Jengo jipya la Kitega Uchumi la NSSF Moshi, lililozinduliwa na Rais Jakaya Kikwete Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete,Waziri wa Kazi na ajira Mh.Gaudensia Kabaka(watano kushoto) Mkurugenzi Mkuu wa NSSF Dkt.Ramadhani Dau(wapili kulia), Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama(wapili kushoto) pamoja na viongozi na wadau wengine wakikata utepe kufungua rasmi jengo la kitega uchumi la NSSF Kilimanjaro Commercial Complex mjini Moshi,Mkoani Kilimanjaro leo. Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiagana na mkurugenzi Mkuu wa NSSF Dkt.Ramadhani Dau baada ya hafla ya ufunguzi wa jengo jipya la kitega uchumi la NSSF mjini Moshi leo.Katikati ni Waziri wa Kazi na Ajira Mh.Gaudensia Kabaka Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akikagua jengo la upasuaji katika hospitali ya rufaa ya Mawenzi mjini Moshi Mkoani Kilimanjaro muda mfupi baada ya kulifungua leo.Kulia ni Naibu Waziri wa Afya Dkt.Steven Kebwe. Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wauguzi wa hospitali ya rufaa ya Mawenzi mjini Moshi muda mfupi baada ya kufungua jengo la upasuaji na kuweka jiwe la msingi kuzindua ujenzi wa wodi ya mama na watoto katika hospitali hiyo leo.(wanne kulia ni Naibu waziri wa Afya Dkt.Steven Kebwe,wanne kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama,Kushoto ni Mbunge wa Vunjo Agustino Lyatonga Mrema,na wapili kushoto ni Mbunge wa Moshi Vijijini Dkt.Cyril Chami. Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete, Mkurugenzi Mkuu wa NSSF Dkt.Ramadhan Dau pamoja na wadau wengine wakitazama ramani ya jengo jipya la kitega uchumi la NSSF mjini Moshi Kilimanjaro Commercial Complex wakati wa hafla ya ufunguzi leo. Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na chipikizi wa Tanzania Girl Guides wakati wa hafla ya ufunguzi wa jengo la kitega uchumi la NSSF mjini Moshi leo.Tanzania Girl Guides,UMATI,Tanzania Red Cross ni wadau wa NSSF katika mradi huo. |
|
a.
|
Uongozi siyo kujisifu – Rais
Kikwete
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amesema
kuwa uongozi siyo kujisifu na kujisifia tu bali ni kutenda vitendo na kufanya
maamuzi yanayothibitisha na yanayolingana na sifa hizo.
Rais
Kikwete ameyasema hayo, Jumanne, Februari 10, 2015, wakati alipofungua jengo la
kisasa kabisa la kitega uchumi lenye thamani ya sh. bilioni 64 kwenye Manispaa
ya Moshi katika siku yake ya kwanza ya ziara ya siku mbili ya kikazi Mkoani
Kilimanjaro.
Jengo
hilo linalojulikana kama Kilimanjaro
Commercial Complex na lililoko katikati ya Manispaa ya Moshi limejengwa kwa
ubia wa Shirika la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii la NSSF, taasisi ya Girls Guide Tanzania, taasisi ya Red Cross na Chama cha Uzazi na Malezi Bora Tanzania (UMATI) na
ndilo jengo kubwa kuliko yote katika manispaa hiyo.
Amelisifia
uongozi na visheni ya maamuzi ya NSSF akisisitiza kuwa shirika hilo
limethibitisha kwa vitendo sifa ambazo shirika hilo linazo na zimethibishwa. “Uongozi
siyo kujisifia na kujisifu tu bali ni kutenda vitendo na kufanya maamuzi
yanayothibisha na kulingana na sifa hizo na katika hilo NSSF imeonyesha njia.”
Jengo
hilo ambalo ujenzi wake ulianza Desemba 2011 na kuchukua miaka mitatu
limejengwa kwa pamoja na Kampuni ya Group Six International ya China na Advent
Construction ya hapa nchini na litakuwa na maduka makubwa na madogo, maofisi,
mabenki na kumbi za mikutano.
Akizungumza
katika shughuli hiyo iliyohudhuriwa na mamia ya wananchi na viongozi wa taasisi
zilizoko katika ubia wa ujenzi wa Jengo hilo, Waziri wa Kazi na Ajira,
Mheshimiwa Gaudencia Kabaka amesema kuwa ni muhimu kwa NSSF kuendelea kuwekeza
katika miradi ya kimkakati na inayolipa, badala ya fedha hizo kubakia kwenye
mabenki tu ambako zinaweza kukumbwa na athari za mfumuko wa bei.
Mapema,
Rais Kikwete katika shughuli yake ya kwanza baada ya kuwasili Mkoani
Kilimanjaro, alifungua wodi ya upasuaji na kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi
wa jengo la wodi ya akinamama na mtoto katika Hospitali ya Mkoa ya Mawezi
katikati ya Manispaa ya Moshi. Mawenzi ni moja ya hospitali kongwe zaidi nchini
ikiwa imeanzishwa mwaka 1920
Akizungumza
kabla ya kufanya shughuli hizo mbili kubwa, Rais Kikwete ameelezea mafanikio
makubwa yaliyopatikana katika utekelezaji wa Sera ya Afrika ya mwaka 2007
iliyochukua nafasi ya sera ya mwaka 1997, ikiwa ni pamoja na kujenga maabara za
kisasa katika kila hospitali ya Mkoa nchini na kuzifanya hospitali hizo kuwa za
rufani ndani ya mikoa.
Rais
Kikwete pia ameelezea jitihada za Serikali kupambana na magonjwa mbali mbali
ikiwemo malaria na ukimwi na juhudi za kupunguza vifo vya watoto na akinamama
kwa sababu ambazo zinazuilika.
Aidha,
Rais amefafanua hatua zilizochukuliwa na Serikali yake kuongeza idadi ya
madaktari na watumishi wengine wa sekta ya afya ambazo ni pamoja na ujenzi wa
vyuo vya kufundishia madaktari katika hospitali mbili kubwa na mpya za
Mlongazila na ile ya Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na upanuzi wa Chuo Kikuu cha
Tiba cha Muhas cha Dar es Salaam.
Rais
Kikwete pia amezungumzia matatizo ya kudumaa kwa watoto wadogo nchini akisema
kuwa matunzo na lishe ya watoto wadogo katika siku 1,000 za kwanza za maisha
yake ni muhimu sana katika maisha ya baadaye ya watoto.
Amesema
kuwa kwa watoto wadogo lishe duni inasababisha kudumaa kwa watoto, watoto kuwa
na kimo kidogo kuliko umri wao, watoto kuwa na uzito mdogo kulinganisha na umri
wao, watoto kuwa na upungufu wa madini joto na upungufu wa vitamin A.
Rais
Kikwete ataondoka kesho kurejea Dar es Salaam baada ya kumaliza ziara hiyo.
Imetolewa na;
Kurugenzi
ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
10
Februari, 2015
Comments