MWANAO AMEJIINGIZA KWENYE MAPENZI? FANYA HIVI!


NIMSHUKURU Mungu kwa Jumatatu nyingine murua, niwape pole wale wote ambao wanakutana na changamoto mbalimbali za maisha ya kila siku, wiki na hata mwezi na mwaka. Katika makala haya wiki hii natoa muongozo kwa wazazi ambao wana watoto ambao wameanza kujiingiza kwenye uhusiano wa kimapenzi.

Natumia fursa hii kukiri kuwa kumlea mtoto tangu kutungwa kwa mimba hadi kuzaliwa na hatimaye kulelewa mpaka kuvuka kile kipindi cha hatari si jambo dogo.
Kusema kweli changamoto ni nyingi na nyingine hatujui jinsi ya kuzitatua, lakini katika mada hii tunajuzana mengi kwa uhakika zaidi.
Wazazi wengi wamekuwa wakilichukulia juujuu suala la mtoto kuingia kwenye mapenzi. Unakuta mama au baba anasikia au anajua kuwa mwanaye tayari ameanza mambo ya kikubwa, lakini anachokifanya ni kumpiga au kumkaripia, jambo ambalo si sahihi kwa sababu zifuatazo;

NI LAZIMA APITIE STEJI HII
Piga ua, garagaza, mwanao ni lazima apitie steji hii ya kushiriki kwenye mapenzi. Ila kwa sababu wewe ni mzazi, unamuonea huruma kwa sababu unamuona bado ni mdogo hivyo pengine angesubiri japo akuekue kidogo. Matokeo yake, kama mzazi, unaona njia sahihi ni kuwa mkali kama pilipili.
Kama mzazi au mlezi, unakuwa humsaidii bali unaweza kumfanya akawa sugu au akaharibika zaidi kwa kuamini kwamba ukiwa mkali ndiyo suluhisho.
Hebu wazazi au walezi ambao watoto wao wamefikia umri wa kuanza kushiriki au kujihusisha na masuala ya mapenzi, jaribuni kukaa na kuzungumza na watoto wenu kuhusu athari za mimba za utotoni, magonjwa na madhara mengine ya kujiingiza kwenye mapenzi wakiwa na umri mdogo kiujumla.
Baadhi ya wazazi wanapoona au kubaini kuwa mtoto wake wa kike au kiume ameanza kujiingiza kwenye mapenzi hugadhabika na kuanza kuwapiga au kuwatukana, jambo ambalo si sawa, si busara. Unapogundua mwanao ameanza tabia hiyo, fanya yafuatayo;

MZAZI AU MLEZI ZUNGUMZA NA MWANAO
Kuna baadhi ya wazazi huwa wanashindwa kutumia busara kuzungumza na mtoto au watoto wao kuhusu suala la kujiingiza kwenye mapenzi. Kwa mzazi ambaye unasoma makala hii, kaa chini na mwanao, awe wa kike au wa kiume kisha zungumza naye kuhusu suala alilolianza.

MUELIMISHE
Kama umri wake ni ule wa vichocheo kuwa tayari kwa ajili ya kushiriki mapenzi, muelimishe athari zake ni zipi kama atapata mimba au kumpa mimba mtu ambaye atakuwa si chaguo lake.

ASIFANYE MAPENZI KWANZA
Kwa mfano, mwanao ana umri wa miaka 18, ni kweli umri wa utu uzima umefika, lakini kwa sababu wewe mzazi unajua tatizo la kufanya mapenzi akiwa na umri huo, basi mshauri asishiriki kwenye suala la mapenzi hadi pale atakapopata mtu ambaye anaamini ni mtu sahihi wa maisha yake.

MPE UHURU
Mzazi unapaswa kumpa mwanao uhuru wa kuchagua mpenzi mmoja ambaye anamuhitaji kwenye maisha yake, lakini ajiridhishe kwanza kwa kumchunguza kwa muda mrefu na siyo kukurupuka.
MPE ANGALIZO
Kama mzazi au mlezi, hakikisha unampa mwanao angalizo kuwa, kama atajiingiza kwenye mapenzi akiwa na umri mdogo, basi kuna uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa hatari ambayo yanaweza kuugharimu uhai wake. Mwambie kama akipiga au kupigwa mimba, uwezekano wa kufukuzwa au kuachishwa shule ni mkubwa mno hivyo kujiharibia maisha yake yote.
Tukutane wiki ijayo kwenye mada nyingine murua.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI

KOCHA WA AL.AHLY ASEMA YANGA NI TIMU BORA NA NGUMU