HABARI LUKUKI KUTOKA TFF

WAKENYA KUICHEZESHA NGORONGORO HEROES NYUMBANI
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Kenya kuchezesha mechi ya raundi ya pili kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 kati ya Tanzania (Ngorongoro Heroes) na Nigeria.
 
Mwamuzi atakayechezesha mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya pili itakayofanyika Julai 29 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam atakuwa Moses Ojwang Osano.
 
Waamuzi wasaidizi watakuwa Peter Keireini na Elias Kuloba Wamalwa wakati mwamuzi wa mezani (fourth official) ni Thomas Onyango. Kamishna wa mechi hiyo atakuwa Charles Masembe kutoka Uganda.
 
Pia CAF imemteua Alfred Kishongole Rwiza wa Tanzania kuwa Kamishna wa mechi ya michuano hiyo kati ya Misri na Kenya itakayochezwa jijini Cairo kati ya Julai 27, 28 na 29 mwaka huu.
 
TEMEKE YAICHAPA DODOMA 2-0 COPA
Temeke imefainikiwa kuilaza Dodoma mabao 2-0 katika mechi ya kundi C ya michuano ya Copa Coca-Cola iliyochezwa leo (Julai 3 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Tanganyika Packers ulioko Kawe, Dar es Salaam.
 
Mabao ya washindi ambao kwa matokeo hayo sasa wamefikisha pointi tano yalifungwa dakika ya tano Hassan Kabunda wakati la pili lilifungwa dakika ya 34 na Abdul Hassan.
 
Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam umeshuhudia Morogoro ikiibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Iringa lililofungwa dakika ya 37 na Mutalemwa Katunzi.
Nayo Kilimanjaro imeibuka na ushindi wa bao 1- dhidi ya Tabora katika mechi iliyochezwa Uwanja wa Nyumbu mkoani Pwani. Bao hilo katika mechi hiyo ya kundi D lilifungwa dakika ya 14 na Eric Christopher. 
 
Kwa matokeo hayo Tabora imebaki na pointi tatu baada ya kushinda mechi moja tu dhidi ya Pwani, na imebakiza mechi moja dhidi ya Kusini Unguja ambayo hata ikishinda haiwezi kuingia hatua ya 16 bora.
 
Nao mabingwa watetezi Kigoma wamejiweka katika nafasi nzuri ya kucheza 16 bora baada ya kuitandika Kusini Pemba mabao 3-1 katika mchezo wa kundi A uliochezwa Uwanja wa Tamco ulioko mkoani Pwani.
 
TIMU 10 TANZANIA KUCHEZA ROLLINGSTONE BURUNDI
Timu 10 za Tanzania Bara zitashiriki kwenye michuano ya Rollingstone kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 ambayo mwaka huu itafanyika Makamba nchini Burundi kuanzia Julai 7 mwaka huu.
 
Jumla ya timu 24 zinashiriki mashindano hayo na zimepangwa katika makundi sita tofauti. Timu nyingine zinatoka Burundi, Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), Uganda na Zanzibar.
 
Timu za Tanzania zilizoingia katika mashindano hayo ni Azam, Bishop High School, Chakyi Academy, Coastal Union, Rollingstone, Ruvu Shooting, Simba, TAYFA Academy, Yanga na Young Life. 

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Rollingstone, Issa Karata timu zote zinatakiwa kwenda vyeti vya kuzaliwa vya wachezaji wake ili kuthibitisha umri wao. Kamati ya Mashindano itakuwa na uamuzi wa mwisho kuhusu umri wa mchezaji yeyote.
 
Kila timu inatakiwa kuwa na wachezaji 20 na viongozi watano ambao watagharamiwa na waandaaji kwa huduma za malazi na chakula kwa muda wote wa mashindano hayo yaliyoanzishwa miaka 13 iliyopita.
 
MCHAKATO UCHAGUZI DRFA KUANZA JULAI 15
Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imeridhia ombi la Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) kuanza mchakato wa uchaguzi wake Julai 15 mwaka huu.
 
DRFA iliwasilisha ombi TFF ili kusogeza mbele kuanza kwa mchakato huo kwa vile Katiba yao ambayo waliagizwa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kuifanyia marekebisho kabla ya kuingia kwenye uchaguzi huo bado iko kwa Msajili. 
 
Awali DRFA ilikuwa ianze mchakato wa uchaguzi Julai Mosi mwaka huu. Kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF, mchakato wa uchaguzi unatakiwa kuchukua siku 40 tangu kuanza kutolewa fomu kwa wagombea hadi siku yenyewe ya uchaguzi.
 
Pia Kamati ya Uchaguzi ya TFF imekubali ombi la Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Kigoma (KRFA) kuanza mapema mchakato wa uchaguzi wake. Sasa mchakato wa uchaguzi wa chama hicho utaanza Septemba Mosi mwaka huu badala ya Septemba 15 mwaka huu kama ilivyokuwa imepangwa awali.
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Comments

HABARI ZILIZOSOMWA ZAIDI

MAKABILA 10 YENYE WANAWAKE WAREMBO TANZANIA

NI SIMBA PEKEE ILIYOFUNGWA ROBO FAINALI

KINANA ASIMIKWA KUWA MMOJA WA MACHIFU WA WAPARE, SAME MAGHARIBI

DK NCHIMBI AMTEMBELEA MZEE YUSUF MAKAMBA*

AZIZ KI AAHIDI KILA ATAKAYEIFUNGA MAMELODI

DKT NCHIMBI AWAAHIDI MAKUBWA WANANCHI WA KWELA, RUKWA

DKT NCHIMBI ASHIRIKI MAZISHI YA ASKOFU.GACHUMA WA KANISA LA NLGCC

π™‚π˜Όπ™ˆπ™Šπ™‰π˜Ώπ™„ π™†π˜Όπ˜Ύπ™ƒπ™€π™•π˜Ό π™†π™„π˜½π™„π™‰π™‚π™’π˜Ό.