AFARIKI AKIVUA SAMAKI
Na Ezekiel
Kamanga,Chunya.
Mwananchi mmoja aliyefahamika kwa jina la Emmanuel
Kidava,amefariki dunia akivua samaki katika Kitongoji cha Kambipotea,Kijiji cha
Iyovyo,Kata ya Totowe Wilaya ya Chunya Mkoani
Mbeya.
Tukio hilo limetokea Septemba 19 mwaka huu majira ya
saa 2 asubuhi,marehemu akiwa na Mtumbwi alipokwenda kuvua samaki na mauti hayo
yamemkuta alipokuwa akivuta nyavu alizotega samaki,lakini nyavu hizo zilikwama
kwenye mwamba ndipo marehemu alichupa kupiga mbizi ndani ya maji ili kujaribu
kuzinasua nyavu hizo.
Aidha katika juhudi hizo za kunasua nyavu hizo marehemu
alikosa hewa na dakika tatu baadae alipoteza maisha kutokana na kunasa katika
nyavu hizo alizokuwa akijaribu kuzinasua.
Baada ya kushindwa kuibuka baadhi ya wavuvi waliokuwa
karibu baada ya kuona marehemu haibuki baada ya kuzama walifuatilia eneo la
tukio na kuanza kuvuta nyavu hizo hadi ufukweni mwa ziwa na kumkuta marehemu
kapoteza maisha.
Wavuvi hao baada ya kuutoa mwili wa marehemu katika
maji walitoa taarifa kwa Mwenyekiti wa Kijiji cha Kambipotea Bwana Richard
Mbuya,ambapo alithibitisha kutokea kwa kifo hicho na yeye kuitaarifu
Polisi.
Jeshi la Polisi lilifika eneo la tukio na kuruhusu
mwili huo kuchukuliwa kwa ajili ya maziko,kutokana na marehemu kutokuwa na ndugu
hivyo Serikali ya kijiji ilichukua jukumu la
mzishi,
Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa marehemu kabla ya
kifo chake imedaiwa alitokea katika Kijiji cha Nzihi,barabara ya kuelekea
Kidamali Mkoani Iringa.
Comments