Emmanuel Okwi kulia akisaini Mkataba wa kuendelea kuichezea Simba SC, huku akishuhudiwa na Rais wa klabu hiyo, Evans Aveva |
MSHAMBULIAJI
Mganda, Emmanuel Arnold Okwi leo amesaini Mkataba mpya na Simba wa
miaka miwili, huku ule wa awali wa miezi sita ukielekea ukingoni.
Mwenyekiti
wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe ameiambia BIN
ZUBEIRY leo kwamba, wameamua kumuongezea Mkataba Okwi baada ya kuvutiwa
na huduma zake.
Okwi amerejea Simba SC Agosti mwaka huu, baada ya kutemwa na Yanga SC iliyomsajili kutoka Etoile du Sahel ya Tunisia.
Okwi
alijiunga na Etoile kwa dau la dola 300,000 za Kimarekani zaidi ya Sh.
Milioni 500 akitokea Simba SC Januari mwaka jana, lakini kufika Mei
akatibuana na klabu hiyo.Klabu ilidai Okwi alipewa ruhusa ya
kwenda kuchezea timu yake ya taifa, The Cranes akachelewa kurudi zaidi
ya mwezi mzima, wakati mchezaji akadai alikuwa halipiwi mishahara.
Okwi
na Etoile wakafunguliana kesi Shirikisho la Soka la Kimataia (FIFA) na
mchezaji huyo wa Uganda akaomba aruhusiwe kuchezea timu nyingine
kunusuru kipaji chake wakati sakata hilo linaendelea.
FIFA
ikatoa ruhusa hiyo na Okwi akajiunga na klabu yake ya zamani, SC Villa
ya Uganda lakini baada ya miezi sita, akasajiliwa na Yanga SC kwa
Mkataba wa miaka miwili na nusu Desemba mwaka jana.
Hata
hivyo, kufika Machi mwaka huu, Okwi akatibuana na Yanga SC na kuamua
kuomba kurejea klabu yake, Simba SC ambako alifanikiwa. Yanga SC
walifungua kesi TFF kupinga, lakini mshambuliaji huyo wa Uganda
akawagaragaza na kupewa ridhaa ya kuendelea na kazi Simba SC, ambako
alipewa Mkataba wa miezi sita.
Na baada
ya kuionzoza timu hiyo kama Nahodha kushinda mbili 2-0 dhidi ya mahasimu
Yanga SC, katika mchezo wa Nani Mtani Jembe Jumamosi, Uwanja wa Taifa,
Dar es Salaam, Okwi leo amepewa Mkataba mpya ambao umemfanya avune
mamilioni kibao, siri yao Simba na yeye mwenywe
Comments