Rais Jakaya Kikwete (kulia) akisalimiana na Naibu Waziri Mkuu wa China, Hui Liangyu aliyewasili Ikulu, Dar es Salaam jana, kwa ziara ya kikazi ya siku tatu nchini.
Makamu Waziri Mkuu Wa China Kuzuru Zanzibar
Na Maelezo Zanzibar 05/09/2012
Makamu Waziri Mkuu wa China Hui Liang anatarajiwa kuwasili Zanzibar kesho Alkhamis kwa ziara ya siku mbili.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Wizara ya Nchi ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Tanzania,imeeleza kuwa mara tu atakapowasili uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Aman Karume atapokelewa na Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd.
Makamu Waziri Mkuu huyo kwenye uwanja huo atajulishwa na mwenyeji wake kwa viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakiwemo Mawaziri na pia kuvishwa Shada la Maua na kuangalia ngoma za Utamaduni wa Zanzibar.
Baadaye ataelekea Ikulu Zanzibar ambapo atakuwa na mazungumzo na Rais Wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohammed Shein na baadaye kutiwa saini makubaliano yatakayoshuhudiwa na Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd na Makamu Waziri Mkuu huyo wa China.
Usiku Makamu Waziri Mkuu wa China Hui Liang atahudhuria Chakula cha Usiku kilichoandaliwa kwa ajili yake na Mwenyeji wake Makamu wa Pili wa Rais huko Hotel ya Lagema.
Ijumaa atatembelea Mji Mkongwe ambapo ataanzia Kanisa la Anglicana Mkunazini na baadaye Beit el Ajaib na Jumba la Wananchi Forodhani na hatimaye kuelekea Uwanja wa Ndege kurejea Dar es Salaam.
Comments