AHADI YA WAZIRI MKUU KWA STARS



Waziri Mkuu Mizengo Pinda tayari amekabidhi sh. milioni 10 kupitia Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ikiwa ni ahadi yake aliyotoa kwa Taifa Stars ikiwa ni motisha kwa wachezaji wa timu hiyo kabla ya mechi yao na Chad iliyochezwa Novemba Mosi mwaka jana jijini N’Djamena.
 
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupitia kwa Meneja wa Taifa Stars, Leopold Tasso linaanda orodha ya wachezaji wanaostahili kunufaika na ahadi hiyo, na baadaye kuiwasilisha BMT kwa ajili ya mgawo kwa wahusika.
 
Tunamshukuru Waziri Mkuu Pinda kwa ahadi hiyo, kwani Taifa Stars ilifanikiwa kushinda mechi hiyo ya ugenini mabao 2-1, ushindi ambao bila shaka ulichagizwa na ahadi hiyo.
 
KUUZWA KWA TIMU YA SMALL KIDS
Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF iliyokutana Desemba 30 mwaka jana ilijadili masuala mbalimbali yaliyofikishwa mbele yake ikiwemo malalamiko juu ya kuuzwa kwa timu ya Small Kids ya Rukwa.
 
Usikilizaji wa suala hilo uliahirishwa na Kamati kuagiza kwanza ipatiwe vitu vifuatavyo; Katiba iliyosajiliwa ya Small Kids, muhtasari (minutes) na uamuzi wa kikao chochote kilichofanyika kuzungumzia mauzo ya timu hiyo ambayo iko daraja la kwanza.
 
Pia Kamati inataka ipatiwe mawasiliano (correspondences) yote yaliyofanyika kuhusiana na ununuzi/mauzo ya timu hiyo. Hivyo suala hilo litasikilishwa katika kikao kingine cha kamati baada ya kuwasilishwa nyaraka hizo.
 
MGOGORO WA UONGOZI TAREFA
Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji itatuma wajumbe wake wawili Tabora kukutana na Kamati ya Utendaji ya Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Tabora (TAREFA).
Wajumbe hao katika kikao chao na Kamati ya Utendaji ya TAREFA watasikiliza kuhusu kiini cha mgogoro uliopo na baadaye watawasilisha taarifa kwa Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji. Kamati itafanyia kazi ripoti hiyo kabla ya kufanya uamuzi.
 
MAREKEBISHO YA KATIBA ZA WANACHAMA
Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji pia ilifanyia kazi suala la marekebisho ya katiba za wanachama wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Katiba hizo zimegawanywa katika makundi matatu; katiba za wanachama wapya, katiba ambazo tayari zimerekebishwa na katiba ambazo hazijarekebishwa.
 
Maelekezo ya Kamati ni kuwa itatoa mwelekeo (roadmap) utakaoonesha muda wa mwisho (deadline) wa kufanya marekebisho kwa makundi yote hayo matatu ambapo kwa wanachama watakaoshindwa hawataruhusiwa kuingia kwenye Mkutano Mkuu wa TFF.
 
Maeneo ya msingi ya marekebisho ni sifa za uongozi. Katiba zote za wanachama wa TFF kwa upande wa sifa za uongozi ni lazima ziwe sawa. Maeneo mengine ni kuainishwa wazi kwa majukumu ya Kamati ya Utendaji, Mkutano Mkuu na namna ya kutatua migogoro ya wanachama ili kuepuka watu kwenda mahakamani.
 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

ALLY KAMWE AZIMIA KWA MKAPA.

RAIS SAMIA KUZINDUA MKUTANO MKUU WA 79 WA BARAZA LA MICHEZO YA MAJESHI DUNIANI

MIGINGO KISIWA KIDOGO ZAIDI AFRIKA KILICHOGOMBEWA NA UGANDA, KENYA