DKT NCHIMBI APOKEA MADAWATI ZAIDI YA 2000 KUTOKA BUNGENI KWA NIABA YA MIKOA YA KASKAZINI


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi leo ampokea madawati 2579 kutoka kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa niaba ya mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro.

Akipokea madawati hayo yaliyosafirishwa katika magari 19 ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Dkt Nchimbi amelipongeza jeshi hilo kwa uzalendo huo wa kuhakikisha mali za umma zinafika Singida kwa ajili ya kuanza kusambazwa katika halmashauri husika zikiwa salama na katika hali nzuri.

Dkt Nchimbi amelipongeza Bunge kwa uzalendo wa kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli katika kuhakikisha sekta ya elimu inaboreka nchini  ili kutimiza azma ya kufikia uchumi wa kati na wa viwanda. 

Amesema madawati hayo yataongeza motisha kwa wanafunzi kujisomea kwakuwa mazingira yatawawezesha kuandika na kusoma kwa ufanisi zaidi.
Aidha Dkt Nchimbi amezitaka halmashauri zitakazopokea madawati hayo kuhakikisha wanayatunza ili yadumu na kuwanufaisha wanafunzi kwa muda unaostahili.

“Madawati na yenyewe yanahitaji ukarabati, sio kwakuwa mmepewa basi muyaache tu, hapana, ukiona ubao unalegea kidogo basi hakikisha unarekebisha na sio kuanza kusubiri waliotupatia ndo waturekebishie”, amesema na kuongeza kuwa.

“Ili madawati haya yadumu waalimu na wanafunzi kwa pamoja wahakikishe wanayatunza vizuri, hasa walimu wasimamieni wanafunzi na muaelekeze namna ya kuyatunza kwakuwa hii ni mali yetu sote”, Amesisitiza.

Aidha Dkt Nchimbi ameongeza kuwa mkoa wa Singida uko tayari kupokea vifaa na mambo mbalimbali ya kitaifa kutokana na kuwa katikati mwa Tanzania hivyo kuwezesha usambazaji kwa mikoa mingine kuwa rahisi.

“Tunakaribisha taasisi, mashirika, na hata serikali kuu kama kuna vifaa vingine leteni Singida ni katikati na usambazaji utakuwa ni rahisi, lakini pia hata shughuli zozote za kitaifa mkoa wa Singida uko tayari kabisa kuzipokea” amesema Dkt Nchimbi.

Kwa upande wake Afisa Elimu Vifaa na Takwimu wa halmashauri ya Wilaya ya Meru Frank Paul Mwambachi amelishukuru Bunge la Jamhuri ya Muungano kwa kuwapatia madawati ambapo halmashauri yake imepata madawati 400.

Mwambachi amelishukuru  JWTZ kwa kuyasogeza madawati jirani na halmashauri yake hivyo itakuwa rahisi na salama zaidi kwake kuyasafirisha na kuyafikisha yakiwa katika hali nzuri na kwa uharaka zaidi.

“Madawati 400 wakikaa wanafunzi watatu watatu ina maana ni wanafunzi 1200 wamenufaika, kwa kweli tunalishukuru sana bunge kwa uzalendo wao, pia jeshi limetusaidia sana kuyaleta madawati yetu Singida ambapo ni jirani” amesema Mwambachi.

Aidha ameongeza kuwa madawati hayo yataboresha mazingira ya ufundishaji na ya kujifunzia hivyo halmashauri itahakikisha wanayatunza ili wanafunzi wanufaike kwa kipindi kirefu.
 Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akipokea kwa furaha moja ya magari ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) yaliyokuwa yamebeba Madawati hayo 2579 yanapelekwa katika mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro. Madawati hayo yametolewa na bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akimpongeza kwa furaha mmoja wa mwanajeshi aliyehusika kusafirisha Madawati 2579 yaliyotolewa na bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro. Madawati hayo yamefikishwa Singida kwa ajili ya urahisi wa kuyasambaza katika mikoa hiyo.
 Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi akishirikiana na wanajeshi kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Askari wa Magereza kushusha madawati yalitolewa na Bunge. Madawati hayo 2579 yanapelekwa katika mikoa ya Manyara, Arusha na Kilimanjaro.

 Askari wa Magereza wakipanda moja ya magari ya JWTZ na kusaidia kushusha sehemu ya madawati 2579 yaliyopokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Singida kwa niaba ya mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro.
Afisa Elimu Vifaa na Takwimu wa  halmashauri ya Wilaya ya Meru Frank Paul Mwambachi akisaidiana na askari kubeba madawati waliyopatiwa na Bunge ambapo halmashauri yake imepewa madawati 400.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI