumzia miundombinu kama vile usafiri na huduma za malazi kitu ambacho mikoa ya Kaskazini imejitahidi kuwekeza kwa kiasi kikubwa. Uwepo wa uwanja wa ndege kimataifa wa Kilimanjaro, barabara naHOTELI kadhaa zenye hadhi na viwango vya kimataifa ni vichocheo vikubwa kwa watalii kupenda kutembelea vivutio vya huko.

Hivyo basi kwa kumalizia, bado serikali na wananchi kwa ujumla tunalo jukumu la kuvitangaza na kuvilinda vivutio tulivyonavyo. Kwa kuvitangaza tunaweza kulifanikisha hilo kwa kuvitembelea na kuwajulisha watu wetu wa karibu juu ya mambo yanayopatikana huko. Pongezi kwa serikali kwani siku chache zilizopita katika kuadhimisha siku ya mazingira duniani ilitoa ofa kwa watanzania wote kutembelea hifadhi za mbuga za wanyama bila ya kiingilio chochote kwa siku tatu mfululizo ili kujionea mazingira na maliasili tulizojaaliwa.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI