JAMES KIBOSHO AZIBA PENGO LA CHAZ BABA TWANGA ,
* DOGO RAMA, VANANCE, JUMANNE WAFUKIA MASHIMO
MPIGA ngoma nguli wa bendi ya
muziki wa dansi ya African Stars 'Twanga Pepeta', James Kibosho,
amerithi mikoba ya aliyekuwa mwimbaji wa bendi hiyo, Charles Gabriel
'Chaz Baba' aliyetangaza kujiengua wiki hii na kuhamia Mashujaa Musica.
Mmoja wa wanamuziki galacha wa
Twanga Pepeta, Khamis Kayumbu 'Amigolas' jana usiku wakati wa onesho la
Twanga Pepeta kwenye ukumbi wa Club Bilicanas, alimtangaza Kibosho kuwa
ndiye kiongozi wa kupanga muziki jukwaani (Stage Master), nafasi
iliyokuwa ikishikiliwa na Chaz Baba.
Tangazo hilo la Amigolas
lilipokewa kwa hoi hoi, nderemo na vifijo kutoka kwa mashabiki
kochokocho wa Twanga Pepeta waliojaa pomoni ukumbini hapo kushuhudia
burudani ambayo pia ilishuhudiwa na mwimbaji wa bendi ya Mapacha Watatu,
Kalala Hamza 'Junior', Meneja wake, Hamisi Dacorta na wanamuziki
wengine wa FM Academia, Patcho Mwamba na Pablo Masai.
Waimbaji wa Twanga Pepeta,
Ramadhan Athuman 'Dogo Rama', Venance Mgori na rapa na mwimbaji, Jumanne
Said, wakiongozwa na kiongozi msaidizi wa bendi hiyo, Saleh Kupaza,
walidhihirisha hakuna pengo lililoachwa na Chaz Baba kutokana na kuimba
kwa ufasaha, 'vipande' alivyokuwa akiimba.
Wanamuziki wengine wa Twanga
Pepeta waliokuwa jukwaani kuongoza mashambulizi ni kiongozi mkuu, Luiza
Mbutu, Amigolas, Haji Ramadhan (mshindi wa BSS 2011), Mwinjuma Muumin,
Janeth Isinika, Khadija Mnoga 'Kimobitel', Grayson Semsekwa na Msafiri
Said 'Diouf'.
Pia walikuwepo wapiga vyombo,
Miraji Shakashia 'Shakazulu', Jojoo Jumanne, Godfrey Kanuti, Selemani
Shaibu, Victor Nkambi na Hassan Kado. Wanenguaji ni Asha Said
'Sharapova', Maria Soloma, Betty Johnson 'Baby Tall', Mary Khamis na
wengineo.
Twanga Pepeta hivi sasa inatamba
na albamu yake ya 11 ya Dunia Daraja yenye nyimbo za Kauli, Kiapo cha
Mapenzi, Umenivika Umasikini, Mtoto wa Mwisho, Dunia Daraja na Penzi la
Shemeji.
Albamu zilizopita za bendi hiyo
ni Kisa cha Mpemba (1999), Jirani (2000), Fainali Uzeeni (2001), Chuki
Binafsi (2002), Ukubwa Jiwe (2003), Mtu Pesa (2004), Safari 2005 (2005),
Password (2006), Mtaa wa Kwanza (2007) na Mwana Dar es Salaam (2009).
SOURCE MICHUZI JR
Comments