KABILA IAKUMBUKA TANZANIA KWA AMANI

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) Joseph Kabila akizungumza na waandishi wa habari wa Tanzania katika Ikulu ya nchi hiyo kuhusu mambo mbalimbali aliyoweza kufanya tangu alipoingia madarakani baada ya kifo cha baba yake Laurent Kabila. Picha na Boniface Meena  

RAIS wa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Joseph Kabila ameikumbuka Tanzania na kusema kuwa harakati za kuikomboa nchi yao walizifanya nchini humo kama walivyofanya baadhi ya marais wengine wa Afrika.
Rais Kabila alisema hayo jana Ikulu mjini Kinshasa wakati alipokuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari wa Tanzania walioko nchini Congo kwa ziara ya siku tano ya kikazi.
Alisema yeye binafsi amewahi kuishi maeneo mengi ikiwa ni pamoja na Nairobi nchini Kenya, Kampala nchini Uganda na Dar es Salaam nchini Tanzania.
“Tanzania ni nchi ambayo ilitukaribisha wakati tukiwa katika harakati zetu kama ilivyofanya kwa Samora Machel, Joachim Chissano na wengine,”alisema Rais Kabila.
Hata hivyo pamoja na kueleza hayo Rais Kabila hakutaka kuelezea kama Serikali ya Tanzania iliwasaidia vipi kuhakikisha wanaikomboa nchi ya Congo kutoka kwa Rais wa zamani wa nchi hiyo Mobutu Seseko.
“Kuhusu  kama  tulisaidiwaje hilo ni jambo ambalo siwezi kulizungumzia hapa, nikija Dar es Salaam ninaweza kuwaeleza na hata kuwaonyesha niliishi maeneo  gani katika jiji la Dar es Salaam,”alisema Rais Kabila.
Alisema kitu muhimu ambacho anakumbuka kuhusu Tanzania ni kwamba ni nchi yenye amani na utulivu.
Akizungumzia mikakati mbalimbali ya Serikali yake na changamoto katika kuijenga nchi ya Congo,  Rais Kabila alisema hivi sasa wameweza kuibadilisha nchi hiyo na kuwa nchi inayoweza kukalika kwa amani isipokuwa eneo moja tu la Mashariki ambalo limekuwa na vita kila wakati.
“Suala la vita Mashariki ni matatizo ambayo tumeyarithi na kwamba yako kuanzia miaka ya 60 lakini vile vita vingine tulivyokuwa navyo nchini viliisha mwaka 2009 , hivi sasa tunajitahidi kuleta amani Mashariki ya Congo,”alisema Rais Kabila.
Alisema ukosefu wa amani katika eneo hilo unasababishwa na nchi jirani hasa Rwanda hivyo wanajitahidi kuhakikisha hilo lina kwisha kwa njia ya mazungumzo.
“Hivi sasa lengo letu kubwa ni kufikia amani ya kudumu kwa kuzungumza. Sasa muda umefika kwani tunachotaka ni amani,”alisema Rais Kabila.
Alisema amekutana na viongozi wote wa Jumuiya ya Afrika Mashariki(EAC), ili kuweza kuhakikisha amani katika eneo la Mashariki ya Congo inapatikana kwa mazungumzo na si vinginevyo. Chanzo Mwananchi

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI

KOCHA WA AL.AHLY ASEMA YANGA NI TIMU BORA NA NGUMU