OFISA WA BUNGE AUAWA KWA RISASI

WAKATI Bunge likiendelea kuomboleza vifo vya wabunge wake wawili, Regia Mtema (Viti Maalumu Chadema) na Jeremiah Sumari Arumeru Mashariki CCM), limepata pigo jingine baada ya mfanyakazi wake, Nicolaus Luther Senge kufariki dunia kwa kupigwa risasi na askari polisi katika tukio ambalo lilisababisha vifo vya watu watatu.
Hata hivyo, kumekuwa na taarifa za kutatanisha na zenye kupingana kati ya polisi na Bunge kuhusu jina halisi la mfanyakazi huyo na mahali ambako mwili wake umehifadhiwa.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana zimeeleza kuwa Senge (49) alifariki dunia usiku wa kuamkia jana katika mauaji yaliyofanyika kwenye kikao cha wanafamilia Kibaha mkoani Pwani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Ernest Mangu amethibitisha kifo hicho lakini akamtaja mtumishi huyo wa Bunge kuwa ni Nkolo Senge.
Kamanda Mangu alisema katika tukio hilo lililotokea nyumbani kwa Pendael Senge ambaye ni Mratibu wa Tasaf Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani, wengine waliofariki dunia ni Andrew Nkolo (30) na askari polisi Nicodemus Senge ambaye ndiye anayetuhumiwa kuwaua wenzake.
Alisema siku ya tukio, watu hao walifika nyumbani kwa Pendael ambaye ni baba yao mdogo kwa ajili ya kupatanishwa juu ya ugomvi wa urithi wa ekari mbili za ardhi zilizoko kijijini kwao Singida.
“Ugomvi huo ulianzia Singida ambako walishtakiana lakini hakimu akawataka waumalize kiukoo. Ndipo Pendaheli ambaye ni baba yao mdogo akaamua kuwaita nyumbani kwake ili wazungumzie suala hilo,” alisema Kamanda Mangu na kuendelea:
“Wakiwa kweye kikao hicho kabla ya kufikia mwafaka, Nicodemus ambaye ni askari polisi wa Kituo cha Usalama Magomeni, Dar es Salaam alichomoa bastola yake na kuwamiminia risasi ndugu zake hao kisha kujimaliza mwenyewe.”
Kwa mujibu wa Kamanda Mangu, miili ya marehemu hao imehifadhiwa katika Hospitali ya Tumbi, Kibaha na hakuna aliyekamatwa kuhusiana na tukio hilo.
Kauli ya Ofisi ya Bunge
Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai amethibitisha kutokea kwa kifo cha mfanyakazi huyo wa Bunge na kueleza kuwa hadi jana mchana, lakini akasema maiti yake ilikuwa imehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Ndugai alisema Ofisi ya Bunge imesikitishwa na kifo hicho kilichotokea usiku wa kuamkia jana, siku chache baada ya taasisi hiyo ya kutunga sheria kupoteza wabunge wawili.
“Kwa sasa nipo Arusha lakini taarifa za kifo cha Senge nilizipata jana. Bado sina taarifa zaidi kuhusu kifo hicho kwa sababu kimetokea kwa njia ambayo lazima ihusishe uchunguzi wa kipolisi,” alisema Ndugai.
Hilo ni pigo jingine kwa taasisi hiyo katika kipindi cha juma moja baada ya Mtema kufariki dunia Januari 14, kwa ajali ya gari iliyotokea Ruvu, Kibaha na Sumari alifariki dunia Januari 17, mwaka huu baada ya kuugua kwa muda mrefu saratani ya ubongo.
Kauli ya familia
Baba mdogo wa marehemu hao Pendael Senge naye alithibitisha mauaji hayo na kueleza kuwa yalitokana na ugomvi wa shamba.
Pendael alisema askari huyo aliwaua ndugu yake Nicolaus Senge ambaye alikuwa mtumishi wa Ofisi ya Bunge, pamoja na binamu yake Andrew Nkolo (mtoto wa shangazi yake).
Akisimulia tukio hilo Pendael alisema kabla ya mauaji hayo, ndugu hao walifika nyumbani kwake Kongowe Kibaha kwa ajili ya kikao cha usuluhishi kuhusiana na ugomvi huo wa shamba. Hata hivyo, alisema usuluhishi huo ulishindikana na badala yake ukazuka ugomvi baina ya ndugu hao uliwafanya wapigane ngumi kabla ya wanandugu kuwaamulia.
Alisema muda mfupi baada ya ndugu kuwaamulia, askari huyo aliwapiga risasi ndugu zake kisha naye kujimaliza.
Alisema chanzo cha ugomvi huo ni shamba la ekari mbili lililoko katika Kijiji cha Ilunda Wilaya ya Iramba, Singida... “Shamba hilo ni la mpwa wangu Andrew ambalo alirithishwa na mama yake aliyefariki dunia takriban miaka 15 iliyopita,” alisema Pendael na kuongeza:
“Lakini kwa kuwa Andrew anafanya shughuli zake za Steshenari Dar es Salaam, basi binamu yake Nicodemus Senge akajenga nyumba katika kiwanja hicho.”
Alisema baada ya Nicodemus kujenga katika kiwanja cha Andrew, walishtakiana katika baraza la ardhi kijijini hapo ambalo liliwaagiza wazungumze wenyewe kwanza ili kuona kama wanaweza kufikia mwafaka.
“Kwa kuwa wote wako hapa Dar es Salaam ndipo jana wakaamua kuja kwangu kwa ajili ya kufanya kikao cha usuluhishi. Wao walifika saa 10 na baada ya ndugu wengine kufika saa 12 jioni ndipo tukaanza mazungumzo:
“Niliwasihi kuwa nikiwa baba yao mdogo ningefurahi kuona jambo hilo linamalizika kindugu,” alisema Pendaeli
Hata hivyo, alisema wakati wa mazungumzo hayo Nicodemus akamshutumu ndugu yake Nicodemus (wa Bunge) kuwa ndiye anayempa msaada binamu yake wa kifedha na kiushauri.
“Alikuja juu (polisi) na kuongea kwa hasira sana. Mimi baada ya kuona kuwa hakuna uelewano tena nilishauri kuwa ni vyema tuliachie baraza la ardhi liamue,” alisema Pendaeli na kuongeza:
“Nico wa Bunge na Andrew walikuwa upande mmoja na huyu askari na baadhi ya ndugu wengine walikuwa pia upande mmoja, hivyo wakaanza kupigana ngumi lakini watu wakawasihi wakaacha.”
“Lakini kabla ya kuondoka huyu askari akaomba maji, walipomletea akakataa glasi akanywea kwenye kidumu kile cha lita tano. Alipokunywa mara moja tu akapiga chini lile dumu kisha akakimbia hadi kwenye gari alimokuwa Nico wa Bunge akampiga risasi moja ya usoni kisha akamfuata Andrew akampiga risasi ya begani, wakati akikimbia akampiga risasi nyingine kiunoni, akaanguka na kufariki dunia,” alisema Pendaeli.
Baada ya matukio alisema watu wote walikimbia akiwamo askari huyo ambaye hata hivyo, alisema alikimbia kama mita 50 kutoka  nyumbani hapo kisha naye akajipiga risasi kifuani na kufariki dunia papohapo.
“Nilikwenda kutoa taarifa kituo cha polisi na askari walipofika na kumpekua mfukoni mwake (muuaji) wakakuta kikaratasi kilichosema: mtu yeyote asisumbuliwe kwa mauaji haya,” alisema Pendaeli.
Habari hii imeandaliwa na Sanjito Msafiri na Julieth Ngarabali, Kibaha, Aidan Mhando, James Magai

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

ALLY KAMWE AZIMIA KWA MKAPA.

RAIS SAMIA KUZINDUA MKUTANO MKUU WA 79 WA BARAZA LA MICHEZO YA MAJESHI DUNIANI

MIGINGO KISIWA KIDOGO ZAIDI AFRIKA KILICHOGOMBEWA NA UGANDA, KENYA