ZITTO AZIBANA TRA,TPA



Na Neema Mgonja
KAMATI ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), imelazimika kuunda kamati ndogo kuchunguza sakata la kuondolewa kwa mashine za kupimia mafuta yanayoingia nchini kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Hatua hiyo imefikiwa jana baada ya kamati hiyo kushindwa kupata majibu ya kuridhisha kuhusiana na sakata hilo kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Wakala wa Vipimo (WMA).
Awali viongozi wa TRA, TPA na WMA walionekana kujikanganya katika maelezo yao  hali iliyozua utata miongoni mwa wajumbe wa kamati hiyo.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Kabwe Zitto, ndiye aliyeanza kuhoji sababu ya kusitishwa matumizi ya mashine hizo ambazo zilikuwa zikitumiwa kupima kiasi cha mafuta yanayoingia nchini kupitia bandari hiyo, na majibu yake kutumika katika kutoza kodi.
Akijibu suala hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa TRA, Harry Kitilya, alisema suala hilo lipo mikononi mwa WMA kwani ndiyo waliyotoa agizo la mashine hizo kutofanyakazi tangu Februari 2, 2011.
Akitoa ufafanuzi wa jambo hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa WMA, Magdalena Chuwa, alisema ofisi ilitoa kibali cha kusitisha matumizi ya mashine hizo baada ya kubaini  hazifanyikazi kwa ufanisi.
Chuwa alisema zilivyofungwa mwaka 2004, WMA haikushirikishwa, lakini ilitoa kibali cha kuendelea kufanyakazi.
Alisema mwaka 2010 WMA ilipokea malalamiko mbalimbali kutoka kwa TRA na wafanyabiashara wa mafuta waliokuwa wakilalamikia mashine hizo kuwa zinahujumu.
Alisema baada ya malalamiko aliandika barua ya kuzifungia kwa vile zilikuwa hazitendi haki kwa sababu kuna wakati zinazidisha kiwango cha kodi na mara nyingine kupunguza.
Kauli hiyo ilianza kupingwa na wajumbe wa kamati hiyo, ambao walitaka ufafanuzi kutoka TPA kuhusiana na mashine hizo zilizofungwa katika bandari yao.
Hata hivyo, viongozi wa TPA walionekana kukwepa jambo hilo wakieeleza kuwa haliko mikononi mwao bali linaihusu TRA ambayo ndiyo inayokusanya kodi kupitia mashine hizo.   Majibu hayo  yalimuibua Makamu Mwenyekiti, Deo Filikunjombe aliyemtaka Chuwa kufafanua vyema jambo hilo kwa kuwa kuna kumbukumbu zinazoonesha aliandikiwa barua ya kuitwa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), lakini hakwenda.
Ilielezwa katika barua hiyo kuwa Chuwa alitakiwa kukutana na CAG pamoja na wawakilishi wa TRA na TPA kujadili suala la mashine hizo, lakini hakutoa taarifa ya kutofika kwake.
“Tuna maelezo ya CAG hapa kuwa uliitwa katika kikao cha pamoja wewe pamoja na TRA na TPA ili kujadili jambo hili, lakini haukufika kwenye kikao, unaweza kueleza sababu ya kutokwenda kwenye kikao hicho?” alihoji Filikunjombe.
Akitoa maelezo juu ya suala hilo, Chuwa alikiri kupata barua ya wito, lakini hakwenda kwenye kikao na badala yake alimua kwenda binafsi kwa CAG kuzungumza naye.
Alisema kilichompeleka kwa CAG ni kumpa maelezo ya kina juu ya jambo hilo hususani maelezo ya kitaalamu yaliyosababisha WMA kusitisha matumizi ya mashine hizo.
Hata hivyo, kauli hiyo ilizua mjadala na minong’ono miongoni mwa wabunge wa kamati hiyo, jambo lilomfanya Zitto kuingilia kati.
Zitto alihoji sababu iliyosababisha Chuwa kukimbilia kwa CAG na kukataa kuhudhuria kikao cha wadau wote.   ”Chuwa hapa kidogo unatuchanganya, umesema ulienda binafsi kwa CAG kumuelezea na kumfafanulia zaidi kuhusiana na jambo hilo, ilikuwaje uende binafsi na ukaacha kusubiri kikao mlichoitiwa kutoa huo unaoita ushahidi? “alihoji Zitto.
Akijibu jambo hilo, Chuwa alisema alishindwa kusubiri kikao hicho kwa kuwa aliona CAG alikuwa amekosea na kwamba hakuwa na maelezo ya kutosha kuhusiana na suala hilo.
Kauli hiyo ilizidi kuonesha mkanganyiko jambo lillilosababisha kamati hiyo kuunda kamati ndogo kuchunguza mchakato wa kusitishwa kufanyakazi kwa mashine hizo.
Hoja ya kuundwa kwa kamati hiyo imewasilishwa kwa Spika ili kupatiwa kibali ambapo itafanyakazi yake kwa muda wa mwezi mmoja.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI

KOCHA WA AL.AHLY ASEMA YANGA NI TIMU BORA NA NGUMU