Forbes: Trump ashuka orodha ya matajiri duniani 2018


Donald TrumpHaki miliki ya pichaGETTY IMAGES
Rais wa Marekani Donald Trump ameshuka nafasi 222 katika orodha ya kila mwaka ya watu tajiri zaidi duniani ambayo hutolewa na jarida la Forbes.
Mali yake imeshuka thamani kutoka $3.5bn (£2.5bn) hadi $3.1bn.
Jarida hilo limesema kushuka kwa utajiri wa Trump kumetokana zaidi na kushuka kwa thamani ya nyumba na vipande vya ardhi New York na pia kushuka kwa mapato kutoka kwa viwanja vyake vya kuchezewa mchezo wa gofu.
Anayeongoza orodha ya matajiri wa kupindukia ni mmiliki wa kampuni ya Amazon, Jeff Bezos.
Utajiri wa Bezos umepanda na kufikia $112bn kutoka takriban $39.2bn mwaka jana.
Kuimarika kwa utajiri wa Bw Bezos ndiko kwa juu zaidi katika historia.
Amemuondoa mwanzilishi wa Microsoft Bill Gates kutoka uongozini kwenye orodha hiyo.
Utajiri wa Gates unakadiriwa kuwa $90bn mwaka huu kutoka $86bn, na ndiye anayeshikilia nafasi ya pili.
Bw Gates ameongoza orodha hiyo kwa miaka 18 kati ya miaka 24 iliyopita.
Forbes wanasema kuna mabilionea 2,208 (kwa kutumia dola za Marekani) ambao walishirikishwa katika orodha ya 32 ya kila mwaka ya jarida hilo.
Matajiri hao kwa pamoja wana utajiri wa $9.1 milioni.
Miongoni mwao, kuna mabilionea 259 wapya ambao walijipatia utajiri wao kutoka wka biashara za aina nyingi zikiwemo nguo za harusi, wanasesere wa kuchezewa na watoto na magari yanayotumia umeme.
Mwekezaji mmarekani Warren Buffett ndiye wa tatu utajiri wake ukiwa $84bn. Utajiri wake umepanda kutoka $75.6bn mwaka uliotangulia.
mtu tajiri zaidi Ulaya ndiye wa nne kwenye orodha hiyo, ambaye ni mmiliki wa kampuni ya bidhaa za kifahari ya LVMH, Bernard Arnault, ambaye utajiri wake ni $72bn.
Matajiri
'Kupanua pengo'
Marekani ndiyo nchi iliyo na mabilionea wengi duniani, ambapo ina mabilionea 585, ikifuatwa na China. Jimbo la California pekee lina mabilionea 144, zaidi kushinda mataifa yote isipokuwa Marekani na China.
Ujerumani ndiyo nchi inayoongoza Ulaya ikiwa na mabilionea 123.
India ina mabilionea 119 nayo Urusi mabilionea 102.
Kuna mabilionea 53 kutoka Uingereza kwa mujibu wa Forbes na idadi hiyo imeshuka kutoka 54 mwaka 2017.
Luisa Kroll na Kerry Dolan kutoka kwa Forbes Media alisema: "Watu matajiri kupindukia wanazidi kupanua mwanya kati yao wenyewe, na pia kati yao na watu wengine."
Orodha ya mabilionea ya Forbes inatumia takwimu za kufikia Februari 9, 2018.
Jarida hilo hutumia bei ya soko la hisa na ubadilishanaji wa fedha za kigeni ya siku hiyo kutoka kila pembe duniani kuandaa orodha hiyo.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.