Rais Mstaafu Ashiriki Maadhimisho ya Miaka 50 ya Jumuiya ya Uingereza na Tanzania (Britain Tanzania Society)
Katika hatua nyingine ya ziara yake, Mheshimiwa Rais Mstaafu alishiriki katika hafla ya kuadhimisha miaka 50 ya Jumuiya ya Uingereza na Tanzania (Britain Tanzania Society – BTS), hafla iliyowakutanisha viongozi, wanadiplomasia na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka Tanzania na Uingereza.
Mheshimiwa Rais Mstaafu ni Rais wa Jumuiya hiyo tangu tarehe 9 Novemba 2024, akimrithi Hayati Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Ali Hassan Mwinyi, aliyewahi kuliongoza Jumuiya hiyo kwa heshima na mafanikio makubwa.
Miongoni mwa waliohudhuria hafla hiyo walikuwa Mheshimiwa Mberwa Kairuki, Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Uingereza, na Mheshimiwa Marianne Young, Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, pamoja na viongozi wengine na wadau wa sekta mbalimbali kutoka mataifa hayo mawili.
Maadhimisho hayo yalitoa fursa ya kutafakari mafanikio ya ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Uingereza katika kipindi cha miaka 50 iliyopita, hususan katika maeneo ya biashara, uwekezaji, elimu, afya, utalii, utamaduni na maendeleo ya kijamii. Vilevile, hafla hiyo ilisisitiza dhamira ya pande zote mbili ya kuendelea kuimarisha uhusiano wa kihistoria na ushirikiano wa kimkakati kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na Uingereza katika kipindi cha miaka 50 ijayo na kuendelea.








Comments