SUMAYE APONDA POSHO ZA WABUNGE

Frederick Sumaye amezungumzia mwelekeo wa taifa huku akionya kuwa nyongeza za posho zisizofuata utaratibu kwa watumishi wa umma ni hatari na ni utawala mbaya kwa nchi.Alisema suala la posho ni jambo ambalo sasa limekuwa tatizo kwa Serikali na kuwa imefika wakati ofisi za Serikali zimehamia hotelini lengo likiwa ni watumishi wa umma kutafuta mwanya wa kulipana posho.

“Ndiyo maana watu wa TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania) wanakusanya fedha nyingi, lakini ni fedha kidogo sana zinazokwenda kwenye huduma za jamii. Nadhani hili ni tatizo na ni utawala mbaya kabisa, lazima kuwepo mabadiliko kama kweli tunataka kuisaidia nchi yetu,” alisema Sumaye.

Kuhusu posho za wabunge, Sumaye alisema ni jambo la hatari kwani ikiwa wabunge watalipwa viwango vya posho vilivyotangazwa, linaweza kuvuruga amani ya nchi.

Sumaye alisema hayo katika kipindi cha dakika 45 kinachotushwa na Kituo cha Televisheni cha ITV. Alisema ongezeko la posho za wabunge linaweza kuchochea makundi mengine kudai akitolea mfano wa wanajeshi, polisi, Mahakama na walimu jambo ambalo alisema litamweka Rais katika wakati mgumu kufanya uamuzi.

“Mwanasiasa mzuri akifanya jambo akiona limewaudhi wananchi anatakiwa aliache, lakini pia kwenye hili, huu mkanganyiko wa Spika na Katibu wake na huu ukimya wa Ikulu ni tatizo. Tungependa waseme ili umma ujue hali ikoje,” alisema Sumaye.  Alisema hatua ya Bunge kujipandishia posho ya kikao kutoka Sh70,000 hadi Sh200,000 kwa siku haliingii akilini na kwamba linakiuka utaratibu uliowekwa na Serikali katika kulipa gharama kwa maofisa wake ikiwa gharama hizo ni zaidi ya kiwango cha fedha za kujikimu zilizowekwa.

“Siyo kwamba napinga posho. Wabunge wanastahili posho, lakini kwa kweli kujiongezea kutoka Sh70,000 hadi Sh200,000 siyo sahihi,” alisema Sumaye.Alisema wakati alipoteuliwa na Rais Benjamin Mkapa kwa Awamu ya Pili kushika wadhifa wa Waziri Mkuu, aligoma kwa sababu alikuwa amekwaruzana na wabunge kuhusu nyongeza ya posho.

“Nilimwambia wabunge watanikataa kwa sababu nimegombana nao sana juu ya suala la posho lakini akasema lazima uwe na mimi ndipo nikakubali. Lazima hili suala liangaliwe mara mbilimbili, leo wabunge mmejiongezea kesho jeshi, polisi na walimu nao watataka, tutafanyaje? Tusifanye mambo ambayo yatamuweka Rais pabaya,” alisema.

Kitanzi cha Gamba Akizungumzia Uchaguzi Mkuu ujao wa 2015, alikitahadharisha chama chake cha CCM akikitaka kutekeleza kwa vitendo mkakati wake wa kujivua gamba, la sivyo utageuka na kuwa kitanzi kwake kwenye uchaguzi huo.

Alisema kama CCM kina nia ya dhati katika kupambana na kuhakikisha kinatokomeza rushwa na ufisadi unaoonekana kuwa kikwazo katika maendeleo ya taifa, lazima kiwavue gamba walioshindwa kujivua wenyewe... “Wasipojivua hilo koti, itabidi watu wengine wawasaidie kulivua,” alisema Sumaye.

Alisema hivi sasa suala hilo limeonekana kama vita dhidi ya pande mbili ndani ya chama hicho, ingawa upande unaotetea ufisadi, hautoki moja kwa moja na kujionyesha. “Lakini ukiangalia sana suala la rushwa utaona kuwa hatujapambana nalo vya kutosha, kinachomfanya mtu awe mla ruswa ni cheo, ukimtoa kwenye hiyo nafasi pamoja na fedha zake hatoweza kufanya chochote,” alisema Sumaye.

Alisema chama hicho ni lazima kihakikishe kinatokomeza rushwa wakati wa uchaguzi wake wa ndani, vinginevyo alisema wananchi watakiangusha.  Matumizi mabaya ya urais Sumaye alisema rushwa, ufisadi na matumizi mabaya ya urais, ni moja ya sababu inayofanya nchi nyingi za Afrika zizidi kuwa masikini.

Alisema hali hiyo haipo kwa viongozi wa sasa pekee, bali hata kwa wale waliowatangulia isipokuwa wale tu waliogombea uhuru wa mataifa hayo. “Matumizi mabaya ya taasisi ya urais ni tatizo, mtu akiwa Rais anafanya taasisi hiyo inakuwa mali yake alikuwa ni mtu wa kawaida lakini ghafla anakuwa tajiri anataka na watoto wake pia wawe matajiri,” alisema na kuongeza:

 “Urais siyo mali ya mtu na familia yake, dhamana hiyo unapewa na wananchi na inatakiwa uwatumikie wao, viongozi kama Nyerere, Kenyatta, Mandela mitizamo yao ilikuwa tofauti sana na viongozi wa sasa,” alisema. Alitoa mfano wa Rais wa Misri aliyepinduliwa Hussein Mubarak ambaye alikuwa na utajiri wa zaidi ya Dola 70bilioni na mtoto wake akiwa na fedha maradufu ya hizo. “Nimesema haya kwa ujumla jinsi nchi nyingi za Afrika zilivyo lakini haya ni matatizo ambayo hata hapa kwetu yapo, Rais Kikwete ameyakuta, atakuja mwingine atayakuta, tusipopiga vita rushwa na ufisadi, hatutakwenda popote,” alisema Sumaye.

Maelezo hayo ya Sumaye, yalitokana na swali aliloulizwa kwamba, kwa nini baadhi ya nchi ikiwemo Korea Kusini miaka ya 1960 zilikuwa karibu sawa kimaendeleo na nchi nyingi za Afrika lakini kwa sasa nchi hizo zimeendelea maradufu huku Afrika ikizidi kuwa masikini.

Rushwa na uchaguzi Sumaye alisema: “Kama tunataka viongozi bora wa kuliongoza taifa hili, lazima tupambane na rushwa katika uchaguzi... Nasema fedha za kuhonga zilizowekwa kwenye bahasha lazima tuhakikishe zinatokomezwa, tusipofanya hivyo tutaondolewa, nadhani ni wakati wa kurudi kwenye enzi za Tanu na ile CCM ya zamani, mtu unazungumza watu wanakuchagua bila kutoa hongo, tusipofanya hivyo wananchi watafanya uamuzi tofauti.”
Alisema watu wanaotaka madaraka kwa kuwanunua wapiga kura lazima wadhibitiwe kwani hali hiyo ikiachwa nchi itaangamia kwa ubinafsi.

Sumaye alilalamika kuwa kuna tatizo ndani ya CCM na Serikali yake ya kupambana na wanaopambana na rushwa badala ya kuwaunga mkono... “Hilo ndilo tatizo kubwa, wale wanaopambana na ufisadi na rushwa sasa wanageuzwa kuwa kambi fulani inayotaka kuiondoa kambi nyingine madarakani. Huo ni ujinga wote tunatakiwa kupambana tukiwa kitu kimoja. Inaonyesha kuna mapambano ya kudhoofisha wale wanaopambana na ufisadi.”

 Alikinyooshea kidole CCM akisema kuwa chaguzi zake nyingi zimejaa rushwa huku wala rushwa wakiachwa bila kukamatwa.   “Wakati wa uchaguzi fedha zinagawanywa lakini kuna watu wanakamatwa na wengine hawakamatiki. Lazima kama Taifa tupambane. Rushwa ikiendelea kuwepo tutakuwa na nchi isiyo na maendeleo,” alisema.

Sumaye aliongeza kuwa, vyama vya siasa vipambane na watu wanaotaka madaraka kwa njia ya fedha kwani kama wataingia madarakani wataanza kujineemesha wao badala ya kuwatumikia wananchi.

 Urais 2015 Kuhusu wanaotaka kugombea urais mwaka 2015 Sumaye alisema alimradi hatafuti nafasi ya kumuondoa Rais aliyepo madarakani wala haleti vurugu, haoni shida kwa mtu yeyote kuota au kutangaza kwamba mwaka 2015 atagombea nafasi hiyo. Alisema kibaya ni endapo mtu huyo atafanya hivyo huku akiwachafua wenzake, jambo ambalo amesema kwa kiasi fulani sasa linajitokeza.

“Tatizo ni pale watu wanapojaribu kuchafua watu, hilo ndiyo tatizo, nafikiri lipo... mimi bado sijatangaza na bado sijaamua nikiamua nitasema. Kuna tatizo kwamba ukisema chochote wanasema huyu anautaka urais sasa ina maana kwamba wanaotaka urais wanyamaze, au wasipumue hata kidogo?”

 Uongozi wa Mkapa Akizungumzia changamoto za uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tatu ya Mkapa, alisema walifanya kazi kubwa ya kuinua uchumi wa nchi kwani walipoanza kazi nchi ilikuwa katika hali mbaya.

“Wakati Rais Mkapa anaingia madarakani ilikuwa ngumu sana. Pili marafiki wa nje, taasisi za fedha zilitukataa kama nchi. Hata mishahara ilikuwa ngumu kupata wakati huo kima cha chini kilikuwa ni Sh17,000,” alisema na kuongeza:    “Hatukuweza kuingia kwenye janga la kuchapisha fedha. Kuchapisha fedha ni janga la kiuchumi. Ukiona nchi inachapisha fedha ujue imeporomoka kiuchumi na ndiyo maana sisi tulihakikisha kuwa hatuingii kwenye kuchapisha fedha,” alisema.

Kuhusu mchango wa viongozi wastaafu katika kuleta maendeleo ya nchi, Sumaye alisema Serikali imewatenga viongozi wastaafu japo wapo wanaotumiwa.

“Kama utakumbuka Mzee Mkapa wakati wa World Economic Forum pale Mlimani City alilalamika akisema tatizo kubwa la Afrika ni kutotumia hazina ya viongozi wa Afrika. Akasema hamtutumii lakini wenzenu wa nje wanatutumia sana na wanatufaidi sana. 

“Hilo ni tatizo la Afrika na ni tatizo la Tanzania kwa sababu tunayo hazina kubwa ya viongozi ambao tungeweza kuwatumia vizuri sana. Lakini hawatumiki. Ili niweze kusaidia, lazima awepo mtu wa kukwambia hebu fulani njoo hapa au wewe useme hebu nimwone fulani lakini bila ya hivyo hakuna namna ya kusaidia.” 

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

HAKUNA BINADAMU ALIYESALIMIKA NA UPOFU HUU...

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WATANZANIA WATAKAOVAA JEZI ZA MAMELODI AU AL AHLY

ALLY KAMWE AZIMIA KWA MKAPA.

RAIS SAMIA KUZINDUA MKUTANO MKUU WA 79 WA BARAZA LA MICHEZO YA MAJESHI DUNIANI

MIGINGO KISIWA KIDOGO ZAIDI AFRIKA KILICHOGOMBEWA NA UGANDA, KENYA