Walimu wazidi kuitilia ngumu Serikali

MUKOBA ASEMA WATAGOMA HATA BAADA YA LIKIZO, ASKOFU RUWA’ICHI ASEMA TUNAKOELEKEA SIKO
Waandishi wetu, Dar, mikoani
CHAMA cha Walimu Tanzania (CWT), kimetoa tamko kikisema hata kama shule zitafungwa wiki hii, mgomo utaendelea baada ya kufunguliwa endapo Serikali itakuwa haijatimiza madai yao.Tayari mgomo huo umesababisha athari kubwa katika mfumo wa utoaji elimu nchini kuanzia msingi na sekondari na jana, Rais wa CWT, Gratian Mukoba alisema Dar es Salaam kwamba mgomo huo hautaathiriwa na kufungwa kwa shule.

“Mgomo huu hauna ukomo, ni Serikali tu ndiyo itakayoamua uishe au uendelee. Tukipewa nyongeza tunazotaka utaisha lakini tusipopewa utaendelea milele,” alisema Mukoba. Jana ilikuwa ni siku ya tatu tangu kuanza kwa mgomo huo.

Alisema mgomo huo ni wa mafanikio makubwa, kwa sababu unahusisha asilimia 95 ya walimu... “Walimu wachache wanaoendelea kwenda shuleni ni waoga, wanafiki wenye kujipendekeza ili wapate vyeo na wanasaliti wenzao wanaodai haki zao,” alisema.

Rais huyo wa walimu alidai kuwa walimu hao wanaoendelea na kazi ndiyo wanaosababisha vurugu kwenye baadhi ya shule kwa sababu wao wamewaagiza walimu kubaki majumbani.

“Tunawaagiza walimu waendelee kubaki majumbani kwani wanaweza kusingiziwa na mwajiri kwamba wanawachochea wanafunzi kuandamana na kuharibu vifaa vya shule,” alisema.
Mukoba alisema mgomo huo ni halali na iwapo walimu waliogoma wataadhibiwa, chama kitafuata taratibu za kisheria kuwatetea wanachama wake.

Vitisho vya wakuu wa mikoa na wilaya
Rais huyo ametaka viongozi wa CWT na walimu waliokamatwa na kufunguliwa mashtaka, waachiliwe mara moja na kufutiwa mashtaka.

Mukoba alidai kwamba kuna viongozi na walimu ambao wamekamatwa katika Wilaya za Tarime, Rungwe, Kyela na Babati na kwamba kwenye Mikoa ya Pwani, Morogoro na Ruvuma, viongozi wa CWT wametishwa na wakuu wa mikoa na kamati za ulinzi na usalama za mikoa.

“Wakuu wa mikoa na wilaya waache kutumia madaraka yao kuwatisha walimu kwa kuwa wao siyo waajiri na mgogoro huu unawahusu walimu na waajiri wao,” alisema Mukoba.
Alisema vitisho vya dola havitasaidia kitu katika mgogoro huo bali, kutimiza madai ya walimu.

Ruwa’ichi: Tuendako siko
Katika hatua nyingine, Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki, Jimbo Kuu la Mwanza, Thadaeus Ruwa'ichi ameonya kuwa taifa ambalo linachezea elimu halitathaminika popote huku akisema madai ya walimu ni ya msingi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, muda mfupi baada ya kumaliza ibada ya misa takatifu ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Shule ya Msingi Nyakahoja ambayo inamilikiwa na Kanisa Katoliki, alisema hakuna taifa ambalo litathaminika duniani kwa kushindwa kuweka elimu kuwa kipaumbele.

Alisema kwa sasa Tanzania imekuwa ni nchi ya migogoro hali ambayo inaonyesha kuwapo kwa tatizo ambalo limetokana na kuzembea mahali fulani na kuonya kwamba isipowekwa sawa italeta tabu baadaye.
“Ni hatari taifa likishindwa kutimiza malengo ya kuwatendea haki watoto na familia... Sijapata kusikia popote watoto ambao wamefaulu kwenda sekondari wakati hawajui kusoma wala kuandika, hii ni aibu kwa taifa na fedheha kubwa,” alisema Askofu Ruwa'ichi.

Akizungumzia msimamo wa kanisa kuhusu mgomo huo wa walimu, alisema Serikali ni lazima ijifunze mazungumzo na maelewano na hayo lazima yazingatie haki na wajibu.

“Wanachogomea walimu ni masilahi, wanayo haki ya kupata masilahi mazuri yanayowawezesha kumudu maisha. Siyo vyema kuwaona wanapogoma kama ni wakorofi, hapana. Kama tumeona sawa wanasiasa wapate maslahi bora lakini walimu wanatizamwa tu, huku ni kuchezea elimu.”

“Sisi wakati tunasoma, mwalimu alikuwa mtu wa kuheshimika, lakini sasa tunathubutu kusema kwamba mtu anapofeli mahali kwingine kote tunaona aende kuwa mwalimu. Hili ni lazima tulibadili.”
Alisema ni vigumu kupata mhandisi bora, askofu mzuri na hata daktari bora iwapo waliofaulu vyema hawatachaguliwa kusomea na kuwa walimu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Goodluck Ole Medeye aliwaomba walimu kutumia njia za kisheria kudai madai yao badala ya kugoma kufundisha watoto kwa vile wanaoathirika ni wanafunzi.

Alisema mgomo huo umeanza wakati mbaya kwa vile kuna wanafunzi ambao wanajiandaa kumaliza elimu ya msingi, jambo ambalo linaweza kuharibu maisha yao ya baadaye na kuwa na athari kubwa kwa jamii.
Aliwasihi walimu kuangalia majaliwa ya wanafunzi ambao wanatarajia kuhitimu elimu yao ya msingi, kwa kufikiria upya njia ya kudai madai yao kisheria.

Dar hali bado tete
Mkoani Dar es Salaam, hali bado ni mbaya kwani walimu katika shule nyingi bado wameendelea na mgomo.
Katika Manispaa ya Ilala baadhi ya shule za msingi na sekondari zilizoathirika na mgomo huo, za Mnazi Mmoja yenye wanafunzi wa msingi na sekondari, Lumumba na Kidongo Chekundu, Kata ya Jangwani, madarasa yake yalikuwa yamefungwa.

Waandishi wetu walishuhudia baadhi ya madarasa katika Shule ya Msingi Lumumba yakiwa yamegeuzwa vituo vya kuandikisha Vitambulisho vya Taifa.

Baadhi ya wanafunzi katika shule hizo walidai wanakosa masomo huku wakiilaumu Serikali kwa kutochukua hatua madhubuti na mapema kutatua suala hilo.

Walimu nchini wamegoma wakidai nyongeza ya mishahara ya asilimia 100, asilimia 50 ikiwa ni posho kwa wale wanaofundisha masomo ya sayansi, asilimia 50 kwa masomo ya sanaa na kwa walimu wanaofundisha katika mazingira magumu wanataka wawe wanapewa nyongeza ya asilimia 30 ya mshahara.
Raymond Kamnyoge, Mashamba Badi, Zakhia Abdallah, Elizabeth Edward, Dar na Frederick Katulanda, Mwanza,

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.