Rais wa klabu hiyo, Mhandisi Hersi Said, ametoa kauli nzito kuhusu malengo ya klabu hiyo katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) akisisitiza kuwa malengo yao ni kufika mbali zaidi na hata kubeba ubingwa wa michuano hiyo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa tawi jipya la Young Africans SC nchini Botswana Injinia Hersi ameonesha azma na maandalizi thabiti waliyonayo msimu huu katika ngazi ya kimataifa ambapo amesema “Gaborone United ni timu nzuri lakini sisi pia tumejiandaa hatujaja hapa kizembe. Kama tukifika fainali basi hatutoliacha kombe.”
Aidha Injinia Hersi ameeleza kuwa uzinduzi huo unatoa fursa kwa wanachama wa nje ya nchi (diaspora) kupata haki zao huku akilipongeza tawi hilo kwa kuwa na wanachama hai 63 na kubainisha kuwa kikatiba tawi linahitaji watu 20 tu ili kuidhinishwa, hivyo idadi yao ingeweza hata kuunda matawi matatu tofauti.
Vile vile Injinia Hersi ameelezea ukuaji wa Chapa ya Dar es Salam Young Africans akibainisha kuwa tawi hilo lililozinduliwa jijini Gaborone ni tawi jipya la 18 lililopo nje ya Tanzania kwa klabu hiyo, jambo linalothibitisha kukua kwa kasi kwa mtandao wa mashabiki na chapa ya Yanga Kimataifa.

Comments