ZUNGU ALIVYONASWA KWA RUSHWA DODOMA

Mbunge wa Ilala, Mussa Azn Zungu (kulia) akiwa katika moja ya shughuli za michezo jimboni mwake


WINGU la rushwa limeendelea kutanda katika Chama Cha Mapinduzi (CCM), na sasa Mbunge wake wa Ilala, Mussa Zungu, anashilikiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), akituhumiwa kutoa rushwa kwa baadhi ya wajumbe wa Jumuiya ya Wazazi.
Zungu ambaye anakuwa mbunge wa pili wa CCM kunaswa na TAKUKURU kwa tuhuma za rushwa, anashikiliwa pamoja na wajumbe wawili wa jumuiya hiyo.

Mbunge huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bunge, alikuwa akigombea nafasi ya Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho (NEC) kupitia Jumuiya ya Wazazi Tanzania Bara na alinaswa juzi sambamba na Dk. Damas Mukasa na Fatuma Kasenga.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Dodoma, Yunis Munisi, alisema Zungu alikamatwa Oktoba 30, mwaka huu, siku moja kabla ya uchaguzi huo.

Akielezea mazingira ya kukamatwa kwao, alisema Zungu alikamatwa akiwa na wapambe wake wanne akitoa rushwa kwa wajumbe ili wampigie kura.

Kuhusu Dk. Mukasa ambaye alikuwa akigombea nafasi ya ujumbe wa Baraza Kuu la Wazazi Taifa na mjumbe wa Mkutano Mkuu CCM Taifa, Munisi alisema alikamatwa Oktoba 8, mwaka huu, nje ya Ukumbi wa Kilimani mjini hapa kwa kosa la kutoa rushwa kwa wajumbe ili wampigie kura.

Pamoja na hilo, wajumbe wengine wawili nao wanashikiliwa na TAKUKURU kwa kosa la kupokea rushwa kutoka kwa Dk. Mukasa ili wamchague.

Mgombea mwingine aliyekamatwa, Fatuma, ambaye ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Mkoa wa Mbeya na Mkutano Mkuu Wazazi Taifa, alikamatwa saa tisa usiku wa kuamkia jana akiwa analipia baadhi ya wajumbe wa mkutano vyakula na vinywaji.

“Inaaminika kwamba huo ulikuwa ni ushawishi ili wajumbe wamchague...alikamatwa katika nyumba ya wageni ya Kitoli iliyopo eneo la Iringa Road mjini Dodoma,” alisema Munisi.

Alisema TAKUKURU imekuwa ikifuatilia taarifa za vitendo vya rushwa tangu kuanza kwa chaguzi za ndani za CCM kuanzia ngazi za chini hadi taifa kwa lengo la kuzuia na kupambana na vitendo hivyo.

Munisi alisema hatua hiyo imefanikiwa kuzuia vitendo vingi ambavyo vilitaka kutendeka baada ya kupata mipango hiyo na kuitibua kabla ya kufanikiwa.

Hata hivyo, alisema changamoto kubwa waliyokumbana nayo ni kitendo cha wajumbe kushirikiana na wagombea na wapambe wao katika vitendo vya rushwa, na hivyo kuwa shida kufanya ushirikiano.

Alisema changamoto nyingine inatokana na wananchi kudai wameona vitendo vya rushwa vikitendeka, lakini hawachukui hatua zozote za kutoa taarifa TAKUKURU.

Kuhusu tuhuma zinazowakabili akina Zungu na wenzake, alisema uchunguzi unaendelea.

Kambi ya Lowassa kidedea
Kambi inayoungwa mkono na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa, imezidi kuonesha umwamba wake ndani ya CCM kwa kuibuka kidedea katika uchaguzi wa Jumuiya ya Wazazi uliofanyika jana.

Abdallah Bulembo ndiye ameibuka mshindi wa nafasi ya mwenyekiti wa jumuiya hiyo kwa kura 677 na kuwatimulia vumbi washindani wake, Martha Mlata aliyepata kura 146 na John Barongo aliyeshika nafasi ya mwisho kwa kuambulia kura 43.

Mapema akifungua mkutano huo wa uchaguzi, Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal, aliitaka jumuiya hiyo kuchagua viongozi watakaoweza kukiepusha chama na rushwa kwa kipindi chao cha miaka mitano.

“Kiongozi anayehonga ili aweze kupata madaraka huyo si kiongozi na hafahi kuchaguliwa,” alisema Dk. Bilal na kuwataka wagombea wote kuachana na imani ya kutumia fedha kutafuta uongozi.

Aidha, makamu huyo aliwataka wazazi kuwa mstari wa mbele katika kuwalea vijana ili maadili yaliyopotea yarudi kama hapo awali.

Dk. Bilal alisema kuwa wazazi ndio wenye jukumu kubwa la kuwalea vijana na kuwaongoza katika maadili mema, hivyo ni jukumu lao kubwa kuhakikisha vijana wanakuwa na tabia njema.

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

CHATANDA AFUNGUA MAFUNZO YA KUWAJENGEA UWEZO MADIWANI WANAWAKE WA MIKOA 11

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

KOCHA BENCHIKHA AMESEPA

MASHUSHUSHU WA MAMELODI WALIKUJA KUTUPELELEZA: HERSI