WATEJA WA NSSF DAR WATIMULIWA KWA MTUTU WA BUNDUKI


Na Mwandishi Wetu.

WATEJA wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), waliokwenda kumuona Meneja wa Tawi la Temeke ili wapatiwe ufumbuzi wa tatizo lao, wametimuliwa kwa mtutu wa bunduki kama majambazi.

Tukio hilo lililo wastaajabisha baadhi ya watu waliouwepo katika Jengo la NSSF Mafao House, Ilala, Dar es Salaam, limetokea leo mchana baada ya wateja hao kuruhusiwa na ofisa wa mapokezi kwenda kuonana na Meneja ili wawasilishe malalamiko ya kusoteshwa kupata taarifa ya madai yao ya pensheni kwa tatizo la kutokuwemo mtandao.

Wateja hao ambao wengi wao wanasema ni mara ya tatu au nne wamekuwa wakienda ofisini hapo kuhudumiwa, lakini maofisa wamekuwa wakiwapa majibu rahisi kwamba hawawezi kuhudumiwa kwa sababu hakuna mtandao.

Wateja hao walielekezwa kupanda lifti na kushuka M1, walipofika walimkuta dada mmoja mlinzi ambaye aliwauliza shida yao na kuelezwa ambapo aliwaambia wasubiri na kuingia ndani, aliporejea aliwaambia Meneja yupo lakini kamwambia awaeleze kuwa tatizo hilo ni la kawaida hivyo waondoke wajaribu tena kwenda kesho watapata huduma.

Wateja hao ambao baadhi yao waliachishwa kazi kutoka taasisi tofauti, walishindwa kumuelewa na kuhoji ni kwa nini Meneja ambaye ni mtumishi wa umma ashindwe kuja kuwasikiliza shida zao, bali anakatalia ofisini?

Walimueleza mlinzi huyo kuwa jibu alilowapa ni sawa na walililopatiwa na maofisa wengine, bali lengo lao ni kutaka majibu muafaka kutoka kwa meneja kuhusu ni lini tatizo la mara kwa mara kukosekana mtandao litapatiwa ufumbuzi? ili waondokane na kero ya kupoteza muda na nauli ya kila mara kwenda hapo.

Baada ya kuona hivyo mlinzi huyo wa kike akawaambia subirini, akaingia ofisini na kurudi na ofisa mmoja wa kike aliyewaangalia wateja hao kwa dharau na kuwahoji kuwa hivi kwa akili zenu mnafikiri kuja kwenu kwa Meneja ndo mtandao utarudi?

Kabla hawajamjibu ofisa huyo wa kike, walishangaa mlinzi yule wa kike kuja na askari wa kampuni binafsi ya ulinzi aliyevalia sare za bluu ambaye aliamriwa ofisa huyo kuwatoa wateja hao nje akidai hataki kuwaona hapo.

Askari baada ya kuambiwa hivyo, akaanza kuwaamrisha wateja kutoka nje huku akiwatishia kwa bunduki.

Wateja walionekana kutotishika ambapo baadhi yao walimjibu kuwa hawawezi kutoka kwani hawana hatia yoyote na hata ikiwezekana wako tayari kupigwa risasi.

Askari akazidi kuwa mbogo huku akiendelea kuwatishia kwa bunduki na kwenda kumkaba shingoni mmoja wa wateja, jambo ambalo lilizua taharuki na mzozo mkubwa huku wateja wakimuamuru askari amuachie mwenzao.

.
Baada ya mzozo kuwa mkubwa, alijitokeza ofisa mmoja wa NSSF na kuamulia huku akimuamuru askari aondoke eneo hilo na kuanza kuwatuliza wateja na kusikiliza malalamiko yao.

Ofisa huyo wa kiume ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja, alisikiliza kwa utulivu malalamiko yao  na kuwaeleza kuwa bahati mbaya Meneja hayupo ametoka muda mrefu kaenda kikazi mjini.

Lakini alikubali kulitatua tatizo hilo pamoja na kukubali ushauri wa wateja hao kuwa ili kuondoa usumbufu kwa wateja kwenda mara kwa mara katika ofisi hizo na kutopata huduma, basi waweke utaratibu wa kuorodhesha namba za kadi za wateja na namba zao za simu na kuziacha hapo zifanyiwe kazi na zikiwa tayari basi waarifiwe kwa simu kwenda kuchukua  taarifa za pensheni zao.

Pia walimweleza ofisa huyo kuwa matandao usipokuwepo kwa muda mrefu kaunta zinakuwa tupu bila maofisa, hivyo kuwawia vigumu wateja wanoingia kupata taarifa za mtandao kutokuwepo hali inayosababisha msongamano na kuwapotezea muda.

Baada ya kukubali ushauri huo, alishuka nao chini kwenye kaunta ambapo waliorodhesha majina, namba za kadi zao pamoja na namba za simu na kumuachia Ofisa aitwaye Seif na kuahidiwa kwenda Ijumaa kuchukua taarifa zao.

Lakini walipokuwa wakitoka nje ya Jengo la NSSF Ilala, wateja hao walibahatika kukutana na Meneja wa NSSF Tawi la Temeke, aliyejulikana kwa jina la Gurisha ambaye walimsimamisha na kumueleza kilichotokea ofisini kwake.

Gurisha alisikitika sana na kuwapa pole kwa kilichowasibu na kuwaahidi lalamiko lao kulifanyia kazi na kuwapatia namba yake 0756140201 ili kesho Alhamisi asubuhi wampigie simu waende kuchukua taarifa zao badala ya Ijumaa.

Baadhi ya wateja waliopatwa na mahasibu hayo ni Kodes Dimbwe, Said Kambangwa, Masudi Abillah,Emmanuel Kapungu, Hamis Shabani na Abdallah Nyamtwe.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

ALLY KAMWE AZIMIA KWA MKAPA.

RAIS SAMIA KUZINDUA MKUTANO MKUU WA 79 WA BARAZA LA MICHEZO YA MAJESHI DUNIANI

MIGINGO KISIWA KIDOGO ZAIDI AFRIKA KILICHOGOMBEWA NA UGANDA, KENYA