Sehemu ya barabara pamoja na Daraja la Kikwete kama inavyoonekana hivi sasa baada ya kukamilika kwa ujenzi wake.
Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli
(Katikati) akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Kanali Msataafu Issa Machibya
(kulia) pamoja na Watendaji mbali mbali wakikagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja
la Kikwete katika Mto Malagarasi mkoani Kigoma.
Waziri
wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli (Katikati) akiongozana na Mkuu
wa Mkoa wa Kigoma Kanali Msataafu Issa Machibya (wa pili kulia) na Naibu
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Eng. Joseph Nyamhanga (kulia) wakipita
kwa pamoja na Watendaji mbali mbali katika Daraja la Kikwete.
----
Ujenzi
wa Daraja la Kikwete katika mto Malagarasi mkoani Kigoma umekamilika.
Waziri wa Ujenzi Mheshimiwa Dkt John Pombe Magufuli akiwa katika ziara
ya kikazi mkoani Kigoma aliweza kutembelea eneo hilo na kujionea magari
yakiwa yanapita katika daraja hilo.
Kampuni
ya M/S Hanil Engineering and Construction Company Limited kutoka Korea
ya Kusini iliingia mkataba na kuanza ujenzi wa daraja hilo mwezi Desemba
2010 na kutakiwa kukamilisha kazi hiyo ifikapo mwezi Desemba 2013.
Mradi huo unajumuisha ujenzi wa madaraja matatu yenye jumla ya urefu wa
meta 275 pamoja na barabara ya lami yenye urefu wa kilometa 48 kwa
gharama ya Dola za Kimarekani milioni 64 ambazo ni sawa na Shilingi
bilioni 90 za Kitanzania zilizotolewa na Benki ya Exim ya Korea ya
Kusini kwa asilimia 90 na kiasi kilichobaki kikiwa ni fedha za ndani.
Akitoa
maelezo ya mradi huo Mhandisi Yu Sing kutoka kampuni ya Hanil
Engineering alimfahamisha Waziri Magufuli kuwa, Mradi huo umegawanywa
katika sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ambayo ndiyo iliyokamilika ni
ujenzi wa madaraja matatu yenye urefu wa meta 25, meta 200 na meta 50
pamoja na kilometa 11 za lami. Sehemu ya pili ni ujenzi wa kilometa 37
za lami ambazo ndizo zinazoendelea kukamilishwa kwa sasa.
Baada
ya kutembelea eneo hilo la mradi, Mheshimiwa Magufuli alielezea
kuridhishwa kwake na utendaji wa mkandarasi huyo kutokana na kukamilisha
ujenzi wa sehemu hiyo ya kwanza kwa mujibu wa mkataba na kwa viwango
vya hali ya juu. “Nimeridhishwa na utendaji wa mkandarasi huyu na hasa
kwa jinsi alivyoweza kumaliza sehemu hii ya kwanza kwa muda mzuri na
viwango vya hali ya juu” alibainisha Mheshimiwa Magufuli.
Kwa
muda mrefu usafiri katika eneo hilo ulikuwa ni kikwazo kikubwa kwa
maendeleo ya mkoa wa Kigoma hasa nyakati za mvua kutokana na kukosekana
kwa daraja la uhakika. Kwa hivi sasa kumenza kuonekana ongezeko kubwa la
magari kati Manyoni – Itingi – Tabora hadi Kigoma kupitia katika Daraja
hilo la Kikwete hali ambayo awali ililazimu kupitia barabara ya Manyoni
– Singida - Nzega – Kahama – Nyakanazi – Kibondo – Kasulu hadi Kigoma.
Naye
Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Kanali Mstaafu Issa Machibya aliyeambatana na
Waziri wa Ujenzi katika ziara hiyo, aliishikuru Serikali kupitia Wizara
ya Ujenzi kwa niaba ya Wananchi wa Kigoma kwa kutimiza ahadi ambayo
imekuwa ikisuburiwa kwa muda mrefu.
“Kukamilika
kwa mradi huu pamoja na mingine mingine ambayo inaendelea kujengwa
katika barabara ya Kigoma kuelekea Tabora hadi Manyoni mkoani Singida,
ni ufumbuzi mkubwa wa matatizo yaliyokuwa yakikwamisha maendeleo katika
ukanda huu wa magharibi, hii ni fursa ya pekee kwa amendeleo ya ukanda
huu wa Maharibi” alimalizia Mhe. Machibya.
Comments