Waziri
Mkuu Mizengo Pinda tayari amekabidhi sh. milioni 10 kupitia Baraza la
Michezo la Taifa (BMT) ikiwa ni ahadi yake aliyotoa kwa Taifa Stars
ikiwa ni motisha kwa wachezaji wa timu hiyo kabla ya mechi yao na Chad
iliyochezwa Novemba Mosi mwaka jana jijini N’Djamena.
Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kupitia kwa Meneja wa Taifa Stars,
Leopold Tasso linaanda orodha ya wachezaji wanaostahili kunufaika na
ahadi hiyo, na baadaye kuiwasilisha BMT kwa ajili ya mgawo kwa wahusika.
Tunamshukuru
Waziri Mkuu Pinda kwa ahadi hiyo, kwani Taifa Stars ilifanikiwa
kushinda mechi hiyo ya ugenini mabao 2-1, ushindi ambao bila shaka
ulichagizwa na ahadi hiyo.
KUUZWA KWA TIMU YA SMALL KIDS
Kamati
ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF iliyokutana Desemba 30
mwaka jana ilijadili masuala mbalimbali yaliyofikishwa mbele yake
ikiwemo malalamiko juu ya kuuzwa kwa timu ya Small Kids ya Rukwa.
Usikilizaji
wa suala hilo uliahirishwa na Kamati kuagiza kwanza ipatiwe vitu
vifuatavyo; Katiba iliyosajiliwa ya Small Kids, muhtasari (minutes) na
uamuzi wa kikao chochote kilichofanyika kuzungumzia mauzo ya timu hiyo
ambayo iko daraja la kwanza.
Pia
Kamati inataka ipatiwe mawasiliano (correspondences) yote
yaliyofanyika kuhusiana na ununuzi/mauzo ya timu hiyo. Hivyo suala hilo
litasikilishwa katika kikao kingine cha kamati baada ya kuwasilishwa
nyaraka hizo.
MGOGORO WA UONGOZI TAREFA
Kamati
ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji itatuma wajumbe wake wawili
Tabora kukutana na Kamati ya Utendaji ya Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa
wa Tabora (TAREFA).
Wajumbe
hao katika kikao chao na Kamati ya Utendaji ya TAREFA watasikiliza
kuhusu kiini cha mgogoro uliopo na baadaye watawasilisha taarifa kwa
Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji. Kamati itafanyia kazi
ripoti hiyo kabla ya kufanya uamuzi.
MAREKEBISHO YA KATIBA ZA WANACHAMA
Kamati
ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji pia ilifanyia kazi suala la
marekebisho ya katiba za wanachama wa Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF). Katiba hizo zimegawanywa katika makundi matatu; katiba
za wanachama wapya, katiba ambazo tayari zimerekebishwa na katiba ambazo
hazijarekebishwa.
Maelekezo
ya Kamati ni kuwa itatoa mwelekeo (roadmap) utakaoonesha muda wa
mwisho (deadline) wa kufanya marekebisho kwa makundi yote hayo matatu
ambapo kwa wanachama watakaoshindwa hawataruhusiwa kuingia kwenye
Mkutano Mkuu wa TFF.
Maeneo
ya msingi ya marekebisho ni sifa za uongozi. Katiba zote za wanachama
wa TFF kwa upande wa sifa za uongozi ni lazima ziwe sawa. Maeneo
mengine ni kuainishwa wazi kwa majukumu ya Kamati ya Utendaji, Mkutano
Mkuu na namna ya kutatua migogoro ya wanachama ili kuepuka watu kwenda
mahakamani.
Comments