Awamu
ya kwanza ya mazungumzo ya amani ya Syria itakamilika hii leo mjini
Geneva, bila ishara ya mafanikio lakini kuna 'matumaini' anasema mjumbe
wa umoja wa mataifa Lakhdar Brahimi.
Serikali ya Syria na waakilishi wa upinzani bado wana misimamo mikali juu ya maswala muhimu.
Lakini
mpatanishi wa Umoja wa Mataifa anayeongoza mazungumzo hayo anasema
anatumai awamu ya pili ya mazungumzo hayo itakayofanyika baada ya siku
kumi zijazo italeta mafanikio kiasi .
Siku
kumi baada ya umoja wa mataifa kuanzisha juhudi ya kumaliza vita wenyewe
kwa wenyewe nchini Syria wajumbe kutoka pande mbili katika mgogoro huo
bado wako kwenye meza moja ya mazungumzo.
Nwenyekiti
wa mazungumzo hayo, Lakhdar Brahimi, anazingatia hilo kuwa ufanisi wa
aina yake, huku akielezea kuwa kulikuwa na baadhi ya nyakati za hasira,
lakini pia nyakati za matumaini.
Kisha
akaelezea jinsi wajumbe wa pande zote mbili walipokubaliana kubaki kimya
kwa dakika moja kukumbuka nyoyo za wale waliofariki katika mapigano
nchini Syria.
"Tulikuwa
na nyakati za hasi hali kadhalika nyakati zenye matumaini. Upinzani
ulipendekeza tuwe na kimya cha dakika moja kuwaenzi waliokufa nchini
Syria, bila kuzingatia kambi wanayotoka na ujumbe wa serikali mara moja
ulikubali na kisha tukabaki kimya kwa dakika moja,'' amesema bwana
Brahimi.
Lakini
hapajakuwa na mafanikio makubwa katika mazungumzo kuhusu maswala muhimu
yanayoikabili Syria kama vile ugavi wa madarakani na kuruhusu misaada
ya kibinadamu kuingizwa katika maeneo yaliyozingirwa.
Hata mpangilio wa jinsi maswala haya yanapaswa kushughulikiwa umezua malumbano.
Bwana
Brahimi ana matarajio kuwa likizo ya siku kumi kwa wajumbe kuanzia baada
ya kikao cha mwisho leo Ijumaa, itatoa hewa safi kwa pande zote
kuzingatia mbinu bora zaidi za kushugulikia maswala hayo na pia kuwapa
fursa wafadhili wao-marekani na Urusi kutumia ushawishi wao.
Mawaziri
wa mashauri ya kigeni, John Kerry wa Marekani na mwenzake wa Urusi
Sergev Lavrov watakutana wikendi hii mjini Munich nchini
Ujerumani.Chanzo BBC Swahili
Comments