TAARIFA YA KUPOROMOKA KWA JENGO LA GHOROFA JIJINI DAR- ES – SALAAM

TAARIFA YA KUPOROMOKA KWA JENGO LA GHOROFA JIJINI DAR- ES – SALAAM MTAA WA INDIRA GANDHI NA BARABARA YA MOROGORO
KIWANJA NA.
 
1. UTANGULIZI.
Sheria zinazosimamia masuala ya ujenzi mijini zilitungwa kwa mara ya kwanza mwaka 1920 wakati wa utawala wa Mwingereza. Sheria hizo zilijukana kama Kanuni za Miji (Township Rules, Cap.101) ambapo Kanuni za Ujenzi Mjini (Township (Building Rules) Cap. 101 zilikuwa sehemu ya Kanuni hizo. Sheria hizo pamoja na mambo mengine zililenga kusimamia shughuli zote za majenzi mjini.

Aidha, Msimamizi wa sheria hizi zilikuwa Mamlaka za Miji, Manispaa na jiji ( kwa wakati huo) kwa sasa ni Majiji, Manispaa na Miji). Hata hivyo sheria hizi hazikuwa zinafanya kazi peke yake kwani mwaka 1968 Serikali ya Tanzania ilitunga sheria ya Wahandisi ( yaani the Engineers (Registration) Act,No.49/1968) na mwaka 1972 ilitungwa Sheria ya kusimamia Wasanifu Majengo ,Wakadriaji Majengo na Wakandarasi, Na.35/1972. Sheria zote hizo kwa pamoja zilikuwa zikisimamia shughuli zote za ujenzi mjini.

Kutokana na taratibu zilizokuwa zimezoeleka tangu huko nyuma usimamizi wa shughuli za ujenzi mjini zimeonekana kuwa mamlaka ya usimamizi ni Halmashauri ya Mji,Manispaa au Jiji husika na siyo wadau wengine. Kwa ujumla dhana hii sio sahihi hata kidogo. Kama tulivyoona hapo juu wadau katika sekta hii ni wengi ambao wanapaswa kusimamia shughuli zote za ujenzi pamoja na ubora wa kazi zinazofanywa na wakandarasi, watalaamu washauri kwa maana ya wahandisi na wasanifu majengo.Taarifa hii inakusudia kutoa ufafanuzi juu ya jengo la ghorofa kumi na sita lililokuwa linajengwa katika kiwanja Na……………………barabara ya Morogoro na mtaa wa Indira Gandhi jijini Dar es salaam kuporomoka siku ya tarehe 29/03/2013.

2. Nini msimamo wa Sheria zinazosimamia Ujenzi Mjini.
Kama ilivyooneshwa hapo juu historia ya sheria zinazosimamia ujenzi mjini zilivyoanza na baadaye mabadiliko ya uchumi yalisababishwa kutungwa kwa sheria ya kusajili Wahandisi mwaka 1968 na baadaye sheria ya Wasanifu majengo ,Wakandarasi na Wakadriaji majengo.

Hivi leo sheria zote hizo hapo juu zilifutwa na kutungwa upya na kutoa majukumu ya msingi kwa kila mamlaka ( Mdau).
Tukianza na Kanuni za Ujenzi Mijini Sura, 101 ilifutwa Mwaka 1994 kwa Sheria Na.8 /1994 (yaani the Law Revision Act, No.8/1994). Baada ya kufutwa sheria hii Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Nchini kote zilikaa kwa kipindi cha miaka 14 bila kuwa na sheria ya kusimamia ujenzi mijini mpaka zilipotungwa Kanuni za Miji chini ya Tangazo la serikali Na.242/2008 (the Local Government (Urban Authourities) (Development Control) Regulations, GN.No.242/2008).

Kanuni hizi zinaweka wajibu kwa Halmashauri kutoa kibali kwa mujibu wa Kanuni Na.124 kulingana na mchoro uliowasilishwa.

Vilevile, kanuni hizi zinaweka wajibu Mhandisi au Msanifu majengo kuandaa hesabu ya uzito wa vyuma vitakavyotumika kujenga jengo husika hii ni kwa mujibu wa Kanuni Na.143.

Kwa mantiki hiyo Halmashauri si Mamlaka pekee ya usimamizi wa majengo makubwa ya umma na /au binafsi ambayo matumizi yake ni kwa ajili ya biashara au shughuli nyinginezo za kibinadamu.Taasisi zifuatazo ni mamlaka za usimamizi ambazo zimeanzishwa na sheria ya Bunge:-

1. Bodi ya Wasanifu Majengo ,Wakadriaji Majengo ni mamlaka iliyoanzishwa na Sheria Na.16/1997( the Architects and Quantity Surveyors (Registration) Act [cap.269 R.E 2002] na mwaka 2010 sheria hii ilifanyiwa marekebisho ambayo kimsingi hayakuathiri majukumu yake. Fungu la 4 la sheria hii linaweka majukumu kwa chombo hiki kufanya yafuatayo;-

• Kusimamia shughuli na utendaji kazi wa wasanifu majengo ,wakadriaji majengo pamoja na kampuni zinazofanya kazi ya utalaamu ushauri katika kusimamia miradi ya ujenzi;

• Kuingia na kukagua shughuli zote za ujenzi unaofanyika hapa nchini kwa madhumuni ya kujiridhisha na kuhakikiksha kama kazi ya ujenzi inayofanyika inafanywa na mtu ambaye amesajiliwa na bodi na anazingatia taratibu,kanuni na sheria zote zinazosimamia ujenzi mijini; na

• Kuhakikisha kuwa maeneo yote ambako ujenzi unafanyika kumewekwa mabango yenye kuonyesha jina na anwani ya mradi, jina la mteja (mmiliki) , watalaamu washauri kwa maana wasanifu majengo na wahandisi pamoja na mkandarasi endapo atakuwa hakufanya hayo atachukuliwa hatua za kisheria.

2. Bodi ya Usajili wa Wahandisi ni mamlaka iliyoanzishwa na sheria Na.15/1997(the Engineers Registration, Act [Cap.63 R.E 2002]. Fungu la 4 la sheria hii linaweka majukumu kwa chombo hiki kufanya yafuatayo;-

• Kufuatilia na kusimamia shughuli na utendaji kazi wa wahandisi ikiwa ni pamoja na kampuni zinazofanya kazi ya utalaamu ushauri wa usimamizi wa miradi ya majenzi mijini;

• Kuingia na kukagua shughuli zote za ujenzi unaofanyika hapa nchini kwa madhumuni ya kujiridhisha na kuhakikiksha kama kazi ya ujenzi inayofanyika inafanywa na mtu ambaye amesajiliwa na bodi na anazingatia taratibu,kanuni na sheria zote zinazosimamia ujenzi mijini; na

• Kuhakikisha kuwa maeneo yote ambako ujenzi unafanyika kumewekwa mabango yenye kuonyesha jina na anwani ya mradi, jina la mteja (mmiliki) , watalaamu washauri kwa maana wasanifu majengo na wahandisi pamoja na mkandarasi endapo atakuwa hakufanya hayo atachukuliwa hatua za kisheria.

3. Bodi ya Wakandarasi [CRB] ni mamlaka iliyoanzishwa na sheria Na.17/1997( the Contractors Registration Act, [Cap.235 R.E 2002] Fungu la 4 la Sheria hii linaweka majukumu kwa chombo hiki kufanya yafuatayo;-

• Kusimamia shughuli na utendaji kazi wa Wakandarasi katika kujenga majengo imara na yenye kufuata viwango kwa mujibu wa michoro ya majengo hayo;

• Kuingia na kukagua shughuli zote za ujenzi unaofanyika hapa nchini kwa madhumuni ya kujiridhisha na kuhakikiksha kama kazi ya ujenzi inayofanyika inafanywa na mtu ambaye amesajiliwa na bodi na anazingatia taratibu,kanuni na sheria zote zinazosimamia ujenzi mijini; na


• Kuhakikisha kuwa maeneo yote ambako ujenzi unafanyika kumewekwa mabango yenye kuonyesha Jina na anwani ya mradi, jina la mteja (mmiliki) , Watalaamu washauri kwa maana wasanifu majengo na wahandisi pamoja na mkandarasi endapo atakuwa hakufanya hayo atachukuliwa hatua za kisheria.

4. Mamlaka nyingine ya usimamizi ni usalama mahali pa kazi (Occupational, Safety and Health Agency). Hiki ni chombo ambacho kinashiriki pia kusimamia miradi ya ujenzi mijini. Mamlaka hii hutoa kibali na kusajili mradi kama ambavyo mamlaka nyingine ambavyo zinafanya kwa kutoa “sticker”.

5. Hitimisho.
Kama ilivyoonyeshwa hapo juu tumeona kwamba zipo sheria mbalimbali zenye kubainisha wadau wote wanaohusika na usimamizi wa majenzi mijini. Hivyo tunaomba ieleweke kwa umma kwamba Halmashauri ya Manispaa ya Ilala si mamlaka pekee ya usimamizi. Hii ni kwasababu muombaji wa kibali anapoomba na kukubaliwa baada ya kupitia michoro yake ambayo mara nyingi huwa imeandaliwa na Wasanifu na Wakadriaji majengo pamoja na “Structural Engineer” ambao wanasimamiwa na mamlaka zilizobainishwa hapo juu. Halmashauri huwa haina nafasi zaidi ya kitalaamu ya kusimamia katika masuala makubwa hasa ya vyuma na kiwango cha “material” yanayotumika katika ujenzi ; isipokuwa kufuatilia kama muombaji (mmiliki) anajenga kama ambavyo alionyesha katika michoro iliyopitishwa kwa mujibu wa mpango wa uendelezaji wa eneo husika.

________________________________
Imetolewa Na:
Mstahiki Meya
katika kikao cha dharura cha Baraza la Madiwani (1/04/2013),
Halmashauri ya Manispaa ya Ilala
Dar- es - salaam.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

HATUTOPAKI BASI DHIDI YA YANGA-MOKWENA

“PEMBA SALUTI KWENU” DK. NCHIMBI*

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA