Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli amesisitiza haja ya watanzania kuendelea kudumisha amani na wasikubali kutumika kuivuruga amani ya nchi.
Katika maadhimisho makuu huko mjini Dodoma ya miaka 54 tangu Tanganyika na Zanzibar zilipoungana na kuunda Tanzania, Rais Magufuli amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwepo kwa Muungano wa nchi.
Licha ya kwamba kumekuwa na mazungumzo kuhusu maandamano dhidi ya Rais wa Tanzania Dokta John Magufuli ambayo yaliopangwa kufanyika leo, hali imekuwa shwari.
Kumekuwa na utulivu wa kawaida katika baadhi ya maeneo nchini licha ya kwamba kumekuwa na mazungumzo kuhusu maandamano dhidi ya kiongozi huyo na utawala wake.
Ndani ya mkoa wa kibiashara wa Dar es Salaam, wakaazi wamekuwa wakiendelea na shughuli mbalimbali kama kawaida.
Ulinzi mkali umeimarishwa sehemu mbalimbali nchini kwa ajili ya kuwa tayari kukabiliana na jambo lolote litakalo onekana kuhatarisha amani.
Kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa, mwanaharakati wa kwenye mitandao ya kijamii, mtanzania ambaye makaazi yake ni nchini Marekani amekuwa akiratibu maandamano kupitia ukurasa wake wa Instagram.
Comments