RAIS KIKWETE AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI DARAJA LA KIGAMBONI
Thursday, September 20, 2012
* Aonya 'wenye viwanda' vya kutunga uongo kuacha tabia hiyo na kuelekeza nguvu kwenye maendeleo
* Asema viongozi wa vyama vya upinzani badala ya kupigania maendeleo, wapo tayari nchi iyakose
*Asema tukio la kuwekwa jiwe la msingi ujenzi huo, leo litawanyima usingizi badala ya kufurahi
DAR ES SALAAM,
TANZANIA
Rais Jakaya Kikwete leo, Alhamisi, Septemba 20,
2012, ameweka Jiwe la Msingi la ujenzi wa Daraja la Kigamboni, Dar es Salaam,
huku akiwaonya watu ambao amewaeleza kuwa wanavyo viwanda vya kutunga uongo
kuacha tabia hiyo na kuelekeza nguvu kwenye maendeleo.
Aidha, Rais Kikwete amewahakikishia wakazi wote
wa Kigamboni ambao wanaondolewa katika maeneo yao kwa ajili ya kupisha ujenzi wa
daraja hilo na ujenzi wa Mji Mpya wa Kigamboni kuwa watalipwa stahili na haki
zao zote.
Daraja hilo la Kigamboni ambalo wazo la
kujengwa kwake lilibuniwa kwa mara ya kwanza zaidi ya miaka 30, tokea mwaka
1978, wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, linajengwa kwa
gharama ya Sh. bilioni 214.6 na litakuwa tayari katika muda wa miezi 36 ijayo,
ingawa muda huo unaweza kupungua na kubakia miezi 30.
Daraja hilo ambalo litakuwa na urefu wa mita
680 linagharimiwa kwa pamoja na Serikali na Shirika la Hifadhi ya Jamii la NSSF
ambalo litachangia kiasi cha asilimia 60 na Serikali asilimia 40.
Daraja hilo ambalo litakuwa na barabara sita za
kupitisha magari kwa wakati mmoja linajengwa na kampuni mbili za China ambazo ni
China Railway Construction Engineering Group na China Railway Major Bridge
Engineering Company na mhandisi msimamizi wa ujenzi huo ni Kampuni moja ya
Misri.
Daraja hilo linatarajiwa kupunguza adha ya
usafiri kati ya Kigamboni na Dar es Salaam ambao kwa sasa unategemea vivuko au
boti ndogo, mitumbwi ama wenye magari kulazimika kufanya mzungumo wa kilomita
52.
Kwa uamuzi wa sasa, wavuka kwa miguu ambao
watakuwa na njia maalum kwenye daraja hilo pamoja na waendesha baiskeli watavuka
bure bila malipo yoyote.
Akizungumza kwenye sherehe hiyo, Rais Kikwete
amesema kuwa Serikali haiwezi kudhulumu wananchi wake na hivyo watu wote ambao
wanastahili fidia kutokana na ujenzi wa daraja hilo na mji mpya wa Kigamboni
watalipwa haki na stahiki zao.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali yake
haitaruhusu mtu yoyote kuzuia ama kuchelewesha miradi ya maendeleo ambayo
inalenga kunufaisha watu wengi.
Rais Kikwete pia amewaonya watu ambao
wamelifanya suala la kutunga na kusema uongo kama sehemu ya utamaduni wao. “Watu
wana viwanda vya kuzalisha uongo. Wanashinda wanasambaza uongo kwenye mitandao,
kila mahali. Wamepata hata kusema kuwa mimi nimemuuzia George Bush eneo la
Kigamboni. Bush aje kufanya nini Kigamboni?”
Rais pia amesema kuwa wapo watu ambao hawapendi
maendeleo ya nchi. “Wanatamani kila siku tushindwe kuwaletea wananchi maendeleo.
Lakini watakufa kwa kihoro kwa sababu hatutashindwa. Kila tulilosema
tutalifanya, litafanyika”.
Amesema kuwa thamani kubwa ya vyama vya siasa
ni maendeleo ya wananchi. “Lakini wapo wenzetu ambao wanaudhika wakiona
maendeleo. Wanapenda hata daraja hili lisijengwe. Leo hawatalala usingizi. Kazi
ya vyama vya siasa ni kuweka maslahi yetu sote mbele.”
Comments