OBREY CHIRWA ASIMAMISHWA KUCHEZA LIGI KUU YA VODACOM, APELEKWA KAMATI YA NIDHAMU


Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM
MSHAMBULIAJI wa Yanga, Mzambia Obrey Chirwa amesimamishwa kucheza Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara hadi suala lake litakapotolewa maamuzi na Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Chirwa amesimamishwa baada ya kutuhumiwa kufanya vitendio vya utovu wa nidhamu katika mechi namba 83 baina ya timu yake, Yanga SC na Tanzania Prisons ya Mbeya iliyomalizika kwa sare ya 1-1 Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
Pamoja na Chirwa, mchezaji wa Tanzania Prisons, Lambart Sabiyanka naye amesimamishwa kwa kuzingatia Kanuni ya 9(5) ya Ligi Kuu kutokana na kufanya vitendo vya utovu wa nidhamu, wakisubiri malalamiko dhidi yao kusikilizwa na Kamati ya Nidhamu ya TFF.
Mzambia Obrey Chirwa (katikati) amesimamishwa kucheza Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara hadi suala lake litakapotolewa maamuzi na Kamati ya Nidhamu  

Hayo yamefikiwa katika kikao cha Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi, maarufu Kamati ya Saa 72 kilichofanyika jana mjini Dar es Salaam kujadili mechi mbalimbali za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Ligi Daraja la Kwanza na Daraja la Pili.
Kamati pia imeiomba TFF iipatie Bodi ya Ligi uamuzi (ruling) wa Kamati ya Nidhamu juu ya mchezaji wa Yanga kusimamishwa baada ya mechi dhidi ya Mbao FC wakati akisubiri mashtaka yake ili kuufanyia kazi kwa ajili ya mapendekezo ya marekebisho ya Kanuni.
Tanzania Prisons imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) baada ya kuhudhuria kikao cha maandalizi ya mechi (pre-match meeting) ikiwa na maofisa watatu badala ya wanne, hivyo kwenda kinyume na Kanuni ya 14(2b) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.
Adhabu dhidi ya Tanzania Prisons katika mechi hiyo iliyochezwa Novemba 25, 2017 Uwanja wa Azam Complex ni kwa mujibu wa Kanuni ya 14(3) ya Ligi Kuu.
Wachezaji Lambart Sabiyanka wa Tanzania Prisons na Obrey Chirwa wa Yanga wamesimamishwa kwa kuzingatia Kanuni ya 9(5) ya Ligi Kuu kutokana na kufanya vitendo vya utovu wa nidhamu, wakisubiri malalamiko dhidi yao kusikilizwa na Kamati ya Nidhamu ya TFF.
Mechi namba 72 (Mbeya City 0 vs Simba 1).Kamishna wa mechi hiyo Billy Mwilima amepewa Onyo Kali kwa kuruhusu mchezaji Hamisi Msabila wa Mbeya City kucheza mechi bila kuonyesha leseni, hivyo kukiuka Kanuni ya 14(16 na 17) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.  
Mechi namba 81 (Ndanda 1 vs Njombe Mji 1). Klabu ya Ndanda imepigwa faini ya sh 500,000 (laki tano) kwa kutowasilisha orodha ya wachezaji wake (team match list) kwenye kikao cha maandalizi ya mechi (pre- match meeting) kama ilivyoainishwa katika Kanuni ya 14(2k) ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo. Adhabu dhidi ya Ndanda katika mechi hiyo iliyofanyika Novemba 24, 2017 kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 14(3) ya Ligi Kuu.
Pia Kamati imeiomba Sekretarieti ya Bodi ya Ligi kutoa Waraka mwingine kwa klabu kuzikumbusha kuhusu kutoa orodha ya wachezaji kwenye kikao cha maandalizi ya mechi (pre-match meeting).
Mechi namba 84 (Mbao 1 vs Mwadui 0). Klabu ya Mbao FC imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kutokana na washabiki wake kuruka uzio wa ndani na kwenda kushangilia katika eneo lisiloruhusiwa katika mechi iliyochezwa Novemba 25, 2017 Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Adhabu dhidi ya Mbao FC ni uzingativu wa Kanuni ya 42(1) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Klabu.
Mechi namba 90 (Lipuli 0 vs Tanzania Prisons 1).Mtunza Vifaa wa Lipuli FC, George Mketo amesimamishwa akisubiri suala lake la kuwatukana waamuzi katika mechi hiyo iliyofanyika Desemba 30, 2017 Uwanja wa Samora mjini Iringa kusikilizwa na Kamati ya Nidhamu. Uamuzi wa kumsimamisha umezingatia Kanuni ya 9(5) ya Ligi Kuu kuhusu Usimamizi wa Ligi.
Mechi namba 94 (Mbao 2 vs Yanga 0). Kocha wa Mbao FC, Etiene Ndayiragije amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) baada ya kuondolewa kwenye mchezo (ordered off) na Mwamuzi kwa kushindwa kuheshimu taratibu na kuonywa mara tatu.
Adhabu hiyo dhidi ya Kocha Ndayiragije katika mechi hiyo iliyofanyika Desemba 31, 2017 Uwanja wa CCM Kirumba imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 40(11) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Makocha.
Pia klabu ya Mbao FC imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) baada ya kuonyeshwa kadi zaidi ya tano katika mechi hiyo. Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42(10) kuhusu Udhibiti wa Klabu.
Mechi namba 96 (Mwadui 2 vs Ruvu Shooting 1).Klabu ya Mwadui imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) baada ya kuonyeshwa kadi zaidi ya tano katika mechi hiyo iliyochezwa Januari 1, 2018 Uwanja wa Mwadui Complex. Adhabu hiyo imetolewa kwa kuzingatia Kanuni ya 42(10) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti wa Klabu

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA