Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akihutubia viongozi mbalimbali pamoja na Wananchi wakati akihitimisha Kilele cha Mbio za Mwenge ambazo kitaifa zimefanyika Jijini Mwanza katika Uwanja wa CCM Kirumba tarehe 14 Oktoba, 2024.
Matukio mbalimbali katika kilele cha Maadhimisho ya
mbio za Mwenge wa Uhuru katika uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza tarehe 14 Oktoba,
2024.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameeleza kuwa maono na fikra za Baba wa Taifa
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere zinaendelea kuishi, na Taifa la Tanzania
linaendelea kujivunia amani, mshikamano na umoja.
Aidha, Rais Dkt. Samia amesema kuwa
historia ya Mwalimu Nyerere haiwezi kutofautishwa na historia ya Mwenge wa
Uhuru, ambayo ni Tunu ya Taifa ambayo Mwalimu Nyerere amewaachia Watanzania.
Rais Dkt. Samia ameyasema hayo wakati wa
Kumbukizi ya Miaka 25 ya Kifo cha Hayati Mwalimu Nyerere na Maadhimisho ya
Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru yaliyofanyika katika Uwanja wa CCM Kirumba.
Rais Dkt. Samia amewapongeza vijana
walioshiriki mbio za Mwenge wa Uhuru za mwaka 2024 kwa kuzunguka nchi nzima
kuhamasisha shughuli za maendeleo na kuwahimiza wananchi kufanya kazi kwa
bidii, kuwajibika na kuwa wazalendo kwa Taifa lao.
Vilevile, ameeleza kuwa Serikali itafanyia
kazi taarifa na mapendekezo yaliyowasilishwa na Kiongozi wa Mbio za Mwenge,
Ndugu Godfrey Eliakim Mzava inayojumuisha changamoto, maombi na ushauri
uliotolewa na wananchi kupokelewa na Mwenge wakati wa mbio hizo.
Kwa upande mwingine, Rais Dkt. Samia
ametoa rai kwa vijana kuendelea kulinda Mwenge wa Uhuru ambayo ni Tunu ya Taifa
na kuuenzi kwa kuendelea kufanya kazi kwa bidii.
Akizungumzia Maonesho ya Wiki ya Vijana,
Rais Dkt Samia ametoa pongezi kwa vijana kwa ubunifu, ujuzi, uthubutu na
utayari wao walioonesha kupitia kazi zao na amewahakikishia kuwa Serikali
itaendelea kutatua changamoto zinazowakabili.
Katika kuchochea zaidi ubunifu wa vijana,
Rais Dkt. Samia ameelekeza Halmashauri zote nchini kununua vifaa vinavyotumika
kwenye vituo vya kutolea huduma za afya na kufundishia wanafunzi ambavyo
vinazalishwa kwa ubora na vijana wabunifu hapahapa nchini.
Rais Dkt. Samia pia amerejea wito wake kwa
wananchi kujiandikisha ili waweze kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ikiwa
ni kuendana na dhamira ya Uhuru ya kuwawezesha wananchi kujiamulia mambo yao
wenyewe, ikiwemo kwa kuwachagua viongozi wao.
Comments