KANISA KATOLIKI LAMALIZA KERO YA MAJI MAHABUSU YA WATOTO


Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo (katikati) akisisitiza jambo kwa wageni waalikwa wakati akikabidhi kisima kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu (Kushoto)  kwa ajili ya mahabusu ya watoto mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kulia ni Padre Timotheo Maganga Mkurugenzi wa Mashirika ya Kipapa Dar es Salaam.
 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee  na Watoto, Ummy Mwalimu (kushoto) akisisitiza jambo kwa wageni waalikwa (hawapo pichani) wakati akipokea kisima toka kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo (katikati) kulia ni Padre Timotheo Maganga.
 Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo (kulia) akikata utepe kuzindua kisma cha maji mapema hii leo jijini Dar es Salaam, kushoto ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu.
 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu (kushoto) akifungua bomba kuashiria kupokea kisima toka kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo kulia.
 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu (kushoto) akisisitiza jambo kwa wageni waalikwa wakati akipokea kisima toka kwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo Mkuu (katikati) kulia ni Padre Timotheo Maganga
Picha na Eliphace Marwa - Maelezo.

Na Agness Moshi na Anthony Ishengoma- Maelezo.
Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam leo limekabidhi Kisima chenye thamani ya  Shilingi Milioni kumi na moja laki saba na themanini (Sh. 11,780,000/=) kwa Serikali ili kutatua tatizo la maji katika Mahabusu ya Watoto iliyoko Upanga jijini Dar es Salaam. 

Akiongea katika hafla ya makabidhiano ya Kisima hicho Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo amesema lengo kuu la Mchango wa Kanisa katika ujenzi wa Kisima hicho ni kuonesha kuwa Kanisa haliko mbali na Serikali katika shughuli mbalimbali za ujenzi wa Taifa. 

Alisema  Kanisa Katolitiki Tanzania linashirikiana na serikali katika juhudi zake za kuwaletea wananchi maendeleo bila kujali itikadi za kidini chama au kikabila ili kusudi wanapotoka kwenye vituo hivyo watambue wamesaidiwa  kutokana na mapenzi mema ya kanisa hilo kwa watu wote.

Naye Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu  amesema ujenzi wa kisima hicho umesaidia serikali kupunguza gharama ya kulipia bili ya maji ambayo kwa mwezi mmoja serikali ilikuwa inalipa Shilingi laki nne kwa ajili ya matumizi ya maji katika mahabusu hiyo. 

 Waziri Ummy amesema kutokana na ujenzi wa kisima hicho tatizo la maji limekwisha kwa asilimia  mia moja kwasababu kisima hicho kina uwezo wa kuzalisha lita 5,000 kwa saa.

Aidha amesema kuwa fedha ambazo zimeokolewa na ujenzi wa kisima hicho zitatumika kwa ajili ya kuwakatia Bima ya Afya Watoto wanaozuiliwa katika vituo hivyo ili kuwahakikishia upatikanaji wa matibabu. 

Amesema ni muhimu kwa jamii  kufahamu kuwa  ni Mahakama tu  ndio yenye uwezo wa kutoa amri ya watoto kuhifadhiwa katika  mahabusu  hiyo na sio mtu au chombo chochote kingine.

Waziri Ummy alimwambia Kardinali Pengo kuwa hapa nchini kuna Mahabusu 5 ambazo ni Mahabusu ya Watoto Dar es Salaam (Upanga), Mahabusu ya Watoto Tanga, Mahabusu ya Watoto Moshi, Mahabusu ya Watoto Arusha na Mahabusu ya watoto Mbeya.

Amezitaja huduma  zinazotolewa na Wizara yake kwa watoto walioko kwenye Mahabusu hizo kuwa ziko za aina tatu  ambazo ni uhifadhi na utunzaji wa  watoto, huduma za maadilisho kwa watoto ambao tayari Mahakama imewahukumu, na huduma za Kijamii za Marekebisho ya tabia kwa watoto waliokinzana na Sheria.

Wakati huo Mkurugenzi wa Mashirika ya Kipapa Kwa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye pia ni  Mwakilishi wa watoto na vijana wainjilishaji mtandaoni Padre Thimotheo Nyasulu  amesema kuwa, wameamua kutoa msaada huo baada ya kuona changamoto hiyo walipotembelea kituo hicho Desemba ,2016 kama sehemu ya matendo ya huruma kwa kanisa.

Aidha Padre Nyasulu ametoa rai kwa Wananchi na waandishi wa habari kutoendelea kuita vituo vya watoto waliokinzana na Sheria Mahabusu na kushauri viitwe vituo vya malezi kwasababu hali hiyo inawafanya kujiona wametengwa hali inayowaongezea adhabu.

Waziri Ummy   alisema Mahabusu  za watoto ni  moja kati ya huduma  kongwe hapa nchini mahususi  kwa  kuwahifadhi watoto walio kinzana na Sheria na ambao kwa sababu moja au nyingine hawakuweza kupata dhamana kwa kesi au  mashauri ambayo yanawakabili  Mahakamani.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI

KOCHA WA AL.AHLY ASEMA YANGA NI TIMU BORA NA NGUMU