BRANDTS NI KIPIMO KINGINE CHA MAHUSIANO YA YANGA NA MAKOCHA, SHAURI YAO

Brandts kulia akisaini mkataba na Yanga. Kushoto ni Sanga akisaini kwa upande wa Yanga

YANGA SC, jana imeingia mkataba wa mwaka mmoja na kocha Ernstus ‘Ernie’ Wilhelmus Johannes Brandts, wiki moja tangu imfukuze Mbelgiji, Tom Saintfiet aliyeitumikia klabu hiyo kwa siku 80 tu.
Na Mahmoud Zubeiry
Akizungumza wakati wa kusaini mkataba huo jana, Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Clement Sanga alisema kwamba wamepata kocha mzoefu wa soka ya Afrika ambaye amefanya kazi APR ya Rwanda.
“Tulikuwa na makocha wengi katika mchakato, tumekuwa makini kutokana na matatizo yaliyojitokeza awali, tumekuwa makini na aina ya mikataba tunayoingia na makocha, ili tusije tukarudia makosa, tumezungumza naye matatizo yaliyotokea na kocha aliyemtangulia, ameridhika, ameona tuko sahihi, naye amesema yuko tayari kutimiza masharti ya mwajiri wake mpya,”alisema Sanga.
Beki huyo wa zamani wa kimataifa wa Uholanzi na klabu ya PSV Eindhoven ya Holanzi, aliwasili juzi majira ya saa 3:45 usiku katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere na ndege ya KLM na kupokewa na Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako na viongozi wengine, Abdallah Ahmad Bin Kleb, Seif Ahmad ‘Magari’ na Majjid Suleiman.
Yanga, imetimiza malengo yake ya kuwa kocha mpya, kabla ya kucheza na wapinzani wao wa jadi, Simba SC, Oktoba 3, mwaka huu baada ya kumfukuza Mbelgiji, Tom Saintfiet, kutokana na kuwasili kwa Brandts, ambaye ataanza kazi mara moja leo.
Kikosi cha Yanga kipo kambini, hoteli ya Uplands, Changanyikeni, Dar es Salaam na kabla ya kucheza na Simba Jumatano, kesho kitacheza na African Lyon, Uwanja wa Taifa pia.
Baada ya kusaini mkataba, kocha huyo alisema kwamba atajitahidi kadiri ya uwezo wake, kuhakikisha anaiongoza timu hiyo kushinda mechi ya Jumatano dhidi ya watani wao wa jadi, Simba SC ingawa anajua utakuwa mtihani mgumu.
Alisema kwanza anaushukuru uongozi wa klabu hiyo kuwa kumuamini, na anaafiki kwa kiasi kikubwa kupewa nafasi ya kurithi mikoba ya Mbelgiji, Tom Saintfiet, aliyetupiwa virago wiki iliyopita, baada ya kuitumikia Yanga kwa siku 80.
“Muhimu kwangu, nitajitahidi kadiri ya uwezo wangu kuipa matokeo mazuri klabu kwa asilimia mia moja. Nilikuwa Uholanzi, nikapigiwa simu na Mwenyekiti, Yussuf Manji, akaniambia anataka nije kufanya kazi Yanga, nilikuwa nina ofa nyingi, ila nilivutiwa naye (Manji), aliponiambia falsafa na sera za klabu, anataka kuindeleza klabu.
Kitu kingine ni kuhusu timu, kama kocha, kweli tuntaka kushinda kila mechi, lakini tunataka kucheza soka ya kuvutia. Jambo muhimu kwangu ni kufanya kila mchezaji mmoja mmoja acheze vizuri, na timu icheze vizuri, kwa sababu hakuna bora zaidi ya timu,”alisema.
Brandts pia alizungumzia nidhamu, akisema; “Kuzingatia nidhamu, ni muhimu si hapa tu Afrika, hata Asia na Ulaya kwa sababu, ukitaka kuamka saa moja kamili amka saa moja kamili na ukitaka kujenga timu nzuri, muhimu kujituma, hata mimi nilipokuwa nacheza ilikuwa hivyo pia, ni muhimu kujivunia timu unayochezea na kila mchezaji anatakiwa kujivunia kuchezea Yanga,”alisema.
Kuhusu kazi, alisema; “Kitu kingine, kuna mechi kesho na kuna mechi Jumatano, dhidi ya Simba itakuwa ngumu sana, tutafanya kila tunachoweza kuhakikisha tunashinda, naijua Yanga nimekuja hapa miaka miwili, ni timu nzuri. Sasa nakwenda kujaribu kuboresha timu, najiona mwenye bahati kusaini mkataba na timu hii,”alisema.
Brandts alikuja mwaka jana na mwaka huu kwa ajili ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, akiwa na APR ya Rwanda na mara zote, Yanga iliibuka bingwa, mwaka jana ikifundishwa na Mganda Sam Timbe na mwaka huu ikifundishwa na Mbelgiji, Saintfiet.
Mwaka jana, APR ilitolewa mapema katika kundi lake Morogoro, lakini mwaka huu ilifika hadi Nusu Fainali na kutolewa na Yanga. 
Mholanzi huyo aliyeifundisha APR ya Rwanda tangu 2010, hakuongezewa mkataba baada ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame, Agosti mwaka huu amepewa ukocha wa Yanga, baada ya Mbrazil Marcio Maximo kukataa nafasi hiyo kwa mara ya pili.
Mtaalamu huyo, alizaliwa Februari 3, mwaka 1956 mjini Nieuw-Dijk, Gelderland, mbali na PSV Eindhoven, alichezea pia Roda JC Kerkrade, MVV Maastricht na De Graafschap.
Brandts aliichezea mechi 28 timu ya taifa ya Uholanzi na kuifungia mabao matano na pia alicheza Fainali za Kombe la Dunia mwaka 1978.
Katika fainali hizo, Raundi ya pili kwenye mechi na Italia, aliweka rekodi ya kuwa mchezaji pekee aliyezifungia mabao timu zote katika mechi moja kwenye fainali za Kombe la Dunia.
Alianza kujifunga dakika ya 18, kisha akaisawazishia Uholanzi dakika ya 50 katika mechi ambayo, mchezaji mwenzake Arie Haan baadaye aliifungia timu yake bao la ushindi na kutoka kifua mbele kwa mabao 2–1.
Alipostaafu soka akawa kocha na katikati ya msimu wa 2007–2008, Brandts aliambiwa hataongezewa mkataba NAC-Breda, licha ya matokeo mazuri ya kushika nafasi ya tatu katika Ligi Kuu Uholanzi (Eredivisie), ingawa uamuzi huo haukuwafurahisha mashabiki wa timu hiyo na nafasi yake akapewa Robert Maaskant kuanzia msimu wa 2008–2009.
Akateuliwa kuwa Kocha wa Rah Ahan mwaka 2009, kabla ya kufukuzwa Desemba 2009 na kuibukia APR ya Rwanda mwaka 2010, ambako ‘riziki’ yake imeisha miezi miwili iliyopita na sasa amepata maisha mapya Yanga.
Akiwa APR, Brandts alifungwa mechi zote mbili na Yanga iliyokuwa ikifundishwa na Mbelgiji Tom Saintfiet katika Kombe la Kagame, moja ya makundi 2-0 na nyingine ya Nusu Fainali 1-0. Yanga iliibuka bingwa, ikiifunga Azam FC 2-0 kwenye fainali.
Brandts atakutana na wachezaji wake wa zamani wawili Yanga, beki Mbuyu Twite anayeanza msimu wa kwanza katika klabu hiyo na kiungo Haruna Niyonzima anayeingia katika msimu wa pili, ambao alifanya nao kazi APR.
Brandts anakuwa kocha wa 19 kuifundisha Yanga, tangu mwaka 1991, na katika kipindi chote hicho ni makocha watatu tu, waliorudishwa kazini, baada ya kuondoka, ambao ni Syllersaid Mziray (sasa marehemu), Mmalawi Jack Chamangwana na Mserbia Kostadin Papic.
Baadhi ya makocha waliamua kuondoka wenyewe, lakini wengi wao walifukuzwa na tawala mbalimbali zilizopita katika klabu hiyo katika kipindi chote hicho.
Kwa nini nimeanzia 1991, ndicho kipindi ambacho vurugu vurugu za kufukuza makocha zilipoanza katika klabu hiyo, tofauti na miaka ya nyuma tangu kuanzishwa kwa klabu hiyo mwaka 1939.
Mapema mwaka 1991, Yanga ilimchukua kocha maarufu zamani nchini, Syllersaid Salmin Kahema Mziray, ambaye aliondoka kwa watani wa jadi, Simba SC, baada ya kushushwa cheo kutoka Simba A hadi Simba B.
Mziray aliiongoza Yanga kwa miaka miwili, akiwa anasaidiwa na Charles Boniface Mkwasa na akaiwezesha kutwaa ubingwa wa Bara na Muungano mfululizo, sambamba na kuwafikisha Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati, ambako walifungwa kwa matuta na watani wa jadi, Simba SC.
Lakini baada ya hapo, marehemu Mziray aliondoka Yanga kutokana na kupata ofa nzuri kutoka Pan African, wakati huo ikiwa inafadhiliwa na Murtaza Dewji, ambaye alikuwa anaipigania irejee Ligi Kuu.
Yanga iliajiri tena kocha wa kigeni baada ya muda mrefu, ikimleta Mrundi, Nzoyisaba Tauzany ‘Bundes’ 1993 (sasa marehemu) ambaye aliendelea kufanya kazi na Mkwasa na katika mwaka wake wa kwanza, akaiwezesha timu hiyo kutwaa Kombe la Kagame mjini Kampala, Uganda.
Tauzany aliporejea katika Ligi Kuu akaendelea vizuri na kazi, lakini haikuchukua muda akaingia kwenye mgogoro na mfadhili wa klabu hiyo wakati huo, Abbas Gulalamli (sasa marehemu).
Tauzany alitumia vyombo vya habari kupambana na Gulamali na ilifikia hadi akawa anachafua jina lake kwa kusema anafanya biashara haramu. Ilikuwa vita kali na mbaya zaidi hata Mrundi hiyo alikuwa anakubalika mbele ya wanachama, hivyo kumfukuza ikawa tabu.
Alichokifanya Gulamali, akamrejesha kocha ambaye alifanya kazi na kupendwa mno Yanga, Tambwe Leya kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ambaye awali alifanya kazi mwaka 1975 na 1976, akiiwezesha Yanga kuifunga Simba katika mechi ya kihistoria Nyamagana kabla ya kuipa Kombe la kwanza la Kagame 1975, kwa kuwafunga hao hao Simba 2-0 Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Tambwe alitua nchini mwishoni mwa mwaka 1994 na jukumu lake alilopewa ni Ukurugenzi wa Ufundi, ambapo yeye akaamua kutengeneza timu nzuri ya vijana, iliyopewa jina Black Stars.
Tauzany na kikosi cha Yanga chenye mastaa kibao nchini wakati huo, akafungwa mabao 4-1 na Simba SC na hapo ndipo timu nzima na kocha wao wakafukuzwa, wakabaki wachezaji saba tu ambao waliunganishwa na yosso wa Tambwe kutengeneza kikosi kipya, kilichofanya vizuri hadi kufika Robo Fainali ya Kombe la Washindi 1996.
Tambwe naye akaondolewa kwa visa na badala yake akaajiriwa kocha mzalendo, Sunday Burton Kayuni 1997 ambaye naye pia hakudumu, kwani alikfukuzwa na akaajiriwa kocha wa muda kutoka Uingereza, Steve McLennan mwaka huo huo 1997.
McLennan, kocha Mzungu wa kwanza mimi kufanya naye kazi Yanga, aliondolewa naye na nafasi yake akakaimu kwa muda aliyekuwa Msaidizi wake, Juma Pondamali ‘Mensah’.
Siwezi kusahau siku alipofukuzwa McLennan, alimfuata msaidizi wake ambaye aliachiwa timu na kumuuliza; “Juma nani ni kocha mzuri, mimi au wewe?” Pondamali akawa anacheka tu, wapo kwenye basi timu inatoka Zanzibar kwenye mechi za Ligi ya Muungano. 
Yanga ikaajiri kocha wa muda, ambaye alikuwa hajulikani kabisa, Tito Oswald Mwaluvanda (sasa marehemu) ambaye katika kujikosha kwa wanachama, aliyekuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo wakati huo, Rashid Ngozoma Matunda (sasa marehemu pia) akawa anamtambulisha kama Msimamizi wa mazoezi, wakati timu inatafuta kocha. Msimamizi wa mazoezi alichukua ubingwa wa Ligi Kuu na Ligi ya Muungano 1998, tena akiweka rekodi ya ushindi mnono zaidi katika Ligi ya Bara, mabao 8-0 waliyoifunga Kagera Shooting Stars (sasa Kagera Sugar), tena ikiwa inafundishwa na kocha wa timu ya taifa, Taifa Stars wakati huo, Zacharia Kinanda ‘Arrigo Sachi’ (sasa marehemu), Edibilly Jonas Lunyamila akifunga mabao matano peke yake. Mungu amrehemu Kinanda, lakini siku hiyo Lunyamila alimfikishia ujumbe, kwani kocha huyo alikuwa hamtaki Eddy katika timu ya taifa- hivyo zile bao tano alizofunga ilikuwa ujumbe tosha, kwamba alikuwa anakosea.
Kana kwamba hiyo haitoshi, Mwaluvanda aliifikisha Yanga hadi hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa, akiweka rekodi mbili kuifanya hiyo iwe klabu ya kwanza Tanzania kucheza hatua hiyo, yeye kuwa kocha wa kwanza mzalendo na wa mwisho hadi sasa kuifikisha timu katika hatua hiyo.
Lakini pamoja na yote, mwaka 1998 mara tu baada ya Yanga kuingia hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa, marehemu Mwaluvanda aliyekuwa anasaidiwa na Freddy Felix Isaya Kataraiya Minziro ‘Majeshi’ wakaondolewa wote na akaajiriwa kocha kutoka DRC, Raoul Jean Pierre Shungu aliyeingia na msaidizi wake, Abeid Mziba ‘Tekero’.
Hii ilimuuma sana Mwaluvanda, kwa sababu ili kuingia hatua ya makundi ilibidi azitoe Rayon ya Rwanda iliyokuwa inafundishwa na Shungu na baadaye Coffee ya Ethiopia, lakini marehemu akawa anasema afadhali angeletwa kocha mwingine, si yule ambaye ameitoa timu yake kwenye mashindano. Wakubwa wakishaamua huwezi kupingana nao.
Shungu aliipa Yanga Kombe la tatu la Kagame, katika michuano iliyofanyika mjini Kampala, Uganda 1999, lakini mwaka 2000 akaondolewa na akaajiriwa Charles Boniface Mkwasa ‘Master’, ambaye naye mwishoni mwa mwaka 2001, akatupiwa virago pia.
Tangu 2002 hadi sasa ni miaka 10 tu, lakini katika kipindi hicho Yanga imefundishwa na makocha 11, tena wengine wakifukuzwa na kurudishwa kwenye kipindi hicho.
Alipoondolewa Master Mkwasa, akaajiriwa Mmalawi Jack Lloyd Chamangwana ambaye mwaka 2003, alifukuzwa na mwaka 2004 akaajiriwa kocha kutoka DRC, Jean Polycarpe Bonghanya ambaye naye hakudumu, mwaka huo huo akaondolewa na kurudishwa Syllersaid Mziray. Marehemu Mziray alikuwa anasoma ishara za nyakati tu, naye alipoona upepo unaelekea kuwa mbaya akamuachia timu aliyekuwa Msaidizi wake, Kenny Mwaisabula.
Mwaisabula akaendelea na kazi hadi msimu wa 2005, lakini baadaye mwaka huo akaondolewa na kurejeshwa Chamangwana., ambaye alifanya kazi hadi 2007 alipompsha Mserbia, Milutin Sredojevic ‘Micho’.
Micho aliondoka kwa sababu ambazo hadi leo bado hazieleweki, kwani alikubalika na timu ilikuwa inafanya vizuri. Alipoondoka Micho, timu akabakia nayo, aliyekuwa kocha wa makipa, Mkenya Razack Ssiwa.
Ssiwa akaiongoza Yanga kutwaa Kombe la Tusker mwaka 2007 mjini Mwanza, lakini aliporudi kwenye ligi, timu inafanya vibaya, naya akatupiwa virago na kurejeshwa Chamangwana.  
Chamangwana naye akaondolewa na kuajiriwa tena Mserbia, Profesa Dusan Savo Kondic, aliyekuja na Wasaidizi wawili, Spaso Sokolovoski na Civojnov Serdan. Kondic naye mwaka 2010 akafukuzwa na kuajiriwa Mserbia mwenzake, Kostadin Papic, ambaye naye alifukuzwa na kuajiriwa Mganda Sam Timbe.
Timbe pamoja na kuipa timu Kombe la nne la Kagame mwaka jana, alifukuzwa miezi miwili baadaye na kurejeshwa Papic, ambaye pia hata kabla msimu uliopita wa Ligi Kuu haujamalizika, akatupiwa virago na kuajirwa Mbelgiji, Saintfiet.
Saintfiet amehitimisha historia yake Yanga ndani ya siku 80, akicheza mechi 14, akishinda 12, sare moja na kufungwa  mbili- huku akiacha Kombe la tano la Kagame Yanga na sasa anakuja Mholanzi Brandts kufungua ukurasa mpya. Kweli makocha wanaamini, wanaajiriwa ili wafukuzwe, lakini bado huu si msemo wa kuuftaisha sana, kwani soka soka ni mchezo wa kitalaamu, ambao unahitaji wataalamu kupewa muda wa kufanya kazi.
Sanga amesema wamemueleza Brandts matatizo yao na kocha aliyepita, naye amewaona wako sahihi na ameahidi kutekeleza matakwa ya mwajiri wake. Hii nzuri sana. Hiki ni kipimo kingine kwa Yanga juu ya mahusiano yake na makocha. Kwa hisani ya Bin Zubeiry Blog
MAKOCHA YANGA TANGU 1991
1.  1991: Syllersaid Mziray(marehemu)
2.  1993: Nzoyisaba Tauzany (marehemu) (Burundi)
3.  1995: Tambwe Leya (marehemu) (DRC)
4.  1997: Sunday Kayuni
5.  1997: Steve McLennan (Uinegereza)
6.  1998: Tito Mwaluvanda(marehemu)
7.  1999: Raoul Shungu (DRC)
8.  2001: Charles Boniface Mkwasa
9.  2002: Jack Chamangwana (Malawi)
10.       2004: Jean Polycarpe Bonganya (DRC)
11.       2004: Syllersaid Mziray (marehemu)
12.       2005: Kenny Mwaisabula
13.       2006: Jack Chamangwana (Malawi)
14.       2007: Milutin Sredojevic ‘Micho’ (Serbia)
15.       2007: Razack Ssiwa (Kenya)
16.       2007: Jack Chamangwana (Malawi)
17.       2008: Dusan Kondic (Serbia)
18.       2010: Kostadin Papic (Serbia)
19.       2011: Sam Timbe (Uganda)
20.       2011: Kostadin Papic (Serbia)
21.       2012: Tom Saintfiet    (Ubelgiji)
22.       2012: Ernie Brandts (Uholanzi)

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI