Meneja wa Arsenal, Arsene Wenger amesema mwamuzi Lee Probert ameigharimu timu yake kupoteza mchezo kwa kufungwa mabao 2-1 na Fulham.
Wenger adai mwamuzi
aliinyonga Arsenal dhidi ya Fulham
Arsenal walionekana dhahiri
wangeondoka na pointi tatu katika uwanja wa Craven Cottage hadi pale wenyeji
walipocharuka na kufunga mabao hayo mawili zikiwa zimesalia dakika tano kabla
ya mpira kumalizika.
Wenger hakufurahishwa na uamuzi
wa kumtoa nje kwa kadi nyekundu mlinzi Johan Djourou baada ya kuoneshwa kadi ya
pili ya njano na pale waliponyimwa mkwaju wa penalti.
"Mwamuzi amesababisha
matokeo yawe yalivyokuwa kutokana na kutoa uamuzi mbovu, hii kwa maoni yangu,"
alisema Wenger.
Arsenal sasa wanashikilia
nafasi ya tano ya msimamo wa Ligi Kuu ya soka ya England, pointi moja nyuma ya
Chelsea, kufuatia kupoteza mchezo wake wa tano ugenini.
Djourou alitolewa nje kwa kadi
nyekundu katika dakika ya 78 kwa kosa la kumvuta na kumuangusha Bobby Zamora
lakini Wenger anahisi mlinzi wake huyo alipewa adhabu kali na akaishutumu
Fulham kwa kufanya mbinu kuhakikisha mlinzi huyo anatolewa nje.
"Wakati Djourou
alipooneshwa kadi ya kwanza ya njano, walikuwa wanajaribu kufanya kila hila
aoneshwe nyingine atolewe nje na mwamuzi aliingizwa mtegoni," alisema
Wenger.
"Nilikuwa naiona kadi
inakuja. Nisingependa kuwa chanzo cha habari cha magazeti. Nakuambia kile
nilichokiona mchezoni. Sijali kitakachotoke."
Wenger pia anahisi timu yake ilipaswa
kupewa penalti katika kipindi cha kwanza.
Alipoulizwa iwapo Gervinho
alifanyiwa rafu ndani ya sanduku la hatari na Philippe Senderos, Wenger
alisema: "Ni aslimia 200, lakini tulijua hatungepewa nafasi ya kupiga
mkwaju wa penalti."
Arsenal ilitawala mchezo katika
kipindi cha kwanza kwa bao lililofungwa kwa kichwa na Laurent Koscielny.
Comments