Kashfa Jeshi la Polisi

Mkuu Wa Jeshi la Polisi Nchini Saidi Mwema
............................................................

JESHI la Polisi nchini limeingia katika kashfa nyingine baada ya kijana Charles Patrick Paulo mkazi wa kijiji cha Mundemu wilayani Bahi mkoani Dodoma kulishushia tuhuma nzito za kupora fedha na kumbambikia kesi ya unyang’anyi.

Kesi hiyo iliyoendeshwa kasi ilimtupa jela miaka 15 kabla ya kuachiwa huru miezi sita baadaye baada ya kushinda rufaa.

Julai 20 mwaka jana, Paulo alitiwa hatiani na Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Mundemu F. Bulyota kwa shitaka la unyang’anyi kifungu namba 286 K/A Sura 16 na kutupwa jela kwa miaka 15.

Hukumu hiyo ilianzisha safari mpya ya maisha kwa kijana Paulo ambaye aliachana na maisha ya uraiani akimuacha mchumba wake, Upendo Masila akiwa na ujauzito wa miezi miwili huku
yeye akipelekwa katika Magereza ya Isanga kuanza kutumikia kifungo chake.

Lakini kwa vile alijua kuwa hukumu yake imetokana na uonevu wa Polisi, wiki moja baadaye kijana Paulo aliwasilisha rufani yake kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Dodoma akipinga hukumu hiyo, rufani ambayo ilizaa matunda Januari 26 mwaka huu, pale Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Dodoma, R.M Ngimilanga alipotoa hati ikiamuru
kijana huyo kuachiwa huru mara moja.

“Siku ya tarehe 20/07/2011 – Charles S/O Patrick Paulo Mshitakiwa katika jinai 52/2011 alifikishwa/ kutiwa hatiani mbele ya F.

Bulyota Hakimu Mahakama ya Mwanzo – Mundemu kwa shitaka la unyang’anyi K/F 286 K/A Sura 16, jela miaka kumi na mitano (15)... “Hati hii inakuamuru wewe Ofisa wa Gereza kumwachia huru Charles S/O Patrick Paulo.

Hati hii imetolewa kwa amri yangu na Mhuri wa Mahakama ya Wilaya leo tarehe 26/01/2012,” inasema hati hiyo ya kifungo baada ya rufaa ambayo inamfanya Paulo kurejea uraiani akimkuta mchumba wake Upendo akiwa tayari amejifungua mtoto Februari 2, mwaka huu, mtoto aliyebatizwa jina la Rogers.

“Mchumba wangu amejifungua lakini sijawahi kumuona mtoto wangu naogopa kwenda kijijini Mundemu maana polisi wanasema wanataka kunipoteza kwa kuniua najua wataweza kwani walinibambikia kesi ya unyang’anyi nikahukumiwa miaka 15 jela lakini Mungu amenisaidia nimetoka….lazima sasa niwe makini,” anasema kijana Paulo ambaye sasa amegeuka kuwa mkimbizi ndani ya nchi yake mwenyewe akiishi kwa kujificha jijini Dar es Salaam.

Mkasa wenyewe
Akizungumza katika ofisi za gazeti hili jijini Dar es Salaam, wiki hii Paulo anasema kisa na mkasa wa sakata lake na Jeshi la Polisi vilianzia katika kijiji cha Kongogo wilayani Bahi alikokwenda kufanya biashara ya mnadani akiuza mitumba na nyama ya ng’ombe.

Anasema baada ya kumalizika kwa mnada huo uliofanyika Desemba 12, 2010, alikwenda pembeni kidogo ya eneo la mnada kwenye kichaka na kujisaidia haja ndogo.

Anasema baadaye alitoa fedha zake Sh 470,000 taslimu alizokuwa nazo awali na Sh 150,000 za mauzo ya mitumba na kuzificha ndani ya bukta ili kuepusha kuibiwa.

“Mara baada ya kuzificha fedha zangu ndani ya bukta walikuja polisi wawili. Kwanza walinihoji kwanini najisaidia vichakani, nikawajibu mara nyingi sehemu za minada huwa tunafanya hivyo kutokana na ukosefu wa vyoo.

Hata hivyo walinipiga piga makofi mgongoni na kunitaka nipotee.

“Kwanza nilianza kukimbia kwa kwenda vichakani lakini baadaye nikashituka kwamba kule hakukuwa na usalama nikaamua kurudi nilipotoka lakini polisi wale walikuwa wakinikimbiza na pikipiki. Baadaye niliamua kusimama… walipofika waliniuliza kwanini narudi kule mnadani tena, nilitaka kuwajibu walinipiga na kitako cha bunduki nikaanguka na kupoteza fahamu.

“Nilipopata fahamu nilikuta wamenibeba kwenye pikipiki nikiwa katikati yao huku mkono wangu mmoja wakiwa wameufunga pingu ambayo ilikuwa pia imefungwa kwenye bomba la pikipiki. Niliwauliza walikuwa wananipeleka wapi…wakasema wanajua wao. Mwendo mfupi mbele waliniuliza kama waende na mimi au waniachie… niliomba waniachie, wakaniachia.”

Alisema baada ya kufika nyumbani (Mundemu) aliamua kwenda hospitali lakini alishindwa kutibiwa akiagizwa kwanza kuwa na fomu ya matibabu (PF 3) kutoka Polisi. Anasema baadaye alipewa fomu hiyo na kutibiwa.

“Baada ya matibabu nilianza kufuatilia suala hili. Nilianzia Polisi Mkoa kwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa (RPC), Ofisa Malalamiko wa Mkoa na hata Polisi Wilaya ya Bahi. Nilifuatilia mara nyingi sana lakini nilikuwa napigwa danadana huku na kule… wale polisi baada ya kuona nawafuatilia sana walianza vitisho na kuniambia watanibambikia kesi nifungwe nipotee.

“Baada ya kufuatilia sana baadaye Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Bahi (OCD) aliitisha gwaride la utambuzi kwa askari wake wote na nilifanikiwa kuwatambua askari walionipiga na kunipora
fedha. OCD alianza kufuatilia suala hilo kwa kunitaka nilete mashahidi na nilifanya hivyo mara kadhaa bila kupewa haki yangu.”

Alisema wakati akiendelea kufuatilia suala hilo, ghafla usiku wa Julai 18, kuamkia Julai 19, mwaka huu saa tisa usiku akiwa amelala nyumbani kwake walikuja watu kutoka ofisi ya Ofisa Mtendaji na kudai kuwa nimetajwa kuhusika katika tukio la uhalifu.

“Asubuhi Julai 29, 2011 nilipandishwa kizimbani nikasomewa mashitaka na nilimuona huyo mama anayesema nilimvamia nyumbani kwake usiku huo nikiwa na wenzangu watatu na kupora mali zake na fedha. Cha ajabu sikuona hao wengine ninaoambiwa nilikuwa nao. Nilipohoji walisema walikuwa wamenitambua mimi ingawa walisema tulikuwa tumevaa soksiusoni.

“Hakimu alinisomea mashitaka yangu na akamwambia mlalamikaji kuleta mashahidi wake. Mimi niliomba nipewe muda nilete mashahidi wangu kwa vile wengi walikuwa wamekwenda mnadani lakini kwa bahati mbaya kesho yake Julai 20, 2011 nilihukumiwa kifungo cha miaka 15 jela.

“Hata hivyo pamoja na kuhukumiwa lakini nilisikitishwa na hatua ya polisi waliokuwa wakinipeleka gerezani kwa pikipiki wakiwa na mgambo kunifunga pingu na kunining’iniza mtini porini na kuanza kunichapa fimbo wakisema ni kutokana na kunikomesha kwa kujifanya
mjanja,” alisema Paulo.

Akizungumzia madai hayo, Ofisa Malalamiko wa Polisi Mkoa wa Dodoma SSP Pancras Mdimi alikiri kupokea jalada la Paulo na kusema kuwa limerudishwa Polisi Wilaya ya Bahi ambapo kesi yake ilipoanzia.

Alisema kuwa, baada ya jalada hilo kuletwa likiwa halina hati ya mashtaka na nakala ya hukumu ambapo awali faili hilo liliitishwa baada ya mlalamikaji kuleta malalamiko yake. Mdimi alisema kuwa, hata mlalamikaji ambaye kwa sasa yuko Dar es Salaam alipotakiwakuleta mashahidi kuhusiana na malalamiko yake alisema kuwa hawezi kumudu kuleta mashahidi hao kutokana na gharama.

Hata hivyo alisema kuwa, watashughulikia madai ya mlalamikaji baada ya kupata faili kutoka Polisi Wilaya ya Bahi. "Mambo mengi yalikuwa hayajakamilika ndiyo maana faili lake halikushughulikiwa kabisa," alisisitiza Mdimi.

Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma Zelothe Stephen alipohojiwa na gazeti hili alimtaka Charles afuate utaratibu wakati shauri lake likishughulikiwa. "Afuate utaratibu aende pale kesi inapohusika kwa nini anatangatanga wakati shauri lake linashughulikiwa?" alihoji Kamanda Zelothe.

Alisema kuwa, ni vizuri kama mtu huyo angefuata utaratibu kusubiri hatma ya madai yake. Hata hivyo kijana huyo ameliambia gazeti hili hawezi kutokana na watuhumiwa katika shauri hilo kuwapo huko na anaogopa safari hii haitakuwa kifungo bali kifo.

Chanzo: Habari Leo Mtandaoni

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.