VURUGU KUBWA ZAZUKA ARUSHA, LINDI

  Askari wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) wakiwa tayari kukabiliana na wanafunzi wa Chuo cha Uhasibu Arusha, waliokusanyika wakilalamikia kuuawa kwa mwenzao juzi usiku.PICHA NA MUSA JUMA 

Liwale/Arusha. Uharibifu mkubwa wa mali ulifanywa juzi usiku
 Mjini Liwale, Lindi baada ya wananchi wenye hasira kuchoma moto nyumba za viongozi waandamizi, makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya na maghala ya mazao kutokana na kuchukizwa kushushwa kwa bei ya korosho.
Nyumba zilizochomwa moto ni za Mbunge wa Liwale (CCM), Faith Mtambo, Mwenyekiti wa Chama cha Msingi cha Umoja, Hassan Myao na Makamu wake, Hassan Mpako, Diwani wa Viti Maalumu (CCM) Liwale, Amina Mnocha, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Liwale, Abbas Chigogola ambaye pia ng’ombe wake tisa walikatwakatwa mapanga na kuachiwa ndama watatu.
Nyingine ni nyumba ya Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Liwale, Mohamed Ng’omambo, Katibu Mwenezi wa CCM Mkoa wa Lindi, Mwenyekiti wa Chama cha Msingi Minali, Mohamed Limbwilindi na Katibu wa chama hicho, Juma Majivuno.
Wakati hayo yakitokea Lindi, huko Arusha, vurugu kubwa za wanafunzi wa Chuo cha Uhasibu zilizuka jana baada ya kuuawa kwa mwanafunzi Henry Kago (22), juzi usiku.
Kago, ambaye alikuwa mwanafunzi wa mwaka wa pili, anadaiwa kuwa alifariki juzi saa nne usiku baada ya kuchomwa kisu na watu wasiojulikana, akiwa njiani eneo la Kanisa la Wasabato akitokea chuoni hapo kujisomea.
Ghasia za Liwale
Ghasia hizo zilianza juzi mchana katika Kijiji cha Liwale B na ziliendelea usiku kucha hadi jana asubuhi.
Watu walioshuhudia ghasia hizo walisema chanzo ni wakulima kudai kulipwa Sh600 na siyo Sh200 za mauzo ya korosho kwenye Chama cha Msingi Minali.
Bei ya kilo moja ya korosho waliyokubaliana wakulima na chama hicho ni Sh1,200 na mara ya kwanza kiliwalipa Sh600 kwa kilo na kuahidi kulipa nusu nyingine baadaye.
Hata hivyo, viongozi wa Ushirika walibadili uamuzi na kulipa Sh200 kwa maelezo kuwa mauzo hayakuwa mazuri kitendo ambacho kiliwakasirisha wakulima hao ambao waligoma kupokea fedha hizo.
Baadaye ilielezwa kuwa viongozi wa Minali walipeleka fedha hizo polisi ili malipo yafanyike huko, lakini ghasia zikaibuka na wakaamua kusitisha malipo hayo na ndipo wananchi wakaamua kuingia mitaani.
Mmoja wa mashuhuda alisema “Polisi walijaribu kuwadhibiti watu hao, lakini walipoona wanazidiwa nguvu, wakawaachia wafanye wanavyotaka ndiyo maana kumekuwa na uharibifu mkubwa.”
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Lindi, George Mwakajinga alisema kwa kifupi: “Hali imetulia na vurugu zimemalizika lakini bado tuko kwenye kikao kuzungumzia suala hili.”

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI