MSIMU MPYA WA LIGI KUU YA VODACOM WAZINDULIWA LEO DAR


Na Rehema Lucas, DAR ES SALAAM
MSIMU mpya wa Ligi Kuu ya soka ya Vodacom Tanzania Bara umezinduliwa rasmi leo kwa wadhamini wakuu, kampuni ya Vodacom Tanzania kukabidhi vifaa kwa timu zote 16 zitakazoshiriki ligi hiyo msimu ujao.
Zoezi hilo limefanyika mjini Dar es Salaam leo na Vodacom wanaodhamini Ligi Kuu inayorushwa moja kwa moja na Azam TV, wamekabidhi vifaa mbalimbali zikiwemo jezi, viatu, mipira na suti za kimichezo.
Akikabidhi vifaa hivyo, Mkurugenzi wa Idara ya Masoko ya Vodacom, Hisham Hendi amesema kwamba, kwa mara nyingine tena katika kuhakikisha Ligi Kuu ya soka hapa nchini inaenda vizuri wanakabidhi vifaa vya ubora wa hali ya juu.
Msemaji wa Simba SC, Hajji Sunday Manara (katikati) akisalimiana na vijana waliokuwa wanaonyesha jezi za Yanga katika uzinduzi huo
Hajji Manara akiwa katikati ya vijana walioonyesha jezi za Simba
Viongozi wa Vodacom, Bodi ya Ligi na klabu zote 16 za Ligi Kuu wakiwa katika picha ya pamoja

Hendi amesema kwamba pia Vodacom imefurahishwa na klabu zilizopanda Ligi Kuu msimu huu kutoka Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara, Singida United, Lipuli na Mji Njiombe FC kuwa zimejiandaa vizuri kwa ushindani.
“Tunajisikia furaha kukabidhi vifaa hivi tukiwa tunatakeleza matakwa ya mkataba wa udhamini  na ni imani yetu kwamba timu zitakazoshiriki Ligi Kuu zimejiandaa vya kutosha kwa msimu mpya wa Ligi,” amesema Hendi
Kwa upande wake, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Boniphace Wambura ameishukuru  Vodacom Tanzania na kuzitaka klabu zinazoshiriki Ligi Kuu kuzingatia na kuheshimu nembo ya mdhamini wakati wa mechi.
Wambura amesema Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) halipendi kutumia kanuni na sheria kuziadhibu klabu zitazokwenda kinyume na maelekezo hayo.
Ameongeza kwamba, msimu huu wa Ligi Kuu utakuwa bora kutokana na maandalizi yote kukamilika mapema – pia timu zitakazoshiriki kuwa zimejiandaa vizuri.
Timu nyingine zinazoshiriki Ligi Kuu ni mabingwa, Yanga SC, washindi wa pili, Simba SC, wa tatu, Kagera Sugar, wa nne Azam FC, wa tano Mtibwa Sugar, wa sita Stand United, wa saba Ruvu Shooting, wa nane Tanzania Prisons, wa tisa Maji Maji, wa 10 Mwadui, wa 11 Mbeya City, wa 12 Mbao FC na wa 13 Ndanda FC.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*