SERIKALI KUENDELEA KUBORESHA UWEKEZAJI NA UKUAJI WA UCHUMI

 Na. Farida Ramadhani na Joseph Mahumi, WF, Dodoma.


Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amesema kuwa Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na ukuaji wa uchumi nchini.

Dkt. Nchemba alisema hayo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano wa Majadiliano ya Kimkakati kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo Ngazi ya Juu, ambao unalenga kubadilishana maarifa, taarifa, na uzoefu kuhusu sera na mikakati ya maendeleo ya nchi.

Alisema Serikali imewasilisha bungeni Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania (Tanzania Investment Act, 2024) na kuanzisha Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi (Tanzania Investment and Special Economic Zones Authority) ili kuboresha mazingira ya uwekezaji. 

“Serikali kupitia Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) na Kituo cha Uwekezaji kati ya Sekta Binafsi na Umma (CPPP) imeendeleza majadiliano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi ili kuongeza ushiriki wa sekta binafsi katika maamuzi”, aliongeza Mhe. Dkt. Nchemba.

Mhe. Dkt. Nchemba ambaye ni Mwenyekiti wa Mkutano huo, alisema Serikali pia inaandaa Mkakati wa Kitaifa wa Uendelezaji wa Uwekezaji (2025/2026 – 2034/2035) ambao utakuwa na mpango wa utekelezaji, ufuatiliaji na tathmini, unaoeleza majukumu ya kila mdau na viashiria vya kupima maendeleo.

Dkt. Nchemba alibanisha kuwa katika kipindi cha mwezi Julai 2024 hadi Desemba 2024, Serikali imeongeza uwezo wa uzalishaji umeme kwa asilimia 30.3, hasa kupitia Mradi wa Umeme wa Maji wa Julius Nyerere (JNHPP) ili kupunguza gharama za biashara.

“Kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2024, Serikali imepunguza au kuondoa ada na tozo mbalimbali ili kuboresha mazingira ya biashara”, aliongeza Mhe. Nchemba.

Dkt. Nchemba alisema Serikali pia imepata mafaniko makubwa katika ukuaji wa uchumi jumuishi ambapo idadi ya shule na wanafunzi imeongezeka, vituo vya afya vimeongezeka na huduma zimeboreshwa, huduma za maji zimeongezeka katika maeneo yote nchini pamoja na ongezeko la ajira.

Aidha, alitoa rai kwa wadau wote kushirikiana kwa karibu na Serikali ili kufanikisha utekelezaji wa Mwongozo wa Ushirikiano wa Maendeleo (DCF) ambao umetilia mkazo utaratibu wa ufadhili wa miradi ya mabadiliko ya tabianchi (climate financing modality) na kuimarisha Ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) kama njia mbadala za ufadhili.

Kwa upande wake Mwenyekiti Mwenza wa Kundi la Washirika wa Maendeleo na Balozi wa Ireland nchini, Mhe. Nicola Brennan aliishauri Serikali kuendelea kuboresha mazingira ya biashara kwa kuondoa vikwazo vinavyozuia uwekezaji wa moja kwa moja wa kigeni.

Alisema hii itaongeza mchango wa sekta binafsi katika kuleta uwekezaji, ajira, uvumbuzi, na suluhisho kwa changamoto mbalimbali ili kujenga uchumi imara. 

“Wadau wa Maendeleo tayari tumekuwa na majadiliano mazuri kuhusu hili, na tunapongeza utayari wa Serikali kushirikiana nasi kuona jinsi bora ya kuondoa vikwazo na kuvutia uwekezaji zaidi wa moja kwa moja wa kigeni (FDI) nchini Tanzania, pamoja na kuimarisha sekta ya biashara ya ndani”, aliongeza.

Mhe. Brennan alisema Washirika wa Maendeleo watahakikisha kuwa Dira ya Maendeleo ya Mwaka 2050 inapata ufadhili wa uhakika na endelevu, hasa katika sekta za afya, elimu na sekta ya kijamii kwa ujumla.

“Tunapopanga vipaumbele katika matumizi ya rasilimali finyu za Msaada wa Maendeleo (ODA), ni muhimu pia kuelewa vyema vyanzo vingine vya ufadhili vinavyopatikana kwa nchi zenye kipato cha kati nje ya ODA, pamoja na mchango ambao sisi kama Wadau wa Maendeleo tunaweza kutoa kusaidia Tanzania kuzifikia na kuzitumia fursa hizo ipasavyo. Tunatazamia kujadili zaidi suala hili kwa kina.”

Aliahidi kuwa Washirika hao wataendelea kushirikiana na Tanzania kuhakikisha maendeleo yanapatikana na kustawisha jamii. 
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akizungumza wakati akifungua Mkutano wa Majadiliano ya Ngazi ya Juu kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo, uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage-Treasury Square, jijini Dodoma, ukiwahusisha baadhi ya Mawaziri wa Kisekta kutoka Tanzania Bara na Tanzania Visiwani, pamoja na Wanadiplomasia na Washirika wa maendeleo wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini, ambapo pamoja na mambo mengine alitoa rai kwa wadau wote kushirikiana kwa karibu na Serikali ili kufanikisha utekelezaji wa Mwongozo wa Ushirikiano wa Maendeleo (DCF) ambao umetilia mkazo utaratibu wa ufadhili wa miradi ya mabadiliko ya tabianchi (climate financing modality) na kuimarisha Ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) kama njia mbadala za ufadhili.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAMBO 8 MWANAMKE HUFANYA KWA MWANAUME ANAYEMPENDA