LRCT - MIFUMO YA SHERIA INAYODUMU MUDA MREFU INAWAVUTIA WAWEKEZAJI

Naibu Katibu Kitengo cha Elimu ya Sheria Kwa Umma Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania (LRCT), Zainabu Chanzi akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam Sabasaba Julai 9,2026.

............................ 

NA DOTO MWAIBALE 

NAIBU Katibu Kitengo cha Elimu ya Sheria kwa Umma Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania (LRCT),  Zainabu Chanzi amesema kuna umuhimu wa kuandaa mifumo ya kisheria ya muda mrefu bila ya kubadilishwa mara kwa mara jambo litakalo wasaidia wawekezaji kufanya shughuli zao bila ya kuwa na hofu.

Hayo ameyasema wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam Sabasaba Julai 9,2026.

‘’ Tunahitaji kuwa na mifumo ya kisheria ambayo itakaa muda mrefu bila ya kufanyiwa mabadiliko mara kwa mara,  wawekezaji wanahitaji kujiridhisha kisheria na ili kuendelea na biashara ukifanyika utafiti utaangalia maslahi ya wadau wote,’’ alisema Chanzi.

Alisema Julai 1, 2026 tume hiyo imeanza utekelezaji wa dira ya Taifa ya Maendeleo ya 20-50 na upo muda wa kutosha kuitekeleza hivyo sheria zetu lazima ziakisi matarajio makubwa ambayo dira hiyo imebeba.

Amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipokuwa akiizindua dira hiyo   aliipa tume yetu jukumu kubwa la kuhakikisha sheria zote zinaakisi matarajio yote ambayo yapo kwenye dira.

Chanzi amesema sheria ni nyenzo muhimu katika utekelezaji wa dira kama ambavyo tunasema tunahitaji uchumi jumuishi na shindani hivyo sheria itoe fursa na ziwezeshe katika maeneo mbalimbali.

Amesema ndani ya dira kuna sekta za  kimageuzi na sekta hizo huwezi kuona umuhimu na manufaa yake kama hazita saidiwa saidiwa zikafanya vizuri.

‘’ Katika kutekeleza maelekezo ya mhe. rais  tume kwa kushirikiana na taasisi nyingine kama vile Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Fedha na Tume ya Taifa ya Mipango tumeandaa jinsi ya kuendana na maboresho hayo,’’ alisema Chanzi. 

Amesema wameweza kufanya umbembuzi wa mifumo ya kisheria ambayo wataendanayo ili kuwezesha dira iweze kufanya kazi.

Chanzi amesema wameainisha mifumo 28 na watakayoanza nayo ni mifumo miwili, mfumo wa nishati.

‘’ Kama tunavyojua nishati ni kichocheo katika dira imewekwa wazi kabisa kwani tunataka kuwa na nchi yenye viwanda na sekta ya kimageuzi hivyo ili tuwe na viwanda ni lazima tuwe na nishati ya kutosha hivyo tutaangalia mfumo mzima wa sekta ya nishati,’’ alisema.

Aidha, alisema kuwa wanakwenda kuangalia mfumo wa kisheria unaosimamia biashara, viwanda na uwekezaji kwa sababu wanaamini sekta nyingine zote za kimageuzi kwa mfano ya kilimo, uchumi wa buluu, utalii, viwanda vyote hivyo vinawezesha ufanyikaji wa biashara.

Chanzi aliongeza kuwa watakapoenda kuangalia mfumo mzima wa ufanyaji wa biashara na sheria kwa kiwango gani imekuwa ni kikwazo na kuzipitia katika maeneo makubwa matatu zitaweza kuinua sekta hizo na hakutakuwa na kipingamizi hasa kwenye mazao ya biashara.

Amesema Sekta nyingine ni Utalii ambayo ni biashara na wanategemea kuwekeza kwa kuweka fedha za kutosha na kuifanya Tanzania kuwa kituo cha utalii na kuwafanya wafanyabiashara wakubwa kuja kuwekeza kwa kufungua mahoteli makubwa na ili mambo haya yaweze kufanyika ni kuwepo kwa sheria nzuri za kuvutia.

Amesema tafiti hizo zitaweza kusaidia utekelezaji wa dira hiyo na kuwa sekta nyingi zinahitaji sheria ambazo ni dhabiti na mifumo ya usimamizi ambayo ni rafiki na ya  kuwavutia wawekezaji, watekelezaji na wananchi kwa ujumla.

Chanzi alisema baada ya mifumo hiyo kupitiwa na sheria zikaandikwa Tume hiyo itarudi tena kutoa elimu kwa sababu wanaamini kwamba wakiwa na sheria nzuri kwenye vitabu na wananchi na wadau kwa ujumla hawazitambui, hawaelewi wajibu wao, haki zao watakuwa hawajafikia lile lengo hivyo watatoa elimu ya mabadiliko ya sheria yatakapotokea ili wazijue fursa na ndiyo maana wanasema uchumi jumuishi.

Alisema tume hiyo inaendelea na tafiti nyingine kwa mfano Akili Mnemba (AI) kwani tukiangalia kwenye dira  tunataka uchumi wa kidijitali na ndiyo uelekeo wa dunia nzima na Tanzania siyo kisiwa hivyo ni lazima kupitia sheria hizo kwa lengo la kuhakikisha AI zinaweza kutumika bila kuleta madhara. 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

DK MAGUFULI ATANGAZA KIAMA CHA MAJAMBAZI, WEZI NA MAFISADI KATIKA MIKUTANO YA KAMPENI SUMBAWANGA,TUNDUMA, ILEJE NA MBOZI

PICHA YA RAIS ILIYOBAMBA WIKI HII

JUA AINA NNE ZA KABILA LA WASUKUMA

18 WAPITISHWA KUGOMBEA UONGOZI YANGA

VIONGOZI BORA BARANI AFRIKA KWA SASA.

IJUE HISTORIA YA PACOME ZOUZOUA

ZIJUE SIFA ZA WANYAKYUSA WA KYELA NA RUNGWE