MAMA SALMA AWAFUNDA WANAFUNZI WA KIKE MKOANI RUKWA
Na Anna Nkinda – Sumbawanga
Watoto
wa kike nchini wametakiwa kuepukana na vishawishi vya chips Kuku,
lifti, simu za mkononi na zawadi za aina mbalimbali wanazorubuniwa nazo
kwani vitu hivyo havina nia njema ya kumkomboa msichana kielimu ,
kijamii na kiuchumi zaidi ya kumuharibia mpango mzima wa maisha yake.
Onyo
hilo limetolewa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akiongea
na wanafunzi wa kike zaidi ya 1000 kutoka shule mbalimbali za mkoa wa
Rukwa katika viwanja vya shule ya Sekondari ya wasichana ya mtakatifu
Theresia iliyopo mjini Sumbawanga.
Mama
Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo
(WAMA) alisema kwamba watoto wengi wa kike wanashindwa kumaliza masomo
na kufikia malengo kutokana na changamoto zinazowakabili ambazo nyingi
siyo za kitaaluma japo zinaathali nyingi kitaaluma , kiafya na
kimaendeleo.
“Tunafahamu
kuwa wanafunzi wengi hupata vishawishi ambavyo huwapelekea kupoteza
umakini, muelekeo na kuwa watoro, kupata ujauzito, maambukizi ya Ukimwi
na hatimaye kupoteza fursa hii adimu na adhimu ya elimu ya Sekondari na
dira ya maisha yao. Ni muhimu kujidhatiti na kujiepusha na mitego,
vishawishi na matendo yanayoweza kusababisha matatizo haya.
Msikubali vishawishi kwani peremende ya dakika si sawa na asali ya maisha.
Iweje
uridhie kuuharibu mpango wa maisha yakokwa kitu cha mara moja? Licha tu
ya kuwa atakayehusika na kosa la kukupa mimba anapaswa kushtakiwa
kisheria, lakini kwako wewe ni hatari kiafya kwani kushika mimba ukiwa
na umri mdogo unahatarisha maisha yako wakati wa kujifungua.
Asilimia ishirini ya vifo vya akina mama wajawazito hutokana na uzazi katika umri mdogo”, alisema Mama Kikwete.
Aidha
Mama Kikwepi pia aliwataka wanafunzi hao kuwatii wazazi wao,kusoma kwa
bidii na kujiamini kwamba wanaweza kwani chochote anachoweza kufanya
mtoto wa kiume kitaaluma na halikadhalika mtoto wa kike anaweza
kukifanya hivyo basi wasome zaidi masomo ya sayansi na hisabati kama
watoto wa kiume.
Akisoma
taarifa ya shule ya Sekondari ya wasichana ya Mtakatifu Theresia Sr.
Beatrice Cromweli ambaye ni mwalimu alisema kuwa shule hiyo ilianzishwa
na shirika la masista wa Maria Mtakatifu Malkia wa Afrika Jimbo la
Sumbawanga mwaka 2007 ikiwa na wanafunzi 85 na hadi sasa kuna wanafunzi
489 na walimu 16.
Alisema
kuwa lengo kuu la kuanzishwa kwa shule hiyo ni kuwaendeleza watoto wa
kike kielimu na kimaadili ili kuwakomboa katika unyanyasaji dhidi ya
mwanamke na hivyo kuwapa uwezo wa kujitambua, kujiamini na kufanya
maamuzi sahihi katika maisha yao.
Sr.
Cromweli alisema,“Shule yetu imefanikiwa kuongeza idadi ya wanafunzi
kila mwaka hii hutokana na ongezeko la vyumba vya madarasa, mabweni ya
kulala, vifaa vya kufundishia, walimu na vitendea kazi mbalimbali na
ufaulu mzuri wa wanafunzi katika mitihani ya kidato cha nne”.
Alizitaja
changamoto zinazowakabili kuwa ni ukosefu wa vifaa vya maktaba ya
kisasa kwani ujenzi wa jengo hilo ambalo halijaanza kutumika
kikamilifu kutokana na ukosefu wa vitabu, meza, viti na kompyuta
umeshakamilika, jengo la bwalo la chakula na ukumbi wa mikutano bado
halijakamilika kwani halina meza na viti na uhaba wa vifaa vya maabara
ambavyo vinawafanya wanafunzi kutofanya majaribio ya kuridhisha.
Mkoa
wa Rukwa umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya kushuka kwa kiwango cha
elimu hasa kwa mtoto wa kike , karibu asilimia 39 ya watoto hao huacha
shule kabla ya kumaliza elimu ya Sekondari kutokana na tatizo la utoro,
ujauzito na wazazi kutotilia maanani suala la elimu.
Comments