MBUNGE wa Chalinze ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, amekutana na kufanya kikao na Madiwani na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze kwa lengo la kujadili utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.
Kikao hicho kiliwakutanisha Madiwani, Watendaji wa Kata, Maafisa Tarafa, Wakuu wa Idara mbalimbali za Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze pamoja na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Ramadhani Possy.
Akizungumza katika kikao hicho, Kikwete alisema majadiliano hayo yamelenga kuweka mikakati ya pamoja na kubainisha majukumu ya kila upande katika utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.
Alisema utekelezaji wa Dira hiyo unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya viongozi wa kuchaguliwa, watumishi wa umma na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuhakikisha vipaumbele vilivyowekwa vinatafsiriwa katika mipango na shughuli zenye tija kwa wananchi.
“Kikao hiki kimetupa nafasi ya kujadili kwa pamoja majukumu na mipango ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050, ambayo itaiwezesha Halmashauri ya Chalinze kutoa mchango mkubwa katika ustawi wa Taifa kwa kuzingatia vipaumbele vilivyowekwa,” alisema Kikwete.
Alisisitiza umuhimu wa viongozi na watumishi wa Halmashauri ya Chalinze kufanya kazi kwa mshikamano, uwajibikaji na weledi ili kuhakikisha mipango ya maendeleo inatekelezwa kwa ufanisi na kuleta matokeo yanayotarajiwa.
Kikwete alisema Chalinze ina nafasi muhimu katika kuchangia utekelezaji wa malengo ya Taifa na kwamba ushirikiano wa taasisi mbalimbali utasaidia kuharakisha maendeleo na kuboresha huduma kwa wananchi.
Kikao hicho kinatarajiwa kuimarisha uratibu wa shughuli za maendeleo na kuongeza ushirikiano kati ya viongozi na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze katika kuelekea utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.
Comments